Friday, August 14, 2026

JAJI MSHIBE ASISITIZA MAANDALIZI YA KISEKTA KATIKA KUKABILIANA NA ATHARI ZA EL NIÑO

Dodoma, 14 Agosti 2026: 


Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Mheshimiwa Jaji Mshibe Ali Bakari, amezitaka sekta zote nchini kutumia ipasavyo taarifa za hali ya hewa katika kufanya maandalizi ya kisekta ya kukabiliana na athari zinazoweza kusababishwa na uwepo wa El Niño.

Mhe. Jaji Mshibe aliyasema hayo wakati akifungua Mkutano wa 25 wa kujadili Utabiri wa Msimu wa Mvua za Vuli, Oktoba hadi Disemba 2026, uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa PSSSF, Dodoma.

“Tunapojiandaa kupokea taarifa ya utabiri wa mvua za Vuli, Oktoba hadi Disemba 2026, ni muhimu kila mmoja wetu kuwa na jukumu la kufuatilia kwa karibu na kuelewa taarifa hizo ili kuanza maandalizi ya hatua za kuchukua katika kukabiliana na athari za hali ya hewa zinazotarajiwa kujitokeza katika sekta yake, kwa kutambua kuwa upo uwezekano mkubwa kwa El Niño kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka 2026,” alisisitiza Mhe. Jaji Mshibe.


Mhe. Jaji mshibe aliongeza kuwa Tanzania, kama ilivyo kwa nchi nyingine duniani, inaendelea kukabiliana na athari za mabadiliko ya hali ya hewa yanayodhihirishwa kupitia ongezeko la joto, ukame, upepo mkali, vimbunga na vipindi vya mvua kubwa vinavyoweza kusababisha mafuriko, hivyo amewataka wadau wasiishie katika kupokea taarifa za utabiri wa hali ya hewa, bali wazitumie katika kufanya maamuzi yanayozingatia mazingira ya sekta na maeneo yao.


Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a, alisema TMA imeendelea kuboresha utoaji wa taarifa za hali ya hewa, ikiwemo kuandaa utabiri mahususi kwa maeneo madogo kwa wilaya 86 zilizopo katika mikoa inayopata mvua za Vuli, hatua inayolenga kuhakikisha kila wilaya na sekta husika zinaweza kutumia taarifa za hali ya hewa katika kufanya maamuzi na kupanga shughuli zao.


Aidha, Dkt. Chang’a alimalizia kwa kusisitiza kuwa taarifa za utabiri na tahadhari zinapaswa kuzingatiwa katika sekta zote za  kiuchumi na kijamii, kwa lengo la kuongeza tija na kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na hali mbaya ya hewa itakayotokana na uwepo wa El nino nchini.


“Nitumie fursa hii kuwajulisha kuwa mwaka huu 2026 tunakabiliwa na changamoto ya El Nino ambayo inatarajiwa kuendelea kuimarika kuelekea  mwishoni mwa mwaka na hivyo kuchagiza mvua za VULI, hivyo basi matumizi sahihi na kwa wakati ya taarifa za hali ya hewa ni muhimu kwa Kila sekta katika kukabiliana na changamoto hii”. Alisema Dkt.Chang’a.


Naye, mwakilishi wa wadau mbalimbali kutoka Zanzibar, Bw. Makame Kh Makame, Mkurugenzi wa kamisheni ya kukabiliana na maafa Zanzibar, Alisema "Utabiri wa hali ya hewa ni jambo moja muhimu mno hasa katika kipindi cha El -Nino ambapo jamii na sekta zote muhimu zina































hitaji kujikinga, kujiandaa, kukabiliana na majanga au maafa yanayoweza kutokea sambamba na kurejesha hali baada ya maafa".


 Mkutano huo uliobeba kaulimbiu: “Kupunguza Pengo la Uelewa wa Tahadhari za Hali ya Hewa kwa Pamoja.” ulihusisha pia utoaji wa mrejesho kutoka kwa wadau kuhusu utabiri wa  msimu wa mvua za Masika  uliokuwa na usahihi wa asilimia 94.1. 


TMA inatarajia kutoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Vuli 2026 tarehe 18 Agosti 2026.

Friday, August 7, 2026

KATIBU TAWALA MKOA WA TANGA AVUTIWA NA SAYANSI YA HALI YA HEWA.











Morogoro, Tarehe 06 Agosti 2026.

 

Katibu tawala wa Mkoa wa Tanga, Bw. Rashid Mchatta avutiwa na sayansi ya hali ya hewa, aliyasema hayo Tarehe 06 Agosti 2026 mara baada ya kupokea elimu ya hali ya hewa iliyokuwa inatolewa na wataalamu Bingwa wa Hali ya Hewa katika Jengo la Mamlaka lililopo katika Viwanja vya NaneNane, Morogoro kupitia maonesho ya NaneNane yanayoendelea kufanyika kuanzia tarehe 01 hadi 08 Agosti 2026.

 

“Sayansi ya hali ya hewa ukiifuatilia vizuri inavutia, lakini pia utaalamu wenu ni wa tofauti na sayansi nyingine, hivyo niwapongeze kwa kazi nzuri ya utabiri”.  Alisisitiza Bw. Mchatta.

 

Kupitia maonesho hayo yaliyokuwa na kauli mbiu “Tambua Soko, ongeza tija, tekeleza Dira 2050”, wageni wameendelea kupokea elimu mbalimbali ya hali ya hewa na kufahamu njia za usambazaji wa taarifa za Mamlaka, iliyopelekea wadau kuendelea kusajiliwa kupitia mifumo mbalimbali ya Mamlaka ili kuweza kupokea taarifa za hali ya hewa kidigitali.

 

Mamlaka inaendelea kuwaalika wadau mbalimbali kuendelea kutembelea katika mabanda ya TMA yaliyopo katika viwanja vya maonesho ya NaneNane, ambapo Kitaifa yanafanyika katika mkoa wa Dodoma na Kikanda ni katika mikoa ya Mbeya na Morogoro.

Tuesday, August 4, 2026

WATAALAM WA TANROADS WASISITIZWA KUZINGATIA MATUMIZI YA TAARIFA ZA HALI YA HEWA KATIKA KUPANGA NA KUTEKELEZA SHUGHULI ZA UJENZI

 





Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesisitiza umuhimu wa kuzingatia  matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa miundombinu ikiwemo barabara na madaraja . 


Akizungumza na viongozi na watumishi mbalimbali wa  Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS)- DODOMA, katika kikao kilichofanyika leo kati ya TMA na Menejimenti na Wataalamu wa TANROAD -Dodoma, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa ya Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt.Ladislaus Chang’a, alisema “Dunia inakabiliwa na changamoto ya kasi kubwa ya ongezeko la joto, idadi na ukubwa wa matukio ya hali mbaya ya hewa ikiwemo mvua kubwa, mafuriko, upepo mkali na ukame. Matukio haya ya hali mbaya ya hewa yanaendelea kuhatarisha maisha ya watu na mali zao, ikiwemo uharibifu wa miundombinu mbalimbali ikiwemo ya barabara na madaraja". 


Aidha, aliongeza kwa kusema kuwa mwaka huu 2026, dunia inakabiliwa na changamoto ya El Nino, ambayo inatarajiwa kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka. Mamlaka ya Hali ya Hewa inaendelea kufuatilia kwa karibu na itatoa taarifa ya kina kuhusu mwelekeo na athari za El-Nino 2026 tarehe 18/08/2026 wakati wa kutoa utabiri wa mvua za VULI. 


Dkt. Chang’a alisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya Mwaka 2019 katika matumizi ya taarifa na huduma za hali ya hewa katika sekta zote za kiuchumi na kijamii ili kuokoa maisha ya watu na mali zao, na pia kuongeza ufanisi na tija katika shughuli zote za kimaendeleo.


Hatua na mikutano hii ni mwendelezo wa mkakati wa kuhamasisha matumizi ya taarifa na  huduma za hali ya hewa katika mipango na maendeleo ya Taifa, hususan kipindi hiki ambapo Dunia kwa ujumla inakabiliwa na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa.

MAONESHO YA NANENANE YAWA CHANZO CHA ELIMU YA HALI YA HEWA KWA WADAU.

3 Agosti 2026, Dodoma.








Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inashiriki  katika maonesho ya NaneNane  2026 yanayofanyika  kuanzia tarehe 1 hadi 8 Agosti 2026,katika viwanja vya John Malecela, Nzunguni jijini Dodoma.


Maonesho hayo yanatoa fursa kwa wadau mbalimbali kupata elimu ya hali ya hewa, shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na TMA,ikiwemo shughuli ya uthibiti na uratibu wa huduma za hali ya hewa nchini.


TMA inashiriki katika maonesho ya Kikanda Mbeya na Morogoro. 


Kaulimbiu ya mwaka huu ni ‘‘Tambua soko, Ongeza tija, Tekeleza Diira 2050

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...