Thursday, September 17, 2026

TANZANIA YAZINDUA WISER ACTIONFIRST™ KUIMARISHA TAHADHARI ZA MAPEMA KWA SEKTA ZA KILIMO NA MIFUGO

















Morogoro, 16 Septemba 2026

Tanzania imezindua rasmi programu ya WISER ActionFirst™ inayolenga kuimarisha matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika kuchukua hatua za mapema, hususan katika sekta za kilimo na mifugo, ili kupunguza athari za majanga yanayohusiana na hali ya hewa na tabianchi.


Uzinduzi huo umefanyika katika Ukumbi wa CATE Hotel, Morogoro, ukiambatana na Warsha ya Kitaifa ya Ushirikishwaji wa Wadau katika Kuandaa Taarifa Mahususi za Hali ya Hewa kwa Sekta za Kilimo na Mifugo, inayofanyika tarehe 16–18 Septemba 2026.


Akizindua rasmi programu hiyo na kufungua warsha, Mkurugenzi wa Idara ya Menejimenti ya Maafa, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Brigedia Jenerali Hosea Maloda Ndagala, alisema Tanzania inalenga kuimarisha mfumo wa tahadhari za mapema unaowezesha wananchi na taasisi kuchukua hatua kabla ya majanga kutokea.


Alisema kutoa utabiri pekee hakutoshi, bali kuna haja ya kueleza nini kifanyike. “Tunapaswa kutoka katika mfumo unaotuambia hali ya hewa inayotarajiwa kuwa vipi, kwenda kwenye mfumo unaotueleza hali hiyo inamaanisha nini, nini kifanyike, nani afanye, wapi na lini.”


Brigedia Jenerali Ndagala alisema kilimo na mifugo ni miongoni mwa sekta zilizo katika hatari kubwa kutokana na mafuriko, vipindi virefu vya ukavu, joto kali, upepo mkali, pamoja na wadudu na magonjwa yanayoathiriwa na hali hivyo, hatua za mapema zina umuhimu mkubwa katika kulinda uzalishaji, usalama wa chakula, maisha na mali, huku zikisaidia kupunguza gharama za kukabiliana na majanga baada ya kutokea.


Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Ofisi ya WMO Kanda ya Afrika, Dkt. Agnes Kijazi, alisema tukio hilo ni hatua muhimu katika safari ya Tanzania ya kuimarisha Utabiri Unaozingatia Hatua za kuchuka (Action-Based Forecasting – ABF).


Dkt. Kijazi alisisitiza, mchakato wa uandaaji shirikishi wa taarifa unalenga kuziba pengo kati ya taarifa za utabiri na hatua za mapema kwa kuimarisha ushirikiano kati ya huduma za hali ya hewa, huduma za kisekta, taasisi za menejimenti ya maafa, wadau wa maendeleo, wizara, vyombo vya habari na jamii zilizo katika hatari.


Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, Dkt. Geofrid Chikojo (Mkurugenzi wa Udhibiti na Ubora-TMA), alisema WISER ActionFirst™ itasaidia kuongeza matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika sekta za kilimo na mifugo.


Alisema TMA tayari inatoa Utabiri Unaozingatia Athari (Impact-Based Forecasting – IBF) kwa sekta mbalimbali, na mpango wa ActionFirst™ utasaidia kuendeleza msingi huo kwa kuhusisha watumiaji wa taarifa katika kuandaa taarifa zinazokidhi mahitaji yao.


“Ushirikishwaji wa wadau utasaidia kuboresha taarifa za tahadhari za mapema zinazolenga mahitaji ya sekta za kilimo na mifugo na kuongeza matumizi yake katika kufanya maamuzi”.Alisisitiza Dkt. Chikojo


Kwa upande wake, Mwakilishi wa WISER na UK Met Office, Bw. John Mungai, alifafanua kuwa ActionFirst™ inalenga kuhamisha mtazamo kutoka kwenye swali la “hali ya hewa itakuwaje?” kwenda kwenye maswali ya “hali hiyo ya hewa itafanya nini?” na “nini kinapaswa kufanyika?”


Programu hiyo inatekelezwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Ofisi ya Waziri Mkuu – Idara ya Menejimenti ya Maafa, pamoja na Serikali ya Uingereza kupitia Ofisi ya Mambo ya Nje, Jumuiya ya Madola na Maendeleo (FCDO), Taasisi ya Hali ya Hewa ya Uingereza (UK Met Office) na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO).

Wednesday, September 16, 2026

DKT CHANG’A NA KATIBU MKUU WMO WAZUNGUMZIA HALI YA EL NINO YA 2026

 


Geneva: 15 Septemba, 2026

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), na Makamu wa Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang’a alikutana na Katibu Mkuu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (World Meteorological Organization - WMO) Prof. Celeste Saulo na kufanya mazungumzo kuhusu uboreshaji wa huduma za hali ya hewa, hali ya El Nino 2026 na umuhimu wa kuendelea kuimarisha utoaji wa taarifa za mapema na maandalizi ya kukabiliana na athari zake. 



Prof. Saulo alimpongeza Dkt. Chang’a na kufurahishwa na namna TMA wanavyoendelea kusimamia vyema utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini Tanzania hususan katika kutoa elimu na kutahadharisha Umma na Wadau mbalimbali kuhusiana na hali ya El Nino na athari zake katika misimu ya mvua.  Aidha, Prof. Saulo ameahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuboresha huduma za hali ya hewa kupitia programu mbalimbali za WMO ikiwa ni pamoja na eneo la matumizi ya akiliunde (AI) katika mnyororo mzima wa utoaji wa huduma za hali ya hewa. 


“Napongeza juhudi za Tanzania katika utoaji wa huduma za hali ya hewa na elimu hususan katika kipindi hiki tunachokabiliwa na Hali ya El Nino yenye nguvu. Tanzania imekuwa mfano wa kuigwa na nimetumia Tanzania kama mfano mzuri wa utoaji wa elimu kuhusu El Nino na maandalizi ya kukabiliana na hali hiyo katika hotuba yangu ya hivi karibuni kuhusiana na hali inavyoendelea” Alisema Prof. Celeste Saulo.


Katika Kikao hicho, Dkt.Chang’a alimshukuru Katibu Mkuu wa WMO kwa kuendelea kuiamini Tanzania na TMA na kuendelea kuisaidia TMA kupitia programu zake mbalimbali za uboreshaji wa huduma za hali ya hewa kikanda na kitaifa ambazo zinatekelezwa kwa ushirikiano na Wadau wa Maendeleo na Nchi Wanachama wa WMO ambapo utekelezaji wake unaendelea vizuri. 


“Naendelea kushukuru sana kwa usaidizi wa WMO kupitia programu zake mbalimbali ambazo zinachangia pakubwa katika kuboresha huduma na utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini na nchi nyingine pia kuongeza nguvu katika uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika sekta ya hali ya hewa”.


Aidha, Dkt. Chang’a alimjulisha Katibu Mkuu wa WMO kuwa, kupitia programu za WMO, Tanzania imeweza kusaidia wataalamu wa hali ya hewa wa nchi nyingine kwa kutoa msaada wa kiufundi na miongoni mwa nchi hizo ni  Seychelles, Burundi, Sudan Kusini, na Namibia. Maeneo ambayo TMA imezisaidia nchi nyingine katika tasnia hii ya hali ya hewa ni pamoja na maeneo ya uboreshaji wa “Mfumo wa Usimamizi wa Ubora wa huduma na Umahiri wa Wataalamu (Quality Management System-QMS and Competency Assessment )”, “Utabiri wa Hali Mbaya ya Hewa (Severe Weather Forecasting)”, “Utabiri wa Hali ya Hewa kwa Kutumia Modeli za Kompyuta (Numerical Weather Prediction-NWP)”, “Mchakato wa kisheria katika sekta ya hali ya hewa (Legal Matters)” na Usambazaji wa Huduma za Hali ya Hewa kwa Umma (Public Weather Services-PWS). 

Vilevile Dkt. Chang’a alimshukuru Katibu Mkuu wa WMO kwa fursa ya kuleta mikutano mikubwa ya kitaalamu nchini ikiwa ni pamoja na mkutano wa nne (4) wa wataalamu wa matumizi ya huduma za hali ya hewa kwa sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi “The Fourth WMO Operational Climate Prediction (OCP-4)” uliofanyika Arusha mwishoni mwa mwezi Juni hadi mwanzo wa Julai 2026 kwa mara ya kwanza barani Afrika na kwa Tanzania na kwa ufanisi mkubwa. Tanzania , kupitia TMA itakuwa mwenyeji wa Mkutano wa nne wa wataalamu wabobezi wa sayansi ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi IPCC (IPCC WG1-LAM3) unaotarajiwa kufanyika Arusha mwanzoni mwa mwezi Novemba 2026.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...