Thursday, December 19, 2019

TMA YAWEKA MSISITIZO WA KUKABILIANA NA CHANGAMOTO ZA MABADILIKO YA HALI YA HEWA BAHARINI.

Dkt. Agnes  Kijazi, akitoa mada kuhusu umuhimu wa kuzijengea uwezo mamlaka za hali ya hewa katika nchi wanachama wa shirika la hali ya hewa duniani.

Dkt. Agnes  Kijazi,  akishiriki katika jopo la majadiliano kuhusiana na  matukio ya hali mbaya ya hewa yanayojitokeza ikiwemo vimbunga katika bahari.

Dkt. Agnes Kijazi, akitoa mada kuhusiana na mahusiano ya masuala ya Jinsia na changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa.

Kutokea kulia ni Dkt. Agnes Kijazi akifuatiwa na Mwenyekiti wa IPCC Profesa. Hoesung Leena pamoja na Dkt. Ladislaus Chang’a katika picha ya pamoja wakati wa majadiliano kuhusiana na maandalizi ya ripoti ya sita ya tathmini ya mabadiliko ya hali ya hewa inayotarajiwa kukamilishwa mwaka 2022.

Dkt. Ladislaus Chang’a (kulia) akishiriki katika majadiliano kuhusiana na maandalizi ya Ripoti ya sita ya tathmini ya mabadiliko ya hali ya hewa inayotarajiwa kukamilishwa mwaka 2022.



Katibu Mkuu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Prof. Petteri Taalas (wa pili kutoka kulia) wakijadiliana na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ambaye pia ni Makamu wa tatu wa Rais wa  Shirika la Hali ya Hewa Duniani, Dkt. Agnes Kijazi, wakiwa pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Uganda pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa  Malawi (wa kwanza kutoka kushoto) mara baada ya kusainiwa kwa makubaliano ya kuimarisha huduma za hali ya hewa katika nchi zinazoendelea baina ya shirika la hali ya hewa duniani na taasisi za kibenki na mashirika mengine ya kimataifa yakiwemo, UNDP, AfDB, WFP.

Madrid, Hispania Tarehe 13/12/2019;
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imeshiriki Mkutano wa 25 wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Hali ya Hewa (2019 United Nations Framework Convention on Climate Change-UNFCCC-COP25) uliofanyika tarehe 02-13 Disemba 2019 nchini Hispania.

Pamoja na kutoa mchango na ushauri katika sayansi ya hali ya hewa kwa ujumbe wa Tanzania ulioshiriki katika Mkutano huo, TMA ilishiriki pia katika mikutano iliyofanyika sambamba na Mkutano huo wa UNFCCC-COP25, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi, alishiriki kutoa mada na baadae katika jopo la majadiliano kuhusiana na umuhimu wa kujenga uwezo na kuimarisha huduma za hali ya hewa, hususan katika nchi zinazoendelea sambamba na kuweka msisitizo wa kuhakikisha dunia inaongeza jitihada za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa katika maeneo ya bahari na yaliyo kandokando ya bahari.

“Kumekuwa na ongezeko la kina cha bahari, ongezeko kubwa la vimbunga kwa upande wa Afrika, mfano kimbunga IDAI kilishosababisha vifo vya mamia ya watu na kuharibu mazao na makazi ya watu katika nchi za Msumbiji, Zimbabwe na Malawi, hii inaonesha kuwa changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa ni halisia, ni vyema tukachukua hatua stahiki sasa”. Alisema Dkt. Kijazi. 

Kwa upande mwingine, Dkt Kijazi alishiriki kutoa mada kuhusiana na masula ya jinsia na changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa. Dkt. Kijazi, alisisitiza kuwa kuna tofauti kubwa ya namnna ambavyo mabadiliko ya hali ya hewa yanawaathiri wanawake, watoto, wazee na wanaume. Wanawake, watoto na wazee wanaathirika zaidi na mabadiliko ya hali ya hewa hasa katika nchi zinazoendelea kutokana na nafasi na shughuli zao katika jamii. Dkt. Kijazi aliitaka jumuiya ya kimataifa kufuata mfano wa Tanzania katika kutoa nafasi kwa wanawake katika nafasi za maamuzi, ambapo Makamu wa Rais wa Tanzania ni mwanamke, Naibu Spika ni mwanamke na akasema vilevile na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa ni mwanamke ambaye ni yeye mwenyewe.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi wa Utafiti na Matumizi kutoka TMA alielezea umuhimu wa kuimarisha uangazi na uboreshaji wa huduma za hali ya Hewa katika bara la Afrika na nchi zinazoendelea pamoja na kushiriki katika jopo la majadiliano kuhusiana na maandalizi ya ripoti ya sita ya tathmini ya mabadiliko ya hali ya hewa duniani, ambapo tayari kuna ripoti maalamu tatu zimetolewa na maandalizi yanaendelea kukamilisha ripoti kuu nne na zinatarajiwa kukamilika mwaka 2022.

Aidha, TMA ilishiriki pia hafla ya WMO ya kusaini ushirikiano na  washirika wa maendeleo katika uboreshaji wa huduma za hali ya hewa (Alliance for Hydromet). Hafla hiyo ilimshirikisha Katibu Mkuu wa WMO, Prof. Petteri Taalas, viongozi mbalimbali wa WMO na viongozi wa Taasisi za Hali ya Hewa-Afrika ikiwemo Malawi, Uganda na Tanzania.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...