Sunday, March 1, 2026

DKT CHANG’A AFANYA MAZUNGUMZO NA KATIBU MKUU WA SHIRIKA LA HALI YA HEWA DUNIANI (WMO)

DKT CHANG’A AFANYA MAZUNGUMZO NA KATIBU MKUU WA SHIRIKA LA HALI YA HEWA DUNIANI (WMO)

 

 Geneva, 27 Februari 2026

Katibu Mkuu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (World Meteorological Organization - WMO) Prof. Celeste Saulo ameahidi kuendelea kushirikiana na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) katika kuboresha huduma za hali ya hewa kwa matumizi katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii.

Ameyasema hayo wakati wa kikao cha pembezoni mwa kikao cha 70 cha Kamati Kuu Tendaji ya Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (Seventieth Session of the Intergovernmental Panel on Climate Change-IPCC (70th IPCC Bureau), alipokutana na  Dkt. Ladislaus Chang’a, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya hali ya Hewa Tanzania (TMA), ambaye pia ni Mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika WMO na Makamu wa Mwenyekiti wa Jopo la IPCC kwa lengo la kujadiliana kuhusu maendeleo ya utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini Tanzania na mipango ya kuendeleza ushirikiano na WMO tarehe 27 Februari 2026 Jijini Geneva, Uswisi.

Prof. Celeste Saulo amempongeza Dkt. Chang’a na kufurahishwa na namna TMA wanavyoendelea kusimamia vyema utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini Tanzania. Aidha, Prof. Celeste Saulo ameahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuboresha huduma za hali ya hewa kupitia programu mbalimbali za WMO ikiwa ni pamoja na eneo la matumizi ya akili mnemba (AI) katika mnyororo mzima wa utoaji wa huduma za hali ya hewa. 

“Nimefurahishwa na maendeleo ya utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini kwenu. Sisi kama WMO tuko tayari kuendelea kushirikiana ili kuboresha zaidi huduma huduma za hali ya hewa nchini Tanzania ikiwa ni pamoja na kuwaunganisha na taasisi nyingine zilizopiga hatua zaidi ili kubadilishana ujuzi zaidi” Alisema Prof. Celeste Saulo.

Katika Kikao hicho, Dkt. Ladislaus Chang’a amemshukuru Katibu Mkuu wa WMO kwa usaidizi kwa TMA kupitia programu zake mbalimbali za uboreshaji wa huduma za hali ya hewa kikanda na kitaifa zikiwemo za “Climate Risk and Early Warning Systems (CREWS-EA), “Systematic Observations Financing Facility (SOFF)” na “Weather and Climate Information Services for Africa (WISER)” ambazo zinatekelezwa kwa ushirikiano na Wadau wa Maendeleo na Nchi Wanachama wa WMO ambapo utekelezaji wake unaendelea vizuri. 

“Nashukuru sana kwa usaidizi wa WMO kupitia programu zake mbalimbali zikiwemo za CREWS, SOFF na WISER ambazo zinachangia pakubwa katika kuboresha utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini na kuongeza nguvu katika uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hususan katika uboreshaji wa miundombinu ya hali ya hewa nchini na kuwajengea uwezo wataalamu. Programu hizi sio tu zimechagiza katika uboreshaji wa huduma za hali ya hewa bali zinawajengea uwezo wataalamu wa TMA wa kusaidia nchi nyingine kuboresha huduma zao za hali ya hewa” Alisema Dkt. Chang’a.

Dkt. Chang’a alimjulisha Katibu Mkuu wa WMO kuwa, Taasisi za Hali ya Hewa za Nchi wanachama wa WMO ambazo wataalamu wa TMA wametoa msaada wa kiufundi Barani Afrika hivi karibuni ni pamoja na Burundi, Sudan Kusini na Zimbabwe ambapo nchi nyingine ikiwa ni pamoja na Zambia, Sierra Leone na Uganda wataalamu wanaendelea na majadiliano ya namna wanavyoweza kusaidiwa na TMA katika maeneo ambayo TMA tumepiga hatua zaidi. Maeneo ambayo TMA imezisaidia nchi nyingine katika tasnia hii ya hali ya hewa ni pamoja na uboreshaji wa “Mfumo wa Usimamizi wa Ubora wa huduma (Quality Management System-QMS and Competency Assessment )”, “Utabiri wa Hali Mbaya ya Hewa (Severe Weather Forecasting)”, “Utabiri wa Hali ya Hewa kwa Kutumia Modeli za Kompyuta (Numerical Weather Prediction-NWP)”, “Mchakato wa kisheria katika sekta ya hali ya hewa (Legal Matters)” na Usambazaji wa Huduma za Hali ya Hewa kwa Umma (Public Weather Services-PWS). 

Katika kuhitimisha mazungumzo yao, Dkt. Chang’a alimshukuru Katibu Mkuu wa WMO kwa fursa ya kuleta mikutano mikubwa ya kitaalamu nchini ikiwa ni pamoja na mkutano wa nne (4) wa Wataalamu bingwa wa utabiri wa hali ya hewa Duniani utakaojadili maendeleo ya utabiri wa hali ya hewa kwa kuzingatia ukuaji wa teknolojia na matumizi ya huduma hizi kwa sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi “The Fourth WMO Operational Climate Prediction (OCP-4)” unaotarajiwa kufanyika Arusha mwishoni mwa mwezi Juni hadi mwanzo wa Julai 2026 kwa mara ya kwanza barani Afrika na kwa Tanzania.

IMETOLEWA NA:
KITENGO CHA UHUSIANO
MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA (TMA)

Tuesday, February 24, 2026

TMA, UDSM ZAIMARISHA MAHUSIANO YA KITAALAM NA KITAALUMA


 TMA, UDSM ZAIMARISHA MAHUSIANO YA KITAALAM NA KITAALUMA


 Dodoma, Februari 18, 2025.


Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) wamejadiliana namna ya kuimarisha ushirikiano wa kitaalam na kitaaluma kwa lengo la kuimarisha taaluma na sayansi ya hali ya hewa ili kuchangia katika kuboresha huduma za hali ya hewa nchini.


Majadiliano hayo yamefanyika katika kikao maalum kilicholenga kuangalia maeneo ya ushirikiano uliopo na namna ya kuuboresha, hususan katika matumizi ya tafiti zinazofanywa na UDSM kuhusiana na masuala ya hali ya hewa na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.


Akifungua kikao hicho, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang’a, alieleza kuwa ushirikiano kati ya taasisi hizo umedumu kwa muda mrefu na kikao hicho kimeweka mkazo katika kuimarisha maeneo mahsusi ya ushirikiano huo, ikiwemo kuimarisha uelewa na matumizi ya akili mnemba (AI) katika utafiti na huduma za hali ya hewa.


Akiongea wakati wa uwasilishaji wake Dkt. Paul T. S. Limbu Mhadhiri Mwandamizi wa Meteorolojia na Sayansi ya Hali ya hewa katika Idara ya Fizikia, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amesema kwa zaidi ya miaka 13 ya kufundisha masomo ya hali ya hewa, bado kuna haja ya kuendelea  kuimarisha zaidi ushirikiano kati ya  UDSM na TMA. 


Tunawashukuru sana TMA kwa kushiriki na kutusaidia  katika mchakato wa kuboresha mitaala, ufundishaji na usimamizi wa tafiti.


Pia ameeleza umuhimu wa wanafunzi kupata elimu kwa vitendo kupitia ziara za kitaaluma katika miundombinu ya TMA, fursa za kujitolea baada ya kuhitimu, pamoja na ushiriki wa TMA katika uandaaji wa vitabu vya kufundishia .


Aidha, pande hizo zimejadili ushiriki wa UDSM katika warsha, semina na maadhimisho ya siku muhimu kama Siku ya Hali ya Hewa Duniani ili kuwajengea wanafunzi uzoefu wa moja kwa moja katika mazingira halisi ya kazi.


Kwa ujumla, kikao hicho kimeweka msingi wa kuendeleza mazungumzo ya kitaalam yatakayosaidia kuunganisha tafiti, elimu na utekelezaji katika kuboresha huduma za hali ya hewa nchini.

Thursday, February 12, 2026

SERIKALI YATENGA BILIONI 13 KUWEZESHA UJENZI WA OFISI ZA TMA.

 









SERIKALI YATENGA BILIONI 13 KUWEZESHA UJENZI WA OFISI ZA TMA.


Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi, Mhe. David Kihenzile, ametembelea ujenzi wa ofisi za Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) zilizopo Sinza Simu 2000, jijini Dar es Salaam. Ujenzi huu, unaofadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, unalenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa taarifa sahihi za hali ya hewa.


Akizungumza katika ziara hiyo,Naibu Waziri wa Uchukuzi,Mhe.David Kihenzile amesema Serikali ya Awamu ya Sita imetenga takribani shilingi bilioni 13 kwa ajili ya ujenzi wa  ofisi za TMA. Miradi hiyo inahusisha ujenzi wa jengo la kisasa la Kanda ya Mashariki na Utoaji Tahadhari za Hali ya Hewa pamoja na kituo cha tahadhari za Tsunami nchini,pamoja na Kituo cha Taifa cha Uhakiki wa Vifaa vya Hali ya Hewa (National Meteorological Calibration Centre) kitakachosaidia kukagua na kuboresha vifaa vya hali ya hewa.


Mhe. Kihenzile amesema majengo yote mawili, yaliyoanza kujengwa mwaka 2023 na 2025, yanatarajiwa kukamilika kabla ya mwisho wa mwaka huu. Ameeleza kuwa miradi hiyo itaongeza ufanisi katika utoaji wa taarifa za hali ya hewa na kuwawezesha wataalamu kufanya kazi katika mazingira bora na ya kisasa.


Kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi,Mhe.David Kihenzile (MB), ametoa rai kwa Bodi na Menejimenti ya TMA kusimamia miradi hiyo kwa weledi, uzalendo na kuhakikisha inakamilika kwa wakati na kwa ubora uliokusudiwa.Aidha aliipongeza TMA kwa kumchagua mkandarasi wa ndani, Chuo cha DIT (Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam), kutekeleza miradi hiyo akieleza kuwa hatua hiyo inachochea maendeleo ya wataalamu na taasisi za ndani.


Pia,Naibu Waziri amewahimiza TMA kutoa taarifa kwa wakati ili kuwasaidia wananchi katika shughuli za kila siku zikiwemo usafiri, kilimo na matumizi ya bahari na amewahimiza wananchi kuendelea kuamini na kutumia taarifa rasmi za hali ya hewa kutoka TMA.

Thursday, February 5, 2026

TMA YATOA UTABIRI WA MSIMU WA MVUA ZA MASIKA 2026 KWA MAENEO YANAYOPATA MVUA MARA MBILI KWA MWAKA.

 


Dar es Salaam, Tarehe 05/02/2026;


Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2026 kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka. Akizungumza wakati wa mkutano na vyombo mbalimbali vya habari katika ukumbi wa Ubungo Plaza, tarehe 05/02/2026, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi Dkt. Ladislaus Chan’ga alisema maeneo mengi ya nchi yanayopata misimu miwili ya mvua yanatarajiwa kupata mvua za wastani hadi juu ya wastani.

 

 “Mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya nchi ikihusisha Pwani ya Kaskazini pamoja na baadhi ya maeneo ya Magharibi mwa ukanda wa Ziwa Viktoria (mikoa ya Kagera na Geita) pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma, isipokuwa maeneo ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki na baadhi ya maeneo ya ukanda wa Ziwa Viktoria (mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Mara na Simiyu) mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani zinatarajiwa”. Alisema Dkt. Chang’a.

 

Katika taarifa hiyo ilielezea kuwa Mvua za Masika zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya mwezi Februari na ya kwanza ya mwezi Machi , 2026 katika maeneo ya kanda ya Ziwa Victoria; na wiki ya kwanza na ya pili ya mwezi Machi katika maeneo ya pwani ya kaskazini; na wiki ya pili na ya tatu ya mwezi Machi,  2026 katika maeneo ya nyanda za juu kaskazini mashariki, Mvua hizo zikitarajiwa kuisha wiki ya nne ya mwezi Mei na wiki ya kwanza ya mwezi Juni 2026 katika maeneo mengi yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka huku ongezeko la mvua likitarajiwa katika kipindi cha mwezi Aprili 2026.


Akizungumzia athari zinazoweza kujitokeza, Dkt. Chang’a alisema vipindi vya unyevu wa kuzidi kiasi pamoja na mafuriko vinaweza kujitokeza na kuathiri ukuaji wa mazao katika baadhi ya maeneo, hususan yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani. Kina cha maji katika mito, mabwawa na hifadhi ya maji ardhini kinatarajiwa kupungua hususan katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani. Magonjwa ya mlipuko yanaweza kujitokeza kutokana na uchafuzi wa maji, hivyo kushauri watumiaji wa tarifa hizo kuzingatia ushauri wa wataalamu katika sekta zao.


Angalizo la matukio ya hali mbaya ya hewa ikiwemo vipindi vya mvua kubwa lilitolewa hata katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani huku watumiaji wa taarifa hiyo wakishauriwa kufuatilia taarifa za utabiri wa saa 24, siku 10, mwezi na tahadhari kama zinavyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).

 

Kwa taarifa zaidi tembelea; https://www.meteo.go.tz/uploads/documents/sw-1770290524-Taarifa%20ya%20Mwelekeo%20wa%20Mvua%20za%20Masika%202026.pdf



Tuesday, February 3, 2026

WADAU SEKTA YA HALI YA HEWA WAJADILI UTABIRI WA MASIKA 2026.

Dodoma, tarehe 2 Februari 2026:

Wadau kutoka sekta mbalimbali nchini wamekutana kujadili utabiri wa msimu wa Masika 2026 na kutoa ushauri wa kisekta katika Mkutano wa 25   wa Wadau wa Sekta ya Hali ya Hewa katika msimu wa Masika uliofanyika tarehe 2/2/2026, Jijini Dodoma. Mkutano huo ni mwendelezo wa ushirikishwaji wa wadau katika utoaji wa taarifa za hali ya hewa kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini. 

Mgeni Rasmi kwenye mkutano huo, Mh. Jaji  Mshibe Ali Bakari ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya TMA  alisema





























“msimu wa Vuli mwaka 2025 ulitawaliwa  na vipindi virefu vya ukavu katika maeneo mengi ya nchi, usahihi wa utabiri ulikuwa kwa asilimia 94.1, ikiwa ni kiwango kikubwa sana, natoa wito kwa wananchi waendelee kuiamini TMA, wazingatie taarifa zinazotolewa na kuzitumia katika shughuli zao za kila siku".  

Aidha, alisisitiza kuwa majadiliano ya mvua za Masika kwa mwaka 2026, yazingatie kwa kina athari zinazoweza kujitokeza pamoja na kutoa ushauri wa hatua stahiki za kuchukua kwa ajili ya matumizi ya taarifa hizo katika sekta mbalimbali zinazochangia ukuaji wa uchumi.

Awali, akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Changa, alisema "katika kupunguza pengo la uelewa wa tahadhari za hali ya hewa, Mamlaka imeendelea na juhudi za kushirikisha wadau, katika kuandaa taarifa zinazolenga kuchochea matumizi sahihi ya huduma za hali ya hewa nchini"

Dkt. Changa aliongeza kuwa TMA imeendelea kufanya shughuli zake kwa ubora unaoendana na viwango vya kitaifa na kimataifa na kuifanya Tanzania kuwa moja ya  nchi zinazoaminika kwa utoaji wa huduma bora za hali ya hewa duniani. Kupitia viwango hivyo,Tanzania imechaguliwa kuandaa  Mkutano wa Nne wa Kimataifa wa Watalaam Bingwa wa Hali ya Hewa Duniani, mwezi Juni 2026.

Kwa upande wa wadau, walitoa pongezi na shukrani kwa TMA kwa ushirikiano wanaoendelea kupata katika kuwasilisha taarifa za hali ya hewa kwa jamii. "Naipongeza TMA kwa kuandaa mkutano huu wa wadau wa hali ya hewa.Sisi ili tuweze kufanya kazi zetu ni lazima tupate taarifa zinazotusaidia katika mipango yetu ya kazi ili kulinda usalama wa wananchi na mali zao".Alisema Kaimu Mkurugenzi  wa Kamisheni Ya Maafa, Ofisi ya Makamu wa Rais wa Pili wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Ndg. Muhidin Ali Muhidin 

Mamlaka inatarajia kutoa utabiri wa msimu wa Masika 2026, tarehe 5/2/2026.

Wednesday, January 28, 2026

RADA ZA HALI YA HEWA NI MUHIMU KATIKA KUKABILIANA NA MABADILIKO YA HALI YA HEWA NCHINI.

 RADA ZA HALI YA HEWA NI MUHIMU KATIKA KUKABILIANA NA MABADILIKO YA HALI YA HEWA NCHINI.











Tarehe 26, Dodoma

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) iliandaa warsha ya mafunzo ya Rada za Hali ya Hewa na matumizi ya taarifa zinazotokana na Rada,  tarehe 26-27 Januari 2026, Dodoma. Lengo kuu la mafunzo haya ni kuimarisha uwezo wa kitaalamu na kiufundi katika matumizi ya teknolojia Rada, hususan katika uchambuzi, tafsiri na matumizi ya taarifa ili kuboresha utoaji wa utabiri zikiwemo tahadhari za  hali mbaya ya hewa kwa wakati na kwa usahihi zaidi.    

                 

Mgeni rasmi kwenye ufunguzi wa warsha hiyo alikuwa ni Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a alisema “Kama mnavyofahamu, kwa sasa dunia inashuhudia ongezeko kubwa la matukio ya hali mbaya ya hewa yanayotokana na  kuchagizwa na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi, ikiwemo mvua kubwa, mafuriko, vipindi virefu vya ukame, pamoja na matukio ya vimbunga na upepo mkali.  Matukio haya yamekuwa  ya mara kwa mara na ya hatari zaidi. Katika kipindi hiki huduma za tahadhari dhidi ya hali mbaya ya hewa ni muhimu sana hususani kwa nchi zinazoendelea, ikiwemo Tanzania, kwani uchumi wetu unategemea sana sekta za kijamii na kiuchumi zinazotegemea hali ya hewa. Katika muktadha huu uimarishaji wa miundombinu ya utoaji wa huduma za hali ya hewa ikiwemo uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali  wa kuimarisha mifumo ya Rada za hali ya hewa ni hatua kubwa na muhimu sana katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.


Aidha, Mratibu  wa mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Mradi wa Kuboresha Mfumo wa Utoaji wa Tahadhari za Hali Mbaya ya Hewa “Climate Risk and Early Warning Systems (CREWS) kwa ufadhili wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO)” Bi. Mecklina Merchades  alisema mafunzo hayo yanalenga katika kuhakikisha wataalam wanakuwa na ujuzi wa kutosha katika kutumia mifumo ya Rada kama nyenzo muhimu ya kuboresha ufuatiliaji na utabiri wa matukio ya hali mbaya ya hewa, yenye athari kwenye sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi. 


TMA inaendelea kuishukuru Serikali kwa uwekezJi mkubwa katika kuimarisha rasilimali watu, miundombinu, teknolojia na mifumo ya kisasa kwa lengo la kuboresha huduma za tahadhari na kuchangia katika kulinda maisha, mali na ustawi wa jamii.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...