Wednesday, December 4, 2019

UWEZEKANO WA KUTOKEA VIMBUNGA PACHA BAHARI YA HINDI


Dar es Salaam, 04 Disemba 2019:
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inatoa taarifa ya uwezekano wa kutokea kwa vimbunga pacha magharibi mwa Bahari ya Hindi upande wa kaskazini na kusini mwa Ikweta na hivyo kuwa na uwezekano wa kuathiri mifumo ya hali ya hewa nchini.

Migandamizo hiyo midogo pacha inaelekea kuimarika na kuwa vimbunga katika Pwani ya Somalia (Upande wa Kaskazini mwa Ikweta ) na Kaskazini Mashariki mwa Kisiwa cha Madagascar (Kusini mwa Ikweta).


Aidha, mgandamizo mdogo wa hewa uliopo kusini magharibi mwa bahari ya Hindi (karibu na kisiwa cha Madagascar) unatarajiwa kuimarika na kuelekea kaskazini mwa kisiwa cha Madagascar, na hivyo unatarajiwa kusababisha ongezeko la mvua pamoja na vipindi vya mvua kubwa hususan katika baadhi ya maeneo ya Pwani ya Kaskazini ya nchi yetu kati ya terehe 5 na 6 Disemba 2019.


Mamlaka imeendelea kutoa tahadhari ya vipindi vifupi vya mvua kubwa kwa baadhi ya maeneo ya mikoa ya Dar es salaam na Pwani na angalizo la mvua kubwa kwa baadhi ya maeneo ya mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Mara, Tanga pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba, Rukwa, Mbeya, Songwe, Iringa, Njombe na Ruvuma.


Kwa upande mwingine, mgandamizo mdogo wa hewa katika pwani ya Somalia unatarajiwa kuendelea kuwa mbali na pwani ya Tanzania na hautarajiwi kuwa na madhara katika nchi yetu.


USHAURI: Wananchi wanashauriwa kuendelea kufuatilia taarifa za utabiri kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania na kuzingatia tahadhari zitakazotolewa na mirejeo yake pamoja na kupata na kuzingatia ushauri na miongozo ya wataalam katika sekta husika ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.


Mamlaka ya hali ya hewa Tanzania inaendelea kufuatilia hali hiyo katika bahari ya Hindi pamoja na mwenendo wa mifumo ya hali ya hewa kwa ujumla na itatoa taarifa za mrejeo kila itakapobidi.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...