Thursday, December 7, 2023

USHIRIKI WA TMA KATIKA MKUTANO WA 16 WA JTSR







Mwakalishi wa Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ambaye pia ni Mkurugenzi wa Muundombinu ya Hali ya Hewa, Dkt. Pascal Waniha akiwasilisha taarifa ya sekta ya hali ya hewa katika mkutano wa 16 wa JTSR.

Aidha, aliwasilisha pia mada ya namna teknolojia na ubunifu katika sekta ya hali ya hewa  inavyochangia usalama wa usafiri katika sekta ya Uchukuzi.

28th SESSION OF THE CONFERENCE OF THE PARTIES (COP 28) UEA


 IPCC vice- Chair Dkt. Ladislaus Chang'a spoke at the Children and Youth Pavilion at #COP28 today.

Calling on the youth and young scientists to play a greater role in the IPCC process.

" Youth are the agent of change and therefore play a critical role"

MHE. PROF MAKAME MBARAWA ATEMBELEA BANDA LA TMA



 Waziri wa Uchukuzi Mhe.Prof.Makame Mbarawa ametembelea banda la Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na kutoa maagizo juu ya usimamizi wa miradi ya rada za hali ya hewa, kwenye maonesho ya mkutano wa 16 wa wadau wa Sekta ya Uchukuzi kuhusu ufuatiliaji na tathimini, unaofanyika jijini Arusha tarehe 05 hadi 08 Disemba, 2023.

Tuesday, December 5, 2023

KATIBU MKUU UCHUKUZI AAGIZA TMA KUTANGAZA MAFANIKIO KIKANDA

 




Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius. W. Kahyarara ametembelea banda la maonesho la TMA katika Mkutano wa 16 wa Wadau wa Sekta ya Uchukuzi kuhusu Ufuatiliaji na Tathmini (16th JTSR) unaofanyika jijini Arusha, tarehe 05 hadi 08 Desemba 2023 na kuagiza Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kutangaza mafanikio ya taasisi yanayopatikana kikanda, kimataifa pamoja na mafanikio yanayopatikana katika utekelezaji wa majukumu ya Taasisi. Katibu Mkuu pia ameisifu TMA kuwa ni taasisi inayofanya kazi nzuri na yenye mafanikio kitaifa na kimataifa.

Katibu Mkuu amesisitiza kuwa “ni wakati sasa, jamii ikatambua mafanikio ya TMA kikanda na kimataifa, natambua kuwa taasisi hii inafanya kazi nzuri inayoonekana, ni vyema kujipanga kuwa na vipindi katika televisheni na kueleza mafanikio hayo”. Alizungumza Prof. Godius. W. Kahyarara, wakati akitembelea mabanda ya maonesho ya wadau wa sekta ya Uchukuzi. Aidha, Katibu Mkuu aliitaka Wizara kusimamia program ya kutangaza mafanikio ya Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Uchukuzi kwa kuanza na TMA.

Naye, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu TMA ambaye pia ni Mkurugenzi wa Huduma za Miundombinu na Ufundi, Dkt. Pascal Waniha, alieleza kuwa TMA imekuwa kielelezo bora katika ukanda wa Afrika Mashariki pamoja na nje ya Kanda. “Kazi kubwa imeendelea kufanyika katika kuiwakilisha nchi vizuri kwenye masuala ya hali ya hewa kimataifa na kueleza kuwa imeteuliwa na WMO kuwa muandaaji wa mafunzo ya rada katika Kanda ya Afrika yanayoratibiwa na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO). Fursa hii imepatikana kutokana na uwekezaji mkubwa wa miundombinu ya hali ya hewa unaoendelea kufanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania”. Alisema Dkt. Waniha.

Mafanikio mengine yaliyoelezwa mbele ya Katibu Mkuu kupitia mabango ni pamoja na maendeleo katika shughuli za uangazi, ununuzi wa vifaa na mitambo ya hali ya hewa, udhibiti wa huduma za hali ya hewa pamoja na njia mbalimbali zinazotumika katika kusambaza taarifa za hali ya hewa kwa jamii na kwa sekta mahsusi.


Saturday, November 25, 2023

DKT. CHANG’A APEWA JUKUMU LA KUSIMAMIA BODI YA SAYANSI KATIKA JOPO LA KIMATAIFA LA SAYANSI YA MABADILIKO YA HALI YA HEWA NA TABIANCHI (IPCC)

 




Geneva, Uswisi: Tarehe 22/11/2023

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi “Intergovernmental Panel on Climate Change (IPCC)”, Dkt. Ladislaus Chang’a, amepewa jukumu la kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Sayansi katika Jopo la IPCC. 

Dkt. Chang’a alipewa jukumu hilo katika mkutano wa 66 wa viongozi wa Jopo la IPCC (Sixty-sixth IPCC Bureau) uliofanyika Geneva, Uswiss tarehe 15 na 16 Novemba, 2023. Lengo kuu la mkutano huo lilikuwa ni kujadili maandalizi ya utekelezaji wa shughuli za IPCC katika Tathmini ya Saba ya IPCC ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC Seventh Assessment Cycle - AR7). Mkutano huo ni wa kwanza tangu uongozi mpya wa IPCC uchaguliwe katika uchaguzi uliofanyika mwezi Julai 2023. Uongozi wa IPCC una jumla ya viongozi thelathini na nne (34), Dkt. Chang’a ni miongoni mwa viongozi hao ambapo alichaguliwa katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti akiwa miongoni mwa Makamu Wenyeviti watatu wa IPCC.

Bodi ya Sayansi ya IPCC atakayoisimamia Dkt. Chang’a inaundwa na Makamu Wenyeviti wote watatu wa IPCC ambao ni Dkt. Ladislaus Chang’a (Tanzania), Prof. Ramón Pichs-Madruga (Cuba), na Prof. Diana Ãœrge-Vorsatz (Hungary). Miongoni mwa shughuli zitakazoambatana na jukumu hilo jipya alilopewa Dkt. Chang’a ni: kusimamia programu ya IPCC ya ufadhili wa mafunzo (IPCC Scholarship Programme); kuratibu ushiriki wa wanasayansi chipukizi (Young Scientists) katika masuala ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi; na kuwakilisha jopo la IPCC katika programu ya WMO ya utafiti “(World Weather Research Programme (WWRP) ”. 

Jukumu jipya alilopewa Dkt. Chang’a la kusimamia Bodi ya Sayansi ya Jopo la IPCC pamoja na fursa za mpya za mashirikiano na WMO ni mwendelezo wa kuaminika kwa TMA na Tanzania kimataifa. Hii inatokana na mchango mzuri unaotolewa na wataalamu wa TMA katika nafasi mbalimbali wanazohudumu, ikiwa ni pamoja na vikosikazi vya WMO. Mafanikio haya yanaendelea kuitangaza Tanzania kimataifa na kuimarisha zaidi mahusiano mazuri ya kidiplomasia kati ya Tanzania na nyingine katika utoaji wa huduma za hali ya hewa.

Katika hatua nyingine, Dkt. Chang’a alishiriki katika mkutano wa kuwajengea uwezo Wawakilishi wapya wa Kudumu wa Nchi katika WMO (Permanent Representatives of Members with WMO) uliofanyika Geneva, Uswis kuanzia tarehe 20 hadi 22 Novemba, 2023. Kupitia mkutano huo, alipata pia fursa ya kukutana na baadhi ya viongozi katika vitengo vya WMO ambapo walijadili maeneo mapya ya ushirikiano na TMA kupitia programu za WMO, ikiwa ni pamoja na WMO kutambua mifumo iliyobuniwa na wataalamu wa TMA ili itumike katika huduma za hali ya hewa. 

IPCC ni Chombo cha Umoja wa Mataifa kinachosimamiwa na WMO na Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira (United Nations Environmental Programme- UNEP). Chombo hicho kilianzishwa mwaka 1988 kwa jikumu la kusimamia sayansi ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi ambapo Jopo hilo hufanya tathmini za mwenendo wa Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi na kuandaa taarifa za tathmini (Climate Change Assessment Reports) ambazo zina mchango muhimu katika kufanya maamuzi ya kukabiliana na madhara yanayosababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi. Tangu kuanzishwa kwake, IPCC imeandaa taarifa sita za tathmini, ambapo tathmini ya sita (IPCC Sixth Assessment cycle) ilianza mwaka 2015 na kukamilika mwaka 2022. Uongozi mpya wa IPCC utasimamia Tathmini ya Saba ya IPCC ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi inayotarajiwa kuanza mapema mwaka 2024 na kukamilika mwaka 2030.

Thursday, November 23, 2023

WADAU WA MAZINGIRA WAPATA ELIMU YA HUDUMA MAHSUSI ZITOLEWAZO NA TMA

 




Matukio mbalimbali kwa picha kupitia jukwaa la mkutano mkuu wa tano wa mwaka wa Chama cha Wataalam wa Mazingira Tanzania (TEEA) pamoja na maonesho ya bidhaa na teknolojia za "Eco - Friendly" uliofanyika katika ukumbi wa Maktaba ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), tarehe 22 Novemba 2023.


Tuesday, October 31, 2023

TMA YATOA RASMI UTABIRI WA MVUA MAENEO YANAYOPATA MSIMU MMOJA KWA MWAKA.



Dar es Salaam; Tarehe 31 Oktoba, 2023;

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi mwelekeo wa mvua za Msimu kwa maeneo yanayopata msimu mmoja wa mvua kwa mwaka ambayo ni mikoa ya  Tabora, Katavi, Kigoma, Singida, Dodoma, Rukwa, Songwe, Mbeya, Iringa, Njombe, Lindi, Mtwara, Ruvuma na  na Kusini mwa Morogoro. Taarifa hiyo imesema  kipindi cha nusu ya msimu (Novemba 2023 hadi Januari, 2024) kinatarajiwa kuwa na mvua nyingi ukilinganisha na nusu ya pili (Februari hadi Aprili 2024), uwepo wa El-Niño unatarajiwa kuwa na mchango mkubwa katika mvua za Msimu.

“Mvua za Juu ya Wastani hadi Wastani zinatarajiwa katika maeneo ya kusini mwa mkoa wa Morogoro, mikoa ya Iringa, Lindi, Mtwara, Singida, Dodoma, kaskazini mwa mkoa wa Katavi, Kigoma na Tabora. Aidha, mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani zinatarajiwa kusini mwa mkoa wa Katavi, mikoa ya Njombe, Rukwa, Songwe, Mbeya na Ruvuma”. Alisema Dkt. Ladislaus Chang’a, Kaimu Mkurugenzi Mkuu TMA na Makamu Mwenyekiti Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabia Nchi (IPCC) wakati wa mkutano na vyombo vya habari kuhusiana na mwelekeo wa mvua za Msimu, katika ukumbi wa Ubungo Plaza, Dar es Salaam,Tarehe 31 Oktoba, 2023. 

Dkt. Chang’a alibainisha athari zinazoweza kujitokeza ikiwa ni vipindi vya unyevu wa kuzidi kiasi pamoja na mafuriko vinaweza kujitokeza na kuathiri ukuaji wa mazao na miundombinu ya kilimo, vile vile, kina cha maji katika mito na mabwawa kinatarajiwa kuongezeka, aidha, Dkt. Chang’a alitoa ushauri kwa wadau mbalimbali kuzingatia matumizi endelevu ya uhifadhi wa rasimali maji.

Katika hatua nyingine, Dkt. Chang’a alifafanua kuwa Msimu wa Vuli kwa miezi ya Oktoba hadi Disemba, 2023 katika maeneo yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka (Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Mara, Manyara, Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Dar es Salaam, kaskazini mwa mkoa wa Morogoro, Pwani (ikijumuisha kisiwa cha Mafia) pamoja na Zanzibar (visiwa vya Unguja na Pemba) utabiri wake ulitolewa tarehe 24 Agosti, 2023. Mvua hizo zimeshaanza katika maeneo ya ukanda wa Ziwa Victoria, pwani ya kaskazini na baadhi ya maeneo ya nyanda za juu kaskazini mashariki kama ilivyotabiriwa. Aidha, ongezeko la mvua linatarajiwa katika miezi ya Novemba na Disemba, 2023. Vilevile, mvua za nje ya msimu zinatarajiwa katika mwezi Januari na Februari, 2024.

Kwa taarifa zaidi tembelea: www.meteo.go.tz

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...