Thursday, February 18, 2021

MASIKA 2021: MAENEO MENGI KUPATA MVUA ZA WASTANI.



Dar es Salaam, Tarehe 18/02/2021

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2021 kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka ikiwa ni mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro, Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani ikijumuisha kisiwa cha Mafia, Tanga na maeneo ya kaskazini mwa mkoa wa Morogoro pamoja na  visiwa vya Unguja na Pemba, Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Mara  pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma.

 

Akizungumzia utabiri huo Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri wa TMA, Dkt. Hamza Kabelwa kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Agnes Kijazi, alisema utabiri unaonesha mvua zitakuwa za wastani kwa maeneo mengi na uwepo wa mvua za juu ya wastani na chini ya wastani katika vipindi tofauti tofuati wakati wa msimu.

 

“Mvua za Masika zinatarajiwa kuwa za wastani hadi juu ya wastani katika maeneo mengi ya mikoa ya Arusha, Manyara, Kilimanjaro, Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Mara pamoja na maeneo ya kaskazini mwa mkoa wa Kigoma (wilaya za Kakonko na Kibondo). Aidha, mvua za wastani hadi chini ya wastani zinatarajiwa katika maeneo ya kaskazini mwa mkoa wa Morogoro, mikoa ya Pwani (ikijumuisha visiwa vya Mafia), Dar es Salaam, Tanga pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba”. Alisema Dkt. Kabelwa.

 

Aliendelea kwa kueleza kuwa mvua za Masika zinatarajiwa kuanza mapema katika wiki ya nne ya mwezi Februari, 2021 hususan katika maeneo ya nyanda za juu kaskazini mashariki na pwani ya kaskazini na vipindi vya ukavu vinatarajiwa kujitokeza hususan katika mwezi Mei, 2021. Hivyo, unyevunyevu wa kutosha kwenye udongo unatarajiwa kuimarisha uzalishaji wa mazao mbalimbali ukiwemo mpunga na uwepo wa malisho na maji ya kutosha kwa ajili ya mifugo na wanyamapori unatarajiwa kupunguza migogoro baina ya wanyama na binadamu

Akizungumzia athari zinazoweza kujitokeza, Dkt. Kabelwa alisema vipindi vifupi vya mvua kubwa vinaweza kujitokeza na kuambatana na mafuriko, hivyo jamii inashauriwa kufuatilia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa mara kwa mara na kuchukua hatua stahiki ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza kama vile uharibifu wa miundombinu, shughuli za kijamii kuathirika, upotevu wa maisha na mali.

 

 Kwa taarifa zaidi tembelea tovuti yetu www.meteo.go.tz

 

Tuesday, February 16, 2021

WADAU WATAKIWA KUTUMIA TAARIFA ZA HALI YA HEWA KUKABILIANA NA MABADILIKO YA HALI YA HEWA.




Mgeni rasmi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya TMA Dkt. Buruhani Nyenzi akizungumza kwa kusisitiza wakati akifungua warsha ya wadau ya kujadili utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2021 unaotarajiwa kutolewa rasmi Tarehe 18 februari, 2021 katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya tatu, Ubungo Plaza - Dar es Salaam, Tanzania


Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi  akifafanua jambo kwa wadau katika warsha ya kujadili utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2021 unaotarajiwa kutolewa rasmi Tarehe 18 februari 2021 katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya tatu, Ubungo Plaza - Dar es Salaam, Tanzania


Wadau kutoka sekta mbalimbali katika picha ya pamoja na mgeni rasmi kwenye warsha ya wadau ya kujadili utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2021 unaotarajiwa kutolewa rasmi Tarehe 18 februari, 2021 katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya tatu, Ubungo Plaza - Dar es Salaam, Tanzania




Matukio katika picha wakati wadau wakifuatilia mada mbalimbali zilizowasilishwa katika warsha ya wadau ya kujadili utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2021 unaotarajiwa kutolewa rasmi Tarehe 18 februari, 2021 katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya tatu, Ubungo Plaza - Dar es Salaam, Tanzania







Wadau kutoka sekta mbalimbali wakiwasilisha athari na ushauri katika sekta zao kwenye warsha ya wadau ya kujadili utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2021 unaotarajiwa kutolewa rasmi Tarehe 18 februari, 2021 katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya tatu, Ubungo Plaza - Dar es Salaam, Tanzania





 Dar es Salaam; Tarehe 15 - 16 Februari, 2021;

Wadau wa hali ya hewa kutoka sekta mbalimbali wametakiwa kutumia taarifa za hali ya hewa ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi. Hayo yalizungumzwa na Mgeni Rasmi na Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Buruhani Nyenzi, wakati akifungua Mkutano wa Wadau wa Utabiri wa Mvua za Msimu wa Masika (Machi -Mei 2021), uliofanyika katika Ukumbi wa Taasisi ya Mafunzo ya Uanasheria kwa Vitendo Tanzania (The Law School of Tanzania), Dar es Salaam.

Nichuke fursa hii kuwasihi wadau wote wa hali ya hewa katika sekta mbalimbali kujihusisha zaidi katika kuelewa na kufuatilia masuala ya hali ya hewa na mabadiliko yake ili kuweza kuchukua hatua stahiki za kujikinga na kukabiliana na athari zitokanazo na mabadiliko ya hali ya hewa. Kwa kufanya hivyo tutasababisha mazingira tunayoishi yaendelee kubaki salama na kuwa katika asili yake na yenye kuvutia kwa shughuli za kiuchumi na kijamii kwa kizazi hiki na vizazi vijavyo”. Alizungumza Dkt. Nyenzi.

Aidha, Dkt. Nyenzi aliendelea kwa kusema kuwa ni jukumu letu kuendelea kuelimishana kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa na namna ya kukabiliana nayo na wakati huo huo tukiendelea kutekeleza sera na mikakati ambayo itatusaidia kutumia vyema huduma za hali ya hewa katika kuinua uchumi wa nchi yetu, kutoka uchumi wa kati tuliofikia sasa kwenda uchumi wa juu zaidi.

Mabadiliko ya tabia nchi  ni halisi ambapo tumeshuhudia athari mbalimbali zinazotokana na mabadiliko haya ikiwa ni pamoja na kuwa na vipindi vya mvua kubwa, kubadilika kwa misimu ya mvua hasa tarehe za kuanza na kuisha kwa mvua, wote tumeshuhudia mvua zilizo nje ya msimu kwa mwaka huu wa 2021 katika maeneo ambayo kwa kawaida huwa ni makavu kwa miezi ya Januari na Februari, hali hii inasababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa (climate change)”. Alifafanua Dkt. Nyenzi.

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi alieleza kuwa mkutano huo unalenga kujadiliana na kupata maoni ya wadau jinsi utabiri wa mvua za Masika utakavyoweza kutumika kwa tija katika sekta mbalimbali hapa nchini na hivyo kuendeleza na kuimarisha utoaji wa huduma za hali ya hewa na matumizi yake kwa jamii. 

“Ipo haja ya kutambua uwezo wa utabiri wa hali ya hewa na  hususan utabiri wa msimu kama zana yenye nguvu katika  kusaidia watoa maamuzi kukabiliana na changamoto zinazosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa. Kaulimbiu ya mwaka huu ni “Tumia taarifa za utabiri kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa”. Alisema Dkt. Kijazi.

Dkt. Kijazi aliishukuru Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa jitihada za kuboresha miundombinu na huduma za hali ya hewa hapa nchini na kufanya huduma zinazotolewa na TMA kuendelea kuwa bora na kukidhi viwango vya kimataifa.

Kwa upande wake, mdau kutoka Wizara ya Kilimo Bw. Robert Dimoso alisema katika kipindi cha msimu wa mvua za vuli ulioanza oktoba mpaka Disemba 2020, maeneo mengi yalipata mvua za chini ya wastani hivyo kupelekea kupata unyevunyevu mzuri kwenye udongo ambao ulisaidia kustawi vizuri kwa mazao, hata hivyo kuna maeneo machache yalipata mvua za juu ya wastani hasa mikoa ya kanda ya ziwa ambayo ilichangia kuharibika kwa zao la maharage, lakini kwa ujumla utabiri uliendana na uhalisia kama ulivyotabiriwa.

Naye, mdau kutoka sekta ya Makazi Mijini Bw. Tim Ndezi alitoa pongezi zilizotolewa na wakazi wanaoishi katika makazi holela akisema wakazi hao wamefurahishwa sana na utabiri uliotolewa katika msimu uliopita kwani umekuwa sahihi sana na hata idadi ya watu wanaoathirika na mafuriko katika msimu uliopita imekuwa ni kidogo sana kama rekodi zinavyoonesha kwasababu watu walipata taarifa mapema na kuchukuwa tahadhari.

Bw. Simon Kadogosa kutoka Redcross alisema utabiri uliwasaidia katika kuboresha akiba ya vifaa vya uokozi na vilevile ulichangia katika kufanikisha  miradi mbalimbali ambayo inafanyika kwa ushirikiano na Ofisi ya Waziri Mkuu hususan kwenye mikoa ya Iringa, Songwe na Arusha.





Tuesday, February 9, 2021

DKT. KIJAZI AONGOZA MKUTANO WA KUJADILI VIPAUMBELE KATIKA MPANGO MKAKATI WA WMO WA KUJENGA UWEZO.

 

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi akimsikiliza Katibu Mkuu wa WMO, Prof. Petteri Taalas alipomkaribisha kutoa neno katika ufunguzi wa mkutano wa pili wa Jopo la Kamati Kuu ya WMO ya Kujenga Uwezo “Second Meeting of the Executive Council Capacity Development Panel (CDP-2)”, Tarehe 3 Februari, 2021.


 Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi akitoa hotuba ya kufungua mkutano wa pili wa Jopo la Kamati Kuu ya WMO ya Kujenga Uwezo “Second Meeting of the Executive Council Capacity Development Panel (CDP-2)”, Tarehe 3 Februari, 2021. Kulia kwake ni Meneja wa Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Wilbert Muruke  na kushoto kwake ni Mtaalamu wa Hali ya Hewa  katika Ofisi ya Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Mathew Ndaki wakimsaidia Mwenyekiti katika kuongoza kikao.


Dar es Salaam; Tarehe 03/02/2021.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi, ameongoza mkutano wa pili wa Jopo la Kamati Kuu ya WMO ya Kujenga Uwezo “Second Meeting of the WMO Executive Council Capacity Development Panel (CDP-2)”.

Akizungumza wakati akifungua rasmi mkutano huo, Dkt. Kijazi aliwataka wajumbe wa mkutano huo, kuzingatia lengo lililokasimiwa kwa jopo la kushauri namna bora ya kujenga uwezo katika uboreshaji wa huduma za hali ya hewa Duniani.

“Mkutano huu umelenga kujadili taarifa za utekelezaji wa majukumu ya Vikosi kazi vinavyounda Jopo hili, na kuandaa mapendekezo ya kuwasilisha kwenye Kamati Kuu ya WMO (WMO Executive Coincil (EC), na mapendekezo ya maeneo ya vipaumbele kwa ajili ya kuandaa Mpango Mkakati wa kujenga uwezo (WMO Capacity Development Strategy) katika utoaji huduma Kimataifa”. Alizungumza Dkt. Kijazi.

 Katika hatua nyingine, Dkt. Kijazi alimpongeza Katibu Mkuu wa WMO, Prof. Petteri Taalas, kwa kupewa tuzo na jarida la “Reader’s Digest Magazine” kama Mtu Mashuhuri wa Bara la Ulaya wa mwaka 2020 (European of the Year), ikiwa ni  kutambua mchango wake wa kuongoza jitihada za WMO kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.

Naye, Prof. Taalas alimshukuru Dkt. Kijazi na kusema kuwa tuzo hiyo ni maalum kwa wadau wote wa WMO na huduma za hali ya hewa kwa ujumla na alimpongeza  Dkt. Kijazi kwa uongozi wake mahiri unaosaidia  kufanikisha utekelezaji wa malengo ya WMO.

Mkutano huo ulifanyika kwa njia ya mtandao (teleconference) Tarehe 3 na 4 Februari, 2021 chini ya Mwenyekiti wa Jopo hilo, Dkt. Kijazi na kuhudhuriwa na Katibu Mkuu wa WMO, Prof. Petteri Taalas na watendaji wengine waandamizi wa WMO. Mkutano ulijadili taarifa za Vikosi kazi vinavyounda jopo hilo na kuandaa mapendekezo mbalimbali ya kujenga uwezo katika huduma za hali ya hewa. Miongoni mwa mapendekezo hayo ni pamoja na yatakayowasilishwa katika mkutano wa 73 wa Kamati Kuu ya WMO na  mapendekezo ya maeneo ya vipaumbele vitakavyotumika kuandaa Mpango Mkakati wa WMO wa kujenga uwezo. Mjadala ulijielekeza kutambua kwamba hali ya hewa haina mipaka hivyo katika kipindi hiki cha kuongezeka majanga yanayosababishwa na hali mbaya ya hewa jopo hilo lihakikishe vipaombele katika kujenga uwezo vinaelekezwa kuzisadia nchi zinazoendelea pamoja na za Bara la Afrika ili kuhakikisha maendeleo katika sekta ya hali ya hewa hayamuachi mtu yoyote nyuma (no one should be left behind).


Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...