Tanzania Meteorological Authority
Tuesday, May 26, 2026
Monday, May 25, 2026
KIPUPWE 2026: UPEPO ULIOPUNGUA NGUVU KIDOGO UNATARJIWA KATIKA MAENEO MENGI YA NCHI.
Dar es Salaam,Tarehe 25/05/2026:
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi mwelekeo wa hali ya hewa katika kipindi cha mwezi Juni hadi Agosti 2026 (Kipupwe). Akizungumza na waandishi wa habari Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang’a aliwataka wananchi kufuatilia na kuutumia ipasavyo utabiri wa msimu wa Kipupwe 2026, hasa ikizingatiwa kuwa katika kipindi hicho baadhi ya maeneo yanatarajia kupata vipindi vichache vya upepo mkali mwezi Juni na Julai 2026.
“Msimu wa Kipupwe 2026 unatarajiwa kutawaliwa na upepo uliopungua nguvu kidogo kama ilivyo kawaida, utakaovuma kutoka Kusini Mashariki kwa maeneo mengi ya nchi, na vipindi vichache vya upepo mkali utakaovuma kutoka kusini hususan katika kipindi cha miezi ya Juni na Julai 2026 hususani katika maeneo ya ukanda wa pwani ya Bahari ya Hindi na maeneo ya nchi kavu”. Alisema Dkt. Chang’a
Akizungumzia hali ya baridi Dkt. Chang’a alisema vipindi vya baridi zaidi vikitarajiwa kujitokeza katika mwezi Julai 2026, aidha, baridi ya wastani hadi joto kiasi inatarajiwa katika baadhi ya maeneo ya nchi.
“Hali ya baridi ya wastani hadi joto kiasi inatarajiwa katika maeneo ya Kanda ya Ziwa Victoria, Kanda ya magharibi, Kanda ya kusini, Nyanda za juu kusini- magharibi pamoja na Mkoa wa Singida. Hata hivyo, hali ya joto kiasi hadi baridi ya wastani ikitarajiwa katika maeneo ya Ukanda wa pwani ya kaskazini na maeneo ya nchi kavu, Nyanda za juu kaskazini mashariki, Ukanda wa pwani ya kusini pamoja na mkoa wa Dodoma huku vipindi vya baridi zaidi vikitarajiwa kujitokeza katika mwezi Julai 2026.” Alisema Dkt. Chang’a.
Akielezea kuhusu mwenendo wa mvua Dkt. Chang’a alisema vipindi vya mvua za nje ya msimu vinatarajiwa katika maeneo ya ukanda wa Ziwa Victoria hususan Mkoa wa Mara, ukanda wa mwambao wa pwani na maeneo ya nchi kavu pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba, na sehemu zenye miinuko za nyanda za juu kaskazini mashariki.
Kwa upande wa Athari zinazoweza kujitokeza Dkt. Chang’a alisema Magonjwa yanayohusiana na hali ya hewa ya baridi kama vile homa ya mapafu na magonjwa ya mifugo yanaweza kujitokeza. Hali ya vumbi linalosababishwa na upepo linaweza kupelekea uwepo wa magonjwa kama vile ya macho, mafua na magonjwa mengine yanayohusiana nayo, huku upungufu wa maji na malisho yakitarajiwa kujitokeza, na mwishoni alishauri Mamlaka husika pamoja na jamii kuchukua hatua stahiki kulingana na ushauri wa kitaalamu kutoka kwa wataalamu katika sekta zao.
Thursday, May 21, 2026
TMA YATOA ELIMU YA HALI YA HEWA KWA WAVUVI KUPITIA MRADI WA ECOFISH
Pemba, 20 Mei 2026.
Mradi wa ECOFISH unaotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Denmark kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Shirika la Denmark la Maendeleo ya Kimataifa (DANIDA), unaendelea kuboresha shughuli za uvuvi kwa jamii ya Pwani na kuimarisha huduma za tahadhari za mapema za hali ya hewa nchini.
Katika utekelezaji wa mradi huo, wataalamu kutoka TMA walikutana na wavuvi pamoja na wakulima wa Mwani kwa lengo la kujionea hali halisi ya shughuli zao za kiuchumi na changamoto zitokanazo na mabadiliko ya hali ya hewa wanazokabiliana nazo, sambamba na kutoa elimu kuhusu matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa katika shughuli za uvuvi na kilimo cha Mwani. Ziara hiyo iliambatana na semina maalum iliyowakutanisha wavuvi na wakulima wa Mwani ikiwa ni sehemu ya juhudi za mradi huo katika kuongeza uelewa wa jamii kuhusu umuhimu wa matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika kufanya maamuzi sahihi na salama.
Akizungumza katika semina hiyo, Mtaalamu wa Hali ya Hewa kutoka TMA na msimamizi wa mradi, Dkt. Sarah Emerald Osima, alisema mradi wa ECOFISH una mchango mkubwa katika kuimarisha huduma za hali ya hewa na ustahimilivu wa jamii za Pwani kupitia tafiti, elimu na teknolojia za tahadhari za mapema.
Dkt. Sarah aliendelea kusema mradi huo pia umewezesha udhamini wa masomo kwa wanafunzi saba wa shahada za uzamili na uzamivu kutoka Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI), Taasisi ya Sayansi za Bahari ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (IMS) pamoja na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), ambapo mmoja wao ni mfanyakazi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA). Alisema hatua hiyo inalenga kujenga wataalamu watakaosaidia sekta ya uvuvi na hali ya hewa kwa siku zijazo.
Aidha, wananchi wa kisiwani hapoo wamepongeza mradi huu wa ECOFISH na TMA kwa kuwapatia elimu hiyo, wakisema imewasaidia kuelewa na kutumia taarifa za hali ya hewa katika kupanga shughuli zao za uvuvi.
“Sasa tunajua umuhimu wa kutafuta na kutumia taarifa za hali ya hewa, jambo ambalo hapo awali tulikuwa tunalifanya kwa uelewa mdogo. Kwa sasa tumejifunza mambo mengi ikiwemo namna ya kutafsiri taarifa hizo kama zinavyotolewa na wataalamu,” alisema Afisa Uvuvi kutoka Wilaya ya Wete, Ndugu,Suleiman Ali Amadi.
Monday, May 18, 2026
TMA NA BRAC MAENDELEO TANZANIA WAJADILI MIKAKATI YA KUIMARISHA USAMBAZAJI NA MATUMIZI YA TAARIFA ZA HALI YA HEWA.
Dodoma, Mei 15, 2026
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na BRAC Maendeleo Tanzania walifanya kikao Makao Makuu ya TMA jijini Dodoma, wakijadili mikakati ya kuimarisha usambazaji na matumizi ya taarifa za hali ya hewa nchini.
Kikao hicho kiliongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang’a, kwa kuwakaribisha wajumbe wa BRAC Maendeleo Tanzania na kueleza kuwa TMA inathamini ushirikiano na wadau katika kuboresha huduma za hali ya hewa. Alisema mkutano huo unatoa fursa ya taasisi hizo mbili kuelewana na kuchunguza maeneo ya ushirikiano katika huduma za hali ya hewa, tahadhari za mapema na hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Pia alieleza kuwa TMA ipo katika mageuzi ya kidigitali yanayolenga kuboresha utoaji wa huduma kwa njia za kisasa.
Dkt. Chang’a Alieleza dhamira ya TMA kuendelea kuboresha huduma za hali ya hewa na ushawishi wa Tanzania katika maduala ya hali ya hewa katika bara la Africa na ukanda wa Nchi zinazoendelea. Aliwashukuru BRAC kwa majadiliano yenye tija na kwa mchango wao katika kuelimisha Jamii na kuimarisha usambazaji wa Taarifa za hali ya hewa kwa jamii. Alisisitiza na kuhamasisha ushiriki wa WADAU wengi katika Mkutano wa nne wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Unaolenga kuboresha miongozo ya Utabiri wa Hali ya Hewa (Operational Climate Prediction OCP-4) na Unatarajiwa kufanyika Arusha kuanzia 29 Juni hadi 3 Julai 2026.
Kwa upande wake Bw. Degefu Getachew Kelbiso, Meneja Mwandamizi wa Programu ya Hali ya Hewa ya Kimataifa na BRAC Maendeleo Tanzania, alieleza kuhusu mpango wa “BigBet” unaolenga kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kupitia huduma za taarifa za hali ya hewa, kilimo kinachozingatia mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi, masoko na uimarishaji wa maisha ya jamii katika nchi kadhaa ikiwemo Tanzania.
Bw. Degefu alieleza haja ya kuimarisha ushirikiano katika kuendelea kuboresha upatikanaji, usambazaji, tafsiri na matumizi ya taarifa za hali ya hewa kwa watumiaji wa mwisho na katika sekta zote za kiuchumi na kijamii na katika miradi ya jamii na maendeleo.
Saturday, May 16, 2026
KAMATI YA URATIBU YA MRADI WA SOFF YAKUTANA JIJINI DODOMA
Dodoma, 14 Mei 2026
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), kwa kushirikiana na Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), walifanya kikao kazi cha tano cha Kamati ya Uratibu wa Mradi wa SOFF (Systematic Observations Financing Facilit) katika Hoteli ya Morena jijini Dodoma.
Kikao hicho kiliwakutanisha wataalamu muhimu ili kupitia maendeleo ya utekelezaji wa mradi wa SOFF na kujadili vipaumbele vya kimkakati kwa mwaka 2026, vinavyolenga kuhakikisha ufanisi katika utekelezaji wa shughuli za mradi.
Majadiliano yalijikita katika utekelezaji wa Mpango Kazi wa Mwaka 2026, ufuatiliaji na tathmini ya mradi, pamoja na shughuli za mawasiliano na uhamasishaji zilizopangwa kwa mwaka 2026. Kamati pia ilipitia maamuzi na maelekezo kutoka kikao cha Tatu cha Kamati Tendaji ya Mradi wa SOFF kilihofanyika Aprili 2026.
Wakizungumza katika ufunguzi, Wenyeviti wenza wa kamati hiyo, Dkt. Paschal Waniha kutoka TMA na Dkt.Abbas Kitogo kutoka UNDP, walisisitiza umuhimu wa kuendelea kushirikiana kikamilifu ili kuhakikisha utekelezaji unafanyika kwa wakati katika shughuli zote zilizopangwa za mradi wa SOFF Tanzania.Aidha,
kikao kilihitimishwa kwa wajumbe kutoa dhamira ya pamoja ya kuimarisha uratibu, kuharakisha utekelezaji wa shughuli zilizopangwa, na kuongeza ufanisi wa jumla wa mradi wa SOFF nchini Tanzania.
THE FIFTH SOFF PROJECT TECHNICAL COORDINATION COMMITTEE IN TANZANIA CONVENES IN DODOMA
Dodoma, 14th May 2026;
The Tanzania Meteorological Authority in collaboration with the United Nations Development Programme (UNDP) convened for the Fifth Meeting of the Systematic Observations Financing Facility (SOFF) Project Technical Coordination Committee (PTCC-5) at Morena Hotel in Dodoma.
The meetin
g brought together Members of the PTCC and key experts to deliberate on the implementation progress of the SOFF project and to discuss strategic priorities for implementation of the project in 2026 aimed at ensuring efficiency in the implementation of project activities.
The agenda of the meeting focused more on the implementation of the approved 2026 SOFF Project Annual Workplan, project monitoring report, as well as planned monitoring, communication and outreach activities for 2026. The committee also strategized on the implementation of decisions and directives by the SOFF Project Steering Committee (PSC), which were given by the PSC at the 3rd meeting held on 9th April 2026.
Speaking during the opening session, the PTCC Co-Chairs, Dr. Paschal Waniha and Dr. Abbas Kitogo from TMA and UNDP respectively, emphasized the importance of continued effective collaboration to ensure timely implementation of all planned SOFF project activities.
Also the PTCC-5 meeting concluded with a shared commitment among PTCC members to strengthen coordination, accelerate the implementation of planned activities, and enhance the overall effectiveness of the SOFF project in Tanzania
Wednesday, May 13, 2026
Featured Post
DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.
Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...
-
DODOMA; Tarehe 19 Agosti, 2024; Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imekutana na wadau kutoka sekta mbalimbali nchini ili kujipanga na...
-
Dar es Salaam, 22 /0 8 /202 4 ; Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa utabiri wa msimu wa mvua za VULI 202 4 kwa maeneo yanayopat...
-
Dar es Salaam, Tarehe 05/02/2026; Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Masika 202 6 kwa maeneo...

























