Friday, August 7, 2026

KATIBU TAWALA MKOA WA TANGA AVUTIWA NA SAYANSI YA HALI YA HEWA.











Morogoro, Tarehe 06 Agosti 2026.

 

Katibu tawala wa Mkoa wa Tanga, Bw. Rashid Mchatta avutiwa na sayansi ya hali ya hewa, aliyasema hayo Tarehe 06 Agosti 2026 mara baada ya kupokea elimu ya hali ya hewa iliyokuwa inatolewa na wataalamu Bingwa wa Hali ya Hewa katika Jengo la Mamlaka lililopo katika Viwanja vya NaneNane, Morogoro kupitia maonesho ya NaneNane yanayoendelea kufanyika kuanzia tarehe 01 hadi 08 Agosti 2026.

 

“Sayansi ya hali ya hewa ukiifuatilia vizuri inavutia, lakini pia utaalamu wenu ni wa tofauti na sayansi nyingine, hivyo niwapongeze kwa kazi nzuri ya utabiri”.  Alisisitiza Bw. Mchatta.

 

Kupitia maonesho hayo yaliyokuwa na kauli mbiu “Tambua Soko, ongeza tija, tekeleza Dira 2050”, wageni wameendelea kupokea elimu mbalimbali ya hali ya hewa na kufahamu njia za usambazaji wa taarifa za Mamlaka, iliyopelekea wadau kuendelea kusajiliwa kupitia mifumo mbalimbali ya Mamlaka ili kuweza kupokea taarifa za hali ya hewa kidigitali.

 

Mamlaka inaendelea kuwaalika wadau mbalimbali kuendelea kutembelea katika mabanda ya TMA yaliyopo katika viwanja vya maonesho ya NaneNane, ambapo Kitaifa yanafanyika katika mkoa wa Dodoma na Kikanda ni katika mikoa ya Mbeya na Morogoro.

Tuesday, August 4, 2026

WATAALAM WA TANROADS WASISITIZWA KUZINGATIA MATUMIZI YA TAARIFA ZA HALI YA HEWA KATIKA KUPANGA NA KUTEKELEZA SHUGHULI ZA UJENZI

 





Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesisitiza umuhimu wa kuzingatia  matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa miundombinu ikiwemo barabara na madaraja . 


Akizungumza na viongozi na watumishi mbalimbali wa  Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS)- DODOMA, katika kikao kilichofanyika leo kati ya TMA na Menejimenti na Wataalamu wa TANROAD -Dodoma, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa ya Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt.Ladislaus Chang’a, alisema “Dunia inakabiliwa na changamoto ya kasi kubwa ya ongezeko la joto, idadi na ukubwa wa matukio ya hali mbaya ya hewa ikiwemo mvua kubwa, mafuriko, upepo mkali na ukame. Matukio haya ya hali mbaya ya hewa yanaendelea kuhatarisha maisha ya watu na mali zao, ikiwemo uharibifu wa miundombinu mbalimbali ikiwemo ya barabara na madaraja". 


Aidha, aliongeza kwa kusema kuwa mwaka huu 2026, dunia inakabiliwa na changamoto ya El Nino, ambayo inatarajiwa kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka. Mamlaka ya Hali ya Hewa inaendelea kufuatilia kwa karibu na itatoa taarifa ya kina kuhusu mwelekeo na athari za El-Nino 2026 tarehe 18/08/2026 wakati wa kutoa utabiri wa mvua za VULI. 


Dkt. Chang’a alisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya Mwaka 2019 katika matumizi ya taarifa na huduma za hali ya hewa katika sekta zote za kiuchumi na kijamii ili kuokoa maisha ya watu na mali zao, na pia kuongeza ufanisi na tija katika shughuli zote za kimaendeleo.


Hatua na mikutano hii ni mwendelezo wa mkakati wa kuhamasisha matumizi ya taarifa na  huduma za hali ya hewa katika mipango na maendeleo ya Taifa, hususan kipindi hiki ambapo Dunia kwa ujumla inakabiliwa na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa.

MAONESHO YA NANENANE YAWA CHANZO CHA ELIMU YA HALI YA HEWA KWA WADAU.

3 Agosti 2026, Dodoma.








Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inashiriki  katika maonesho ya NaneNane  2026 yanayofanyika  kuanzia tarehe 1 hadi 8 Agosti 2026,katika viwanja vya John Malecela, Nzunguni jijini Dodoma.


Maonesho hayo yanatoa fursa kwa wadau mbalimbali kupata elimu ya hali ya hewa, shughuli mbalimbali zinazotekelezwa na TMA,ikiwemo shughuli ya uthibiti na uratibu wa huduma za hali ya hewa nchini.


TMA inashiriki katika maonesho ya Kikanda Mbeya na Morogoro. 


Kaulimbiu ya mwaka huu ni ‘‘Tambua soko, Ongeza tija, Tekeleza Diira 2050

Tuesday, July 14, 2026

WATAALAMU WAKUTANA KUJADILI KUIMARISHA MIFUMO YA TAHADHARI ZA MAPEMA NA HUDUMA ZA HALI YA HEWA UKANDA WA MASHARIKI NA KUSINI MWA AFRIKA










ARUSHA, Tanzania, 13 Julai 2026:


Mkutano wa kikanda unaolenga kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema na huduma za hali ya hewa kwa Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika umefunguliwa rasmi leo tarehe 13 Julai 2026 jijini Arusha. 


 Mkutano huu unawakutanisha wataalamu wa hali ya hewa na wadau kutoka nchi mbalimbali katika Bara la Afrika kujadili na kuweka mikakati ya kuimarisha utoaji wa tahadhari za matukio ya hali mbaya ya hewa na kuimarisha huduma za hali ya hewa kwa ujumla.  Baadhi ya Nchi zinazo shiriki ni pamoja na Tanzania,  Kenya, Misri, Angola, Madagascar, Afrika Kusini n.k.


Mkutano huo umeandaliwa kwa ushirikiano wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Ofisi ya Hali ya Hewa ya Uingereza (UK Met Office) na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).


Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dkt. Ladislaus Chang'a, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kitaifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa naTabianchi (IPCC), alisisitiza umuhimu wa kuimarisha usambazaji na uzingatiaji wa taarifa za utabiri na tahadhari.  Vile vile, alibainisha kuwa, Mkutano wa 20 wa Baraza la Sekta ya Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa kwa Afrika Mashariki ulipitisha mapendekezo ya kuimarisha Taasisi za Kitaifa za Hali ya Hewa na kuchukua hatua stahiki ili kupunguza athari zinazoweza kusababishwa na El Nino 2026.


Kwa upande wake, Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi wa Ofisi ya Kanda ya Afrika ya WMO, alisisitiza kuwa hali ya hewa haina mipaka, na hivyo ushirikiano wa kimataifa ni muhimu sana. Alifafanua kuwa mkutano huo unalenga kuimarisha uratibu kati ya taasisi za kikanda ikiwemo Vituo Maalum vya Hali ya Hewa vya Kikanda ili kuongeza uwezo wao wa kusaidia Wanachama wa WMO katika kutoa huduma za hali ya hewa. "Hili ni jukumu kubwa ambalo haliwezi kutekelezwa bila kukuza ushirikiano wa kimataifa," alisisitiza Dkt. Kijazi.


Naye, Bi. Fionne Marshall, Kiongozi wa Kanda ya Afrika kutoka Ofisi ya Hali ya Hewa ya Uingereza, alitoa wito wa utabiri na tahadhari kuwa sahihi, zenye kuaminika, na zenye kutoa hatua stahiki zakuchukuliwa. "Haitoshi kujua kwamba mvua kubwa inakuja ikiwa watu hawaelewi athari kubwa zinaweza kutokea. "Haitoshi kutoa tahadhari ikiwa jamii hazipati, haziiamini, au hazijui hatua ya kuchukua," alisema Bi. Marshall, akiwataka taasisi kufanya kazi kwa mwelekeo mmoja wa kuelewa athari. 


Wawakilishi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AUC) walithibitisha majukumu yao katika kuimarisha mifumo ya tahadhari za mapema, huku Bw. James Kivuva wa EAC akibainisha kuwa uratibu bado ni pengo muhimu ambalo lazima lifanyiwe kazi na lifungwe. Naye, Dkt. Jolly Wasambo wa AUC alisisitiza dhamira ya bara kama ilivyoainishwa katika Agenda 2063, akisisitiza kwamba hali ya joto duniani inavyoendelea kuongezeka ndivyo ulazima wa kuimarisha mifumo ya tahadhari mapema unavyohitajika kwaajili ya jamii salama.

 

Kuanzia tarehe 13 hadi 17, washiriki watajadili namna ya kuimarisha vituo vya kikanda, kuimarisha Taasisi za Kitaifa za Hali ya Hewa, kuimarisha utabiri unaozingatia athari kwa ajili ya El Nino 2026, na kuimarisha ushirikiano katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) na Akili Unde.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...