Dodoma, 14 Agosti 2026:
Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Mheshimiwa Jaji Mshibe Ali Bakari, amezitaka sekta zote nchini kutumia ipasavyo taarifa za hali ya hewa katika kufanya maandalizi ya kisekta ya kukabiliana na athari zinazoweza kusababishwa na uwepo wa El Niño.
Mhe. Jaji Mshibe aliyasema hayo wakati akifungua Mkutano wa 25 wa kujadili Utabiri wa Msimu wa Mvua za Vuli, Oktoba hadi Disemba 2026, uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa PSSSF, Dodoma.
“Tunapojiandaa kupokea taarifa ya utabiri wa mvua za Vuli, Oktoba hadi Disemba 2026, ni muhimu kila mmoja wetu kuwa na jukumu la kufuatilia kwa karibu na kuelewa taarifa hizo ili kuanza maandalizi ya hatua za kuchukua katika kukabiliana na athari za hali ya hewa zinazotarajiwa kujitokeza katika sekta yake, kwa kutambua kuwa upo uwezekano mkubwa kwa El Niño kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka 2026,” alisisitiza Mhe. Jaji Mshibe.
Mhe. Jaji mshibe aliongeza kuwa Tanzania, kama ilivyo kwa nchi nyingine duniani, inaendelea kukabiliana na athari za mabadiliko ya hali ya hewa yanayodhihirishwa kupitia ongezeko la joto, ukame, upepo mkali, vimbunga na vipindi vya mvua kubwa vinavyoweza kusababisha mafuriko, hivyo amewataka wadau wasiishie katika kupokea taarifa za utabiri wa hali ya hewa, bali wazitumie katika kufanya maamuzi yanayozingatia mazingira ya sekta na maeneo yao.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a, alisema TMA imeendelea kuboresha utoaji wa taarifa za hali ya hewa, ikiwemo kuandaa utabiri mahususi kwa maeneo madogo kwa wilaya 86 zilizopo katika mikoa inayopata mvua za Vuli, hatua inayolenga kuhakikisha kila wilaya na sekta husika zinaweza kutumia taarifa za hali ya hewa katika kufanya maamuzi na kupanga shughuli zao.
Aidha, Dkt. Chang’a alimalizia kwa kusisitiza kuwa taarifa za utabiri na tahadhari zinapaswa kuzingatiwa katika sekta zote za kiuchumi na kijamii, kwa lengo la kuongeza tija na kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na hali mbaya ya hewa itakayotokana na uwepo wa El nino nchini.
“Nitumie fursa hii kuwajulisha kuwa mwaka huu 2026 tunakabiliwa na changamoto ya El Nino ambayo inatarajiwa kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka na hivyo kuchagiza mvua za VULI, hivyo basi matumizi sahihi na kwa wakati ya taarifa za hali ya hewa ni muhimu kwa Kila sekta katika kukabiliana na changamoto hii”. Alisema Dkt.Chang’a.
Naye, mwakilishi wa wadau mbalimbali kutoka Zanzibar, Bw. Makame Kh Makame, Mkurugenzi wa kamisheni ya kukabiliana na maafa Zanzibar, Alisema "Utabiri wa hali ya hewa ni jambo moja muhimu mno hasa katika kipindi cha El -Nino ambapo jamii na sekta zote muhimu zina
hitaji kujikinga, kujiandaa, kukabiliana na majanga au maafa yanayoweza kutokea sambamba na kurejesha hali baada ya maafa".
Mkutano huo uliobeba kaulimbiu: “Kupunguza Pengo la Uelewa wa Tahadhari za Hali ya Hewa kwa Pamoja.” ulihusisha pia utoaji wa mrejesho kutoka kwa wadau kuhusu utabiri wa msimu wa mvua za Masika uliokuwa na usahihi wa asilimia 94.1.
TMA inatarajia kutoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Vuli 2026 tarehe 18 Agosti 2026.












































