Tuesday, September 13, 2022

SATELAITI KUENDELEA KUBORESHA TAARIFA ZA HALI YA HEWA.


 




Dar es Salaam; Tarehe 13 Septemba, 2022;

Serikali imewahakikishia wadau wa hali ya hewa nchini kuwa itaendelea kuboresha miundombinu na watalaam wake ili kuhakikisha usahihi wa taarifa za hali ya hewa unaongezeka na kusaidia kwenye maendeleo na ukuaji wa uchumi.

 

Akizungumza wakati wa kufungua rasmi Kongamano la 15 la Wadau wa  Satelaiti za Hali ya Hewa wa Shirika la EUMETSAT  Barani Afrika, katika Ukumbi wa Mikutano wa Julius Nyerere, Dar es Salaam,Naibu Waziri wa Uchukuzi, Mhe. Atupele Fred Mwakibete (MB) ambaye alimuwakilisha Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mhe. Kassim Majaliwa, amesema kuwa masuala ya hali ya hewa ni mtambuka na yanagusa sekta zote hivyo kongamano hilo litakuwa muarobaini wa changamoto zinazokabili sekta hizo.

 

“Kwa namna ya pekee niwashukuru EUMETSAT kwa kuamua kufanyia Mkutano huu wa kimataifa nchini Tanzania, ni imani yangu kuwa siku hizi nne (4) mtachakata changamoto zote na kuja na suluhu ili sekta zote zipate ahueni katika utekelezaji wa mipango yake kwani taarifa za hali ya hewa ni muhimu sana” amesema Naibu Waziri Mwakibete.

 

Naibu Waziri Mwakibete aliendelea kwa kusema kupitia teknolojia ya satelaiti, huduma za hali ya hewa zinaendelea kuboreshwa na hivyo kuchangia katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa yanayoikumba Afrika na Dunia kwa ujumla. Aidha, ameitaka Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini (TMA) kuendelea kutumia njia mbalimbali kuifikishia jamii taarifa za hali ya hewa kwa wakati.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt Agnes Kijazi amesema Kongamano hilo litajadili kwa pamoja changamoto mbalimbali na kuja na mikakati mahususi ya kuhakikisha taarifa za hali zinapatikana kwa urahisi na kwa haraka sambamba na kukidhi matakwa ya watumiaji wa taarifa hizo. Vile vile, alieleza kuwa Tanzania kuwa mwenyeji wa Kongamano hili ni heshima kubwa kwa nchi na kuonesha mafanikio makubwa katika sekta ya hali ya hewa nchini pamoja na ushirikiano ulipo baina ya nchi za Afrika na nje ya Afrika.

 

“Kupitia makongamano haya nchi za Afrika zimeendelea kunufaika na uboreshaji wa utabiri wa hali ya hewa na hivyo kuchangia katika kupanga mipango ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii”. Alisema Dkt. Kijazi

 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la EUMETSAT, Dkt. Phil Evans amesema mipango ya shirika hilo ni kurusha satelaiti ya kisasa zaidi (Meteosat third Generation – MTG) mwishoni mwa mwaka huu ili kuboresha uangazi na utoaji wa taarifa za hali ya hewa hususani katika ukanda wa Afrika.

 

Kongamano la 15 la Wadau wa Satelaiti za Hali ya Hewa wa Shirika la EUMETSAT barani Afrika linalofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 12 hadi 16 Septemba 2022, limewakutanisha Wadau wa Masuala ya Hali ya hewa kutoka nchi 59 Barani Afrika na nje ya Afrika wakiwemo Wakurugenzi wa Mamlaka za Hali ya Hewa katika Nchi za Afrika, Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) na Umoja wa Ulaya (EU).

 

EUMETSAT ni miongoni mwa Taasisi za kimataifa zinazoshirikiana na WMO katika shughuli za uangazi wa hali ya hewa kwa kutumia teknolojia ya satelaiti za hali ya hewa kwa nchi wanachama wa WMO.

 


Friday, September 2, 2022

VULI 2022: MVUA ZA CHINI YA WASTANI HADI WASTANI ZINATARAJIWA KATIKA MAENEO MENGI YA NCHI.


 


Dar es Salaam; Tarehe 2 Septemba, 2022;

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Vuli 2022 kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka. Akizungumza wakati wa mkutano na vyombo vya habari katika Makao Makuu ya TMA, Ubungo Plaza, Tarehe 2/9/2022, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi alisema maeneo ya nchi yanayopata misimu miwili ya mvua yanatarajiwa kupata mvua za chini ya wastani hadi wastani.

Kutokana na mifumo ya hali ya hewa ilivyo kwa sasa na inavyotarajiwa katika kipindi chote cha msimu, kwa ujumla mvua za chini ya wastani hadi wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya nchi yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka. Msimu unatarajiwa kuanza kwa kuchelewa na kuambatana na mtawanyiko wa mvua usioridhisha. Vipindi virefu zaidi vya ukavu vinatarajiwa katika miezi ya Oktoba na Novemba 2022, hata hivyo vipindi vya ongezeko kidogo la mvua vinatarajiwa kujitokeza katika maeneo machache hususan wiki ya tatu na ya nne mwezi Disemba, 2022. Kwa kawaida msimu wa mvua za Vuli huisha mwezi Disemba. Hata hivyo, kunatarajiwa kuwepo na muendelezo wa mvua kwa mwezi Januari, 2023”. Alieleza Dkt Kijazi

 Vilevile Dkt. Kijazi alisema kuwa matarajio ya Vipindi vya joto kali kuliko kawaida katika msimu wa Vuli vinatarajiwa.  Pamoja na matarajio ya   mvua za chini ya wastani hadi wastani, ongezeko la joto linatarajiwa katika msimu wa Vuli hususani katika Maeneo ya kaskazini mwa mkoa wa Morogoro, mikoa ya Pwani (ikijumuisha visiwa vya Mafia), Dar es Salaam, Tanga pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba) na Mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro” Alisema Dkt Kijazi.

Taarifa hiyo pia imetoa angalizo la mvua kubwa kwa baadhi ya maeneo nchini. “Ingawa maeneo mengi yanatarajiwa kupata mvua za chini ya wastani hadi wastani, izingatiwe kuwa matukio ya vipindi vifupi vya mvua kubwa yanaweza yakajitokeza katika maeneo machache, watumiaji wa taarifa za utabiri huu wanashauriwa pia kufuatilia utabiri wa saa 24, siku 10 pamoja na mwezi kama unavyotolewa na Mamlaka ya hali ya Hewa Tanzania.” Alizungumza Dkt Kijazi

 

Akimaliza kutoa taarifa hiyo, Dkt. Kijazi alisema, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania itaendelea kufuatilia mwenendo wa mifumo ya hali ya hewa na kutoa mirejesho ya mwelekeo wa mvua nchini kadri inavyohitajika. Aidha, wadau wanashauriwa kuwasiliana na Mamlaka ili kupata taarifa mahsusi za utabiri wa msimu ili kukidhi mahitaji maalum katika sekta zao.

Thursday, September 1, 2022

DKT KIJAZI AWAHIMIZA WANAHABARI KUTOA UTABIRI ULIOSAHIHI KWA JAMII.

 

Mgeni rasmi na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Dkt Agnes Kijazi, Akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa wanahabari  wa Utabiri wa Mvua za Vuli 2022 katika Ukumbi wa TARI, Kibaha, Tarehe 31/08/2022.

Kaimu Mkurugenzi wa kituo kikuu cha utabiri cha TMA Dkt. Mafur Kantamla akiongea na wanahabari katika Mkutano wa wanahabari  wa Utabiri wa Mvua za Vuli 2022 katika Ukumbi wa TARI, Kibaha, Tarehe 31/08/2022

 

 Meneja Mitambo na miundombinu  wa TMA  Ndugu. Samwel Mbuya akiongea na wanahabari katika Mkutano wa wanahabari  wa Utabiri wa Mvua za Vuli 2022 katika Ukumbi wa TARI, Kibaha, Tarehe 31/08/2022.







Matukio katika picha wakati waandishi wakisikiliza mada mbalimbali zilizowasilishwa katika Mkutano wa wanahabari  wa Utabiri wa Mvua za Vuli 2022 katika Ukumbi wa TARI, Kibaha, Tarehe 31/08/2022. 

Waandishi kutoka vyombo mbalimbali katika picha ya pamoja na mgeni rasmi katika katika Mkutano wa wanahabari  wa Utabiri wa Mvua za Vuli 2022 katika Ukumbi wa TARI, Kibaha, Tarehe 31/08/2022. Utabiri huo unatarajiwa kutolewa rasmi Tarehe 02 Septemba,2022 katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya tatu, Ubungo Plaza - Dar es Salaam, Tanzania.

 

Tarehe 31 Agosti, 2022; Kibaha

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Dkt Agnes Kijazi, amewataka wanahabari kutoa taarifa za hali ya hewa kwa jamii zilizosahihi  haswa kwa maeneo ya ziada ya kisekta kutoka kwa wataalamu ili taarifa iweze kuifikia jamii kwa ukamilifu. Aliyasema hayo wakati akifungua rasmi Mkutano wa wanahabari  wa Utabiri wa Mvua za Vuli 2022 katika Ukumbi wa TARI, Kibaha, Tarehe 31/08/2022.

“Napenda kuwakumbusha kufikisha taarifa hizi kwa usahihi na kutafuta, kupata na kuwasilisha ufafanuzi na maeneo ya ziada ya kisekta kutoka kwa wataalamu ili taarifa iweze kuifikia jamii kwa ukamilifu”. Alisema Dkt. Kijazi

Dkt.Kijazi alisema kuwa taarifa  za hali ya hewa zilizo sahihi na za uhakika zitaisaidia jamii kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa. Pia zitazisaidia Mamlaka zinazohusika kupanga mipango ya kukabiliana na majanga yatokanayo na hali mbaya ya hewa, upatikanaji wa chakula na lishe bora pamoja na afya kwa ustawi wa jamii na hivyo kuchangia katika maendeleo endelevu.

Aidha, wakati akiendelea kusema hayo, aliongezea kuwa kupatikana kwa utabiri wa msimu wa Vuli 2022 kwa usahihi na kwa wakati kutachangia katika jitihada za seriakali ya awamu ya sita katika kukuza uchumi wa mwananchi mmoja mmoja, nchi kwa ujumla pamoja na kuboresha miundombinu na huduma za kijamii hapa nchini.

Kwa upande wake David Gumbo, mwandishi kutoka EATV akizungumza kwa niaba ya waandishi aliipongeza Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kwa kutoa ushirikiano mzuri kwa vyombo vya habari ambao umesaidia kutoa taarifa za hali ya hewa zilizo sahihi na kwa wakati kwa jamii.

Katika Mkutano huo, wahabari  walipata fursa ya kuona rasimu ya utabiri wa hali ya hewa katika kipindi cha mwezi Oktoba hadi Desemba 2022  na kujadili na kupata uelewa wa pamoja ili kurahisisha uwasilishwaji wa utabiri huu kwa jamii kwa ufanisi na katika lugha inayoeleweka kirahisi pindi utakapotolewa rasmi Tarehe 02 Septemba,2022.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...