Tanzania Meteorological Authority
Tuesday, August 18, 2026
TMA YATOA ANGALIZO DHIDI YA EL NINO, MSIMU WA VULI 2026
Dar Es Salaam – 18 Agosti, 2026
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Vuli (Oktoba – Desemba) 2026, ikitoa angalizo la msimu huo kuathiriwa kwa kiwango kikubwa na hali ya El Niño yenye nguvu kubwa iliyotokana na joto la bahari kuwa Juu ya Wastani katika Bahari ya Pasifiki, hali itakayochagiza ongezeko la Mvua za Vuli 2026 kuwa za Juu ya Wastani hadi Wastani katika maeneo mengi ya Ukanda wa Pwani ya Kaskazini, Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki, Ukanda wa Ziwa Viktoria na kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma.
Akizungumza juu ya utabiri huo, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabia Nchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang'a alisema:-
"Msimu wa mvua za Vuli 2026 unatarajiwa kuathiriwa kwa kiwango kikubwa na hali ya El Niño yenye nguvu kubwa, hivyo mvua za Juu ya Wastani hadi Wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya nchi Ukanda wa Pwani ya Kaskazini, Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki, Ukanda wa Ziwa Viktoria na kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma”. Aliongezea kusema kuwa Mvua hizo zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya mwezi Septemba hadi wiki ya kwanza ya mwezi Oktoba 2026 katika maeneo ya ukanda wa Ziwa Viktoria, na kusambaa taratibu katika maeneo mengine katika mwezi Oktoba 2026, aidha alifanunua kuwa kwa kawaida mvua za Vuli huisha mwezi Desemba japo katika msimu wa Vuli 2026 mvua za nje ya msimu zinatarajiwa kuendelea hadi mwezi Januari 2027, na ongezeko la mvua likitarajiwa hasa katika kipindi cha mwezi Novemba 2026.
Akielezea juu ya athari zinazotarajiwa, Dkt. Chang’a ametahadharisha kuwa "vipindi vya unyevu kwenye udongo wa kuzidi kiasi pamoja na mafuriko vinaweza kujitokeza na kuathiri ukuaji wa mazao na miundombinu ya kilimo," pia aliongezea kusema kuwa ongezeko la kina cha maji katika mabwawa na mito linaweza kuathiri miundombinu ya rasilimali za maji na nishati, huku magonjwa ya mlipuko yanaweza kujitokeza kutokana na uchafuzi wa maji. Magonjwa ya mazao yanayosababishwa na kuvu, bakteria na virusi yanaweza kuathiri uzalishaji wa viazi mviringo, alizeti, maharage, ufuta pamoja na matunda na mbogamboga, huku sekta za usafiri, ujenzi na utalii zikitarajiwa kukumbwa na changamoto za mmomonyoko wa barabara, uharibifu wa madaraja na kuhama kwa wanyamapori kutokana na mafuriko.
Katika hitimisho lake, Dkt. Chang’a amewashauri Wadau wa sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii kupanga na kutekeleza shughuli zao kwa kuzingatia taarifa mahususi za hali ya hewa zinazotolewa na TMA ikiwa ni pamoja na kuvuna maji ya mvua, kuimarisha miundombinu, kutoa tahadhari za mapema na kudhibiti mazalia ya mbu ili kupunguza magonjwa ya mlipuko.
Kwa taarifa zaidi tembelea: https://www.meteo.go.tz/uploads/documents/sw-1758375754-Mwelekeo%20wa%20Mvua%20za%20Vuli%202025.pdf
Monday, August 17, 2026
ATHARI ZA EL NIÑO KATIKA MVUA ZA VULI 2026: TMA YAWANOA WANAHABARI
Dar es Salaam, 17 Agosti 2026
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imebainisha kuwa hali ya El Niño iliyoanza kujitokeza mwezi Aprili 2026 imeendelea kuimarika na inatarajiwa kuchagiza mwenendo wa mvua za msimu wa Vuli wan Oktoba hadi Disemba 2026 na kuleta vipindi vya hali mbaya ya hewa katika baadhi ya maeneo ya nchi.
Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabia Nchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang'a, wakati wa warsha ya wanahabari iliyofanyika jijini Dar es Salaam. Warsha hiyo ni mwendelezo wa juhudi za TMA za kuhakikisha kuwa wanahabari wanapata uelewa wa utabiri wa hali ya hewa na tafsiri zake kabla haujatolewa rasmi ili kuifikia jamii kwa usahihi.
"Hali ya El Niño inatarajiwa kuendelea kuimarika na kufikia kiwango cha El Nino yenye nguvu kubwa kuelekea mwishoni mwa mawaka na hivyo kusababisha ongezeko la mvua katika ukanda wa Afrika Mashariki " alisema Dkt. Chang'a.
Dkt. Chang'a aliongeza kuwa, katika hatua za kuboresha Tuzo za Wanahabari Bora wa Habari za Hali ya Hewa kwa mwaka 2026, TMA na Taasisi ya Usimamizi wa Mazingira na Maendeleo ya Kiuchumi (EMEDO) wameungana ili kuhakikisha kuwa tukio la utoaji wa tuzo hizo linakuwa kubwa na la kuvutia zaidi. Kwa sababu hiyo, aliwasisitiza wanahabari wote nchini kuwasilisha kazi zao za ushindani ili kuwania Tuzo hizo.
Aidha, kwa upande wao, wanahabari, wameipongeza TMA kwa kuendelea kuboresha usahihi wa utabiri na huduma za hali ya hewa kwa ujumla.
Utabiri rasmi wa Mvua za Vuli ulitolewa rasmi tarehe 18 Agosti 2026.
Kauli mbiu ya warsha hiyo ilikuwa: "Kupunguza Pengo la Uelewa wa Tahadhari za Hali ya Hewa kwa Pamoja."
Friday, August 14, 2026
JAJI MSHIBE ASISITIZA MAANDALIZI YA KISEKTA KATIKA KUKABILIANA NA ATHARI ZA EL NIÑO
Dodoma, 14 Agosti 2026:
Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Mheshimiwa Jaji Mshibe Ali Bakari, amezitaka sekta zote nchini kutumia ipasavyo taarifa za hali ya hewa katika kufanya maandalizi ya kisekta ya kukabiliana na athari zinazoweza kusababishwa na uwepo wa El Niño.
Mhe. Jaji Mshibe aliyasema hayo wakati akifungua Mkutano wa 25 wa kujadili Utabiri wa Msimu wa Mvua za Vuli, Oktoba hadi Disemba 2026, uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa PSSSF, Dodoma.
“Tunapojiandaa kupokea taarifa ya utabiri wa mvua za Vuli, Oktoba hadi Disemba 2026, ni muhimu kila mmoja wetu kuwa na jukumu la kufuatilia kwa karibu na kuelewa taarifa hizo ili kuanza maandalizi ya hatua za kuchukua katika kukabiliana na athari za hali ya hewa zinazotarajiwa kujitokeza katika sekta yake, kwa kutambua kuwa upo uwezekano mkubwa kwa El Niño kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka 2026,” alisisitiza Mhe. Jaji Mshibe.
Mhe. Jaji mshibe aliongeza kuwa Tanzania, kama ilivyo kwa nchi nyingine duniani, inaendelea kukabiliana na athari za mabadiliko ya hali ya hewa yanayodhihirishwa kupitia ongezeko la joto, ukame, upepo mkali, vimbunga na vipindi vya mvua kubwa vinavyoweza kusababisha mafuriko, hivyo amewataka wadau wasiishie katika kupokea taarifa za utabiri wa hali ya hewa, bali wazitumie katika kufanya maamuzi yanayozingatia mazingira ya sekta na maeneo yao.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a, alisema TMA imeendelea kuboresha utoaji wa taarifa za hali ya hewa, ikiwemo kuandaa utabiri mahususi kwa maeneo madogo kwa wilaya 86 zilizopo katika mikoa inayopata mvua za Vuli, hatua inayolenga kuhakikisha kila wilaya na sekta husika zinaweza kutumia taarifa za hali ya hewa katika kufanya maamuzi na kupanga shughuli zao.
Aidha, Dkt. Chang’a alimalizia kwa kusisitiza kuwa taarifa za utabiri na tahadhari zinapaswa kuzingatiwa katika sekta zote za kiuchumi na kijamii, kwa lengo la kuongeza tija na kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na hali mbaya ya hewa itakayotokana na uwepo wa El nino nchini.
“Nitumie fursa hii kuwajulisha kuwa mwaka huu 2026 tunakabiliwa na changamoto ya El Nino ambayo inatarajiwa kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka na hivyo kuchagiza mvua za VULI, hivyo basi matumizi sahihi na kwa wakati ya taarifa za hali ya hewa ni muhimu kwa Kila sekta katika kukabiliana na changamoto hii”. Alisema Dkt.Chang’a.
Naye, mwakilishi wa wadau mbalimbali kutoka Zanzibar, Bw. Makame Kh Makame, Mkurugenzi wa kamisheni ya kukabiliana na maafa Zanzibar, Alisema "Utabiri wa hali ya hewa ni jambo moja muhimu mno hasa katika kipindi cha El -Nino ambapo jamii na sekta zote muhimu zina
hitaji kujikinga, kujiandaa, kukabiliana na majanga au maafa yanayoweza kutokea sambamba na kurejesha hali baada ya maafa".
Mkutano huo uliobeba kaulimbiu: “Kupunguza Pengo la Uelewa wa Tahadhari za Hali ya Hewa kwa Pamoja.” ulihusisha pia utoaji wa mrejesho kutoka kwa wadau kuhusu utabiri wa msimu wa mvua za Masika uliokuwa na usahihi wa asilimia 94.1.
TMA inatarajia kutoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Vuli 2026 tarehe 18 Agosti 2026.
Featured Post
DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.
Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...
-
Dar es Salaam, Tarehe 05/02/2026; Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Masika 202 6 kwa maeneo...
-
DODOMA; Tarehe 19 Agosti, 2024; Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imekutana na wadau kutoka sekta mbalimbali nchini ili kujipanga na...
-
Dar es Salaam, 22 /0 8 /202 4 ; Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa utabiri wa msimu wa mvua za VULI 202 4 kwa maeneo yanayopat...






.jpeg)





























