Friday, June 26, 2020

WATAALAMU WA HALI YA HEWA WATAKIWA KUJENGEWA UWEZO KATIKA UTOAJI WA HUDUMA ZA HALI YA HEWA KWA WATUMIAJI WA BAHARI

Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO, Dkt. Agnes Kijazi akichangia katika mjadala kwenye mkutano wa “WMO-IOC Joint Collaborative Board” uliofanyika tarehe 16 Juni, 2020  kuhusiana na vipaumbele vya maeneo ya ushirikiano kati ya WMO na IOC.

Baadhi ya washiriki wa mkutano wa “WMO-IOC Joint Collaborative Board” uliofanyika tarehe 16 Juni, 2020 wakichangia mijadala katika mkutano huo. Washiriki walio pichani kutoka upande wa kushoto ni mratibu wa Mkutano Bi. Sarah Grimes kutoka Sekretarieti ya  Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Mwenyekiti Mwenza wa WMO-IOC Joint Collaborative Board”, Dkt. Louis Uccellin, ambaye pia ni Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Hali ya Hewa ya Marekani na Bi. Monika Breuch-Moritz, ambaye ni Afisa kutoka Sekretarieti ya IOC.

Dar es Salaam; 

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi amesisitiza  kwamba suala la kuwajengea uwezo wataalamu wa hali ya hewa wanaotoa huduma kwa watumiaji wa bahari ni la umuhimu wa kipekee ili kuweza kukidhi mahitaji ya wadau hao wa bahari. 


Amezungumza hayo wakati akishiriki katika mkutano wa Bodi ya Mashirikiano kati ya WMO na Kamisheni ya Kimataifa ya Masuala ya Huduma za Hali ya Hewa kwa watumiaji wa Bahari (WMO-Intergovernmental Oceanographic Commission Collaborative Board (WMO-IOC JCB)) uliofanyika tarehe 16 Juni, 2020 kwa njia ya mtandao (videoconference). 


“Taasisi nyingi za Hali ya Hewa zina vituo vya kufuatilia hali ya bahari na kutoa huduma kwa wadau, lakini wataalamu bado hawajapewa ujuzi wa kutosha kuhusiana na mahitaji ya wadau. Hivyo tunahitaji kushughulikia masuala muhimu ya kisera na kimkakati yatakayowezesha kujenga uwezo kwa wataalamu katika ngazi ya nchi, kwani wataalamu hao bado hawajapewa elimu na ujuzi wa kutosha kukidhi mahitaji ya wadau wa bahari wanaowahudumia”. Alisema Dkt. Kijazi.


Aidha, Dkt. Kijazi alitaja kipaumbele kingine kuwa ni kuimarishwa kwa miundombinu ya upimaji na ufuatiliaji katika maeneo ya bahari ili kuwezesha upatikanaji wa takwimu ambazo ni muhimu katika utoaji wa huduma katika sekta hii, pamoja na ushirikiano kati ya taasisi husika kuanzia ngazi ya nchi.


Bodi ya mashirikiano katika ya WMO na IOC (WMO-IOC Joint Collaborative Board) huratibu maeneo ya mashirikiano kati ya WMO na IOC, na kwa sasa pamoja na masuala mengine itashughulikia pia suala la kujenga uwezo katika maeneo ya mashirikiano. Miongoni mwa masuala yaliyojadiliwa katika mkutano huo ni pamoja rasimu ya mkakati wa miaka kumi (10) wa kujenga uwezo, ambao utahusisha utaratibu wa kufanya kazi pamoja; utaratibu wa kushirikiana na washirika wengine; na uendelevu katika shughuli za kujenga uwezo. 


Bodi hiyo ilikutana kwa lengo la kujadili vipaumbele vya maeneo ya ushirikiano yanayohitaji kujengewa uwezo, ambayo yatashughulikiwa na majopo ya kujenga uwezo ya WMO na IOC. Dkt. Kijazi ni  Mwenyekiti wa Jopo la WMO la kujenga uwezo (WMO Capacity Development Panel).

TMA KUWA MSTARI WA MBELE KUSAIDIA HUDUMA ZA HALI YA HEWA KATIKA NCHI ZA AFRIKA


Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Kanda ya Afrika, Dkt. Daouda Konate (kushoto aliyevaa miwani) aliyekuwa Mwenyekiti wa Kikao akimsikiliza Katibu Mkuu wa WMO, Prof. Petteri Taalas (kushoto aliyekaa katikati ya wataalamu) akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za WMO katika Kanda ya Afrika (RA I) katika Mkutano wa viongozi wa WMO Kanda ya Afrika (WMO Regional Association I Management Group) uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 10 hadi 12 Juni 2020.

Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi akichangia katika taarifa ya utekelezaji wa shughuli za WMO katika Kanda ya Afrika (RA I) iliyowasilishwa na Katibu Mkuu wa WMO, Prof. Petteri Taalas katika  Mkutano wa viongozi wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Kanda ya Afrika (WMO Regional Association I Management Group) uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 10 hadi 12 Juni 2020.

Dar es Salaam; 
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema iko tayari kushirikiana na Taasisi za Hali ya Hewa za Nchi  Wanachama wa Shirika la Hali ya Hewa  Duniani (WMO) Kanda ya Afrika (WMO Regional Association  I (RA I), kusaidia kuboresha huduma za hali ya hewa katika maeneo ambayo imekwisha kupiga hatua zaidi. Hayo yalisemwa katika Mkutano wa Viongozi wa WMO Kanda ya Afrika (RA I Management Group), uliofanyika kwa njia ya mtandao (videoconference) kuanzia tarehe 10 hadi  12 Juni, 2020.

Akizungumza wakati akichangia taarifa ya utekelezaji wa shughuli za WMO katika Kanda ya Afrika iliyowasilishwa na Katibu Mkuu wa WMO Prof. Petteri Taalas, Mkurugenzi Mkuu wa TMA ambaye pia ni Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa  Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi alieleza kwamba Tanzania imepiga hatua katika uandaaji wa majarida ya taarifa za klaimatolojia (hali ya hewa ya muda mrefu) kwa nchi ya Tanzania, hivyo iko tayari kusaidia nchi nyingine Wanachama wa WMO Kanda ya Afrika.
“Kuhusiana na uandaaji wa taarifa za klaimatolojia (hali ya hewa ya muda mrefu), nafurahi kusema kwamba Tanzania tumekwishaanza kutoa machapisho hayo tangu mwaka 2011 na tuko tayari kusaidia katika ngazi ya Kanda”. Alisema Dkt. Kijazi.

Aidha, aliendelea kusisitiza utayari wa Tanzania katika kusaidia nchi zingine wakati akielezea faidi za kuwa na Mfumo wa Kitaifa wa Huduma za Hali ya Hewa (National Framework for Climate Services) ambapo alisema kwa upande wa Tanzania, mfumo huo umesaidia kuboresha sana huduma za hali ya hewa. Moja ya uboreshaji huo ni  kutungwa kwa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Na. 2 ya mwaka 2019 ambayo ina malengo ya kuiwezesha TMA kusimamia vyema huduma zote za hali ya hewa zinazotolewa nchini Tanzania na hivyo kutekeleza vyema program zote za WMO kwa ustawi wa wananchi wa Tanzania na dunia kwa ujumla hasa ikizingatiwa kwamba hali ya hewa haina mipaka. Aliongeza Dr. Kijazi.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa WMO alimpongeza Dr. Kijazi kwa umahiri anaoonyesha katika kushiriki kwenye program za WMO katika nafasi yake kama Mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika Shrika la Hali ya Hewa Duniani na kama Makamu wa tatu wa rais wa shirika hilo. Aidha, aliipongeza Tanzania kuwa imefanya kazi kubwa katika kutekeleza program za WMO ikiwemo program ya Global Framework for Climate services na akasema WMO inafurahishwa na utayari wa Tanzania kusaidia nchi zingine barani  Afrika.

Kwa upande mwingine, Mkurugenzi wa WMO Ofisi ya Kanda ya Afrika, Dkt. Amos Makarau alitoa taarifa ya wataalamu walioteuliwa kuongoza majopo na vikosi kazi mbalimbali vya WMO, ambapo taarifa hiyo ilibainisha uteuzi wa Mkurugenzi wa Miundombinu na Huduma za Ufundi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, Dkt. Pascal Waniha kuwa Makamu Mwenyekiti (Vice Chair) wa   Kikosi Kazi cha Mtandao wa Dunia wa Upimaji wa Hali ya Hewa (Study Group on Global Basic Observing Network (GBON), akiwa miongoni mwa wataalamu watatu (3) walioteuliwa kutoka Afrika kuongoza majopo na vikosi kazi vya WMO.  Hii ni sifa na heshima kwa Tanzania na TMA.

Awali akifungua mkutano huo, Mwenyekiti ambaye ni Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Kanda ya Afrika, Dkt. Daouda Konate kutoka Ivory Coast alisema lengo la mkutano ni kujadili utekelezaji wa shughuli za huduma za hali ya hewa katika Kanda ya Afrika. Mkutano ulijadili masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na shughuli za WMO katika Kanda ya Afrika; utekelezaji wa maazimio ya Mkutano Mkuu wa WMO (WMO Congress) wa mwezi Juni, 2019; Uteuzi wa wataalamu katika majopo na vikosikazi vya WMO; Vipaumbele vya Kanda; Mpango Mkakati wa Kanda; na athari za janga la ugonjwa wa “COVID-19” katika huduma za hali ya hewa. 

Aidha, baada ya majidiliano ya kina, mkutano ulikuja na  mapendekezo ambayo  ni pamoja na: kutoa nafasi kwa watunga sera kushiriki katika mikutano ya Kanda ya Masuala ya hali ya hewa; na kuziomba Nchi Wanachama kuridhia katiba ya Kamati ya Mawaziri wenye dhamana ya hali ya hewa “African Ministerial Conference on Meteorology (AMCOMET).

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...