Monday, November 29, 2021

DKT. NYENZI AIAGIZA TMA KUSIMAMIA SHERIA KIKAMILIFU.


Mgeni Rasmi na Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Buruhani Nyenzi wakati akifungua rasmi Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), lililofanyika katika Ukumbi wa Magadu, Morogoro.



Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Dkt. Agnes Kijazi akiongea wakati wa ufunguzi Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), lililofanyika katika Ukumbi wa Magadu, Morogoro.


Washiriki mbalimbali wa Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kwenye picha ya pamoja na Mgeni rasmi  katika Ukumbi wa Magadu, Morogoro.

Washiriki mbalimbali wa Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA)wakati wa ufunguzi wa Baraza la Wafanyakazi wa TMA katika Ukumbi wa Magadu, Morogoro.

Morogoro, Tarehe: 29/11/2021;

Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Buruhani Nyenzi ameiagiza TMA kusimamia sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya Mwaka 2019 kikamilifu. Alizungumza hayo wakati akifungua rasmi Baraza la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), lililofanyika katika Ukumbi wa Magadu, Morogoro, tarehe 29/11/2021.

 

“Nawaagiza mkasimamie Sheria hii kikamilifu ikiwa ni pamoja na ukusanyaji wa mapato katika maeneo yaliyoainishwa. Hii itasaidia kuwezesha utekelezaji wa majukumu yenu kwa ufanisi mkubwa pamoja na kutatua changamoto mbali mbali zilizo katika uwezo wenu”.Alisema Dkt. Nyenzi

 

“Nimejulishwa pia kuwa ili kutekeleza sheria iliyoanzisha taasisi hii mmefanikiwa kuandaa kanuni zitakazowezesha utekelezaji wa sheria hiyo. Katika eneo hili, niwapongeze kwa kukamilika kwa Kanuni saba za Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya mwaka 2019 ikiwemo Kanuni ya Tozo, natambua kuwa kanuni hizi zimeshasainiwa, kilichobaki ni utekelezaji wake”.Alizungumza Dkt. Nyenzi.

 

Aidha, Dkt. Nyenzi aliipongeza TMA kwa kazi nzuri inayofanyika na kuwataka kuchapa kazi kwa bidii na kuendelea kutoa taarifa kwa watoa maamuzi ili kusaidia ufanyaji wa maamuzi na kuwezesha Serikali kukabiliana na changamoto zinazosababishwa na matukio ya hali mbaya ya hewa ambayo yanazidi kuongezeka kutokana na mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumzia ushiriki wa TMA katika Mkutano mkubwa wa COP26 ambao Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alishiriki na kuhutubia mkutano huo. Alisema, anatambua katika maazimio ya mkutano huo TMA inajukumu la kufanya ili kufanikisha jitihada za kuhimili athari za mabadiliko ya tabia nchi, hivyo, jukumu hilo litatimizwa vyema kwani TMA ina wataalamu wanaokubalika kimataifa wakiwemo wajumbe katika kamati mbali mbali za Shirika la Hali ya Hewa Duniani na Mwenyekiti wa Baraza hili ambaye ni Makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani.Aliongeza Dkt. Nyenzi.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Dkt. Agnes Kijazi aliishukuru Serikali na kueleza madhumuni maalum ya Baraza hilo ni kufanya tathmini ya utendaji wa Mamlaka, tathmini ambayo itasaidia kuongeza ubora na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa umma kwa lengo la kupunguza athari za mabadiliko ya hali ya hewa na tabia nchi.

“Hivi karibuni tumeshuhudia athari mbalimbali zitokanazo na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi ikiwa ni pamoja na kuwa na vipindi vya ongezeko la joto hadi kufikia nyuzi joto 35.6 kwa maeneo ya ukanda wa Pwani. Aidha, nichukuwe fursa hii kuendelea kutoa wito kwa watanzania wenzangu kuendelea kufuatilia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kila mara ili kupunguza madhara yatokanayo na hali mbaya ya hewa”.Alifafanua Dkt. Kijazi.

Vile vile, Dkt. Kijazi alieleza baadhi ya changamoto  ni mishahara midogo hali inayopelekea wataalamu kuhamia katika Taasisi zingine, hata hivyo ‘Job Evaluation’ ilishafanyika ambayo TMA inaendelea kusubiri idhini ya kutekeleza mapendekezo yaliyotolewa. 

Tuesday, November 9, 2021

COP26: TANZANIA NA MKAKATI WA KUBORESHA HUDUMA ZA HALI YA HEWA NCHINI

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Selemani Jafo na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais – Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mhe. Dkt. Saada Mkuya (Wanne kutoka kulia) katika picha ya pamoja na Katibu Mkuu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Prof. Petteri Taalas. Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ambaye pia ni Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO (wa kwanza kushoto) na Wakurugenzi wa Mazingira kutoka Zanzibar Bi. Farhat Mbarouk na Dkt. Andrew Komba kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais.


Dkt. Saada Mkuya, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais – SMZ akizungumza wakati wa tukio la uzinduzi wa programu ya WMO ya SOFF.

Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ambaye pia ni Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO, akiwasilisha mada katika jopo la “High-level launch of the Climate Science Information for Climate Action Initiative”.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi na Mkurugenzi wa TMA Ofisi ya Zanzibar, Bw. Mohammed Ngwali (watatu kutoka kulia) katika picha ya pamoja na Ujumbe wa Burundi uliojumuisha Katibu Mkuu wa Wizara yenye dhamana ya mazingira Burundi, Bw. Emmanuel Ndorimana (wa kwanza kushoto) na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Hali ya Hewa ya Burundi, Bw. Deogratius Babonwanayo (Wapili kushoto) na Mjumbe kutoka Wizara ya Mazingira Burundi (Wa kwanza Kulia). 




 Glasgow; Tarehe 07/11/2021

Tanzania imeendelea kushiriki katika Mkutano wa 26 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (COP26) unaoendelea Glasgow, Uingereza, ambapo viongozi mbalimbali wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar akiwemo mheshimiwa Rais na mawaziri wameshiriki. Kwa upande wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), iliwakilishwa na Mkurugenzi Mkuu na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi pamoja na Wataalamu wa TMA.

Katika hatua za kuhakikisha huduma za hali ya hewa zinaendelea kuboreshwa kwa manufaa ya nchi, Mhe. Dkt. Saada Mkuya, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais – Serikali ya Mapinduzi Zanzibar alipata fursa ya kuzungumza na washiriki wakati wa tukio la uzinduzi wa programu ya Shirika la Hali ya Hewa Duniani ya “Systematic Observation Financing Facility (SOFF)” ambapo alielezea umuhimu wa program hiyo kwa nchi zinazoendelea pamoja na Tanzania ambazo uchumi wake kwa asilimia kubwa hutegemea zaidi kilimo.

Aidha katika hatua nyingine, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Selemani Jafo pamoja na Mhe. Dkt. Saada Mkuya, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais – Serikali ya Mapinduzi Zanzibar walifanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Prof. Petteri Taalas ambapo walishukuru ushirikiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na Shirika hilo kupitia utekelezaji wa programu mbalimbali ikiwemo changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa. Kwa upande wake Prof. Taalas aliwashukuru Waheshimiwa Mawaziri kwa kuwezesha ushiriki wa TMA katika utekelezaji wa programu hizo za WMO ikiwa ni pamoja na kazi anayofanya Dkt. Agnes Kijazi katika nafasi yake kama Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO. Ujumbe wa Tanzania ulitambulishwa na Mkurugenzi Mkuu wa TMA ambaye pia ni Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO Dkt. Agnes Kijazi. 

Kwa upande wa TMA, Dkt. Kijazi alikuwa miongoni mwa washiriki katika jopo (High level Panelist) la kujadili umuhimu wa sayansi na taarifa za  hali ya hewa kwa ajili ya kupanga mipango na kutoa maamuzi katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi ambazo hutegemea sana hali ya hewa, “High-level launch of the Climate Science Information for Climate Action Initiative”, vile vile, TMA ilishiriki mazungumzo yenye lengo la kuboresha ushirikiano kati yake na Taasisi ya Hali ya Hewa ya Denmark (DMI). Kati ya maeneo ya uboreshaji wa ushirikiano huo ni pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya uangazi wa hali ya hewa; uendelezaji wa wataalamu wa hali ya hewa; utafiti na utoaji wa tahadhari kwa ajili ya uratibu na kupunguza athari za maafa yanayosababishwa na hali mbaya ya hewa.

TMA pia ilifanya mazungumzo na Taasisi ya Hali ya Hewa ya Burundi kuhusiana na mwendelezo wa ushirikiano uliyopo kati ya taasis hizo mbili ikiwa Pamoja na eneo la mafunzo ambapo Burundi wanatarajiwa kuleta wataalamu wao kusoma katika Chuo cha Hali ya Hewa cha Taifa (NMTC) kilichopo Mkoani Kigoma.

Mkutano huo wa COP26 unajadili namna ya kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi na athari za mabadiliko hayo katika sekta mbali mbali za kijamii na kiuchumi. Katika mikutano ya COP, taasisi za hali ya hewa zimepewa jukumu la kufuatilia masuala yanayohusu tafiti za kisayansi na masuala ya uangazi ‘Research and Systematic Observation’, pamoja na masuala ya teknolojia ya hali ya hewa.

Monday, November 8, 2021

ONGEZEKO LA JOTO NCHINI

 


Dar es Salaam, 08 Novemba 2021:

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inatoa taarifa juu ya uwepo wa ongezeko la joto katika maeneo mengi hapa nchini.

Ongezeko hili la joto linatokana na kusogea kwa jua la utosi sambamba na upungufu wa mvua katika maeneo mengi ya nchi yetu kama ilivyotabiriwa awali. Hapa nchini, vipindi vya jua la utosi hufikia kilele mwishoni mwa mwezi Novemba wakati jua la utosi likiwa linaelekea kusini (Tropiki ya Kaprikoni) na hali hiyo hujirudia tena mwezi Februari wakati jua la utosi likiwa linaelekea kaskazini (Tropiki ya Kansa). Jua la utosi huambatana na hali ya Joto kali kwa sababu uso wa dunia katika eneo tajwa huwa karibu zaidi na jua kuliko maeneo mengine. Vilevile, hali ya joto kali hujitokeza zaidi kunapokuwa na upungufu wa mvua kama ilivyo katika kipindi hiki.

Katika kipindi hiki viwango vya joto vilivyoripotiwa katika maeneo mbalimbali ni vikubwa ambapo mkoa wa Kilimanjaro uliripoti kiwango cha juu cha joto kilichofikia nyuzi joto 36.4 sawa na ongezeko la nyuzi joto 4.6 ukilinganisha na wastani wa muda mrefu kwa mwezi Novemba. Vilevile, kiwango cha juu cha joto katika mkoa wa Dar es salaam kimefikia nyuzi joto 33.8 sawa na ongezeko la nyuzi joto 2.2 wakati katika mkoa wa Ruvuma kimefikia nyuzi joto 34.4 sawa na ongezeko la nyuzi joto 4.3. Hali kama hii imejitokeza pia katika mikoa yote nchini ambapo kiwango cha joto kimekuwa kikubwa kuliko wastani wa muda mrefu.

Vipindi vya joto kali vinatarajiwa kuendelea kujitokeza katika mwezi Novemba, 2021 na kupungua kidogo ifikapo mwezi Disemba, 2021 ambapo mtawanyiko wa mvua unatarajiwa kuongezeka sambamba na mionzi ya jua la utosi kuwa imeondoka katika maeneo ya nchi yetu.

Hivyo, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania inaendelea kutoa wito kwa wananchi kufuatilia taarifa za mwenendo wa hali ya hewa zinazotolewa pamoja na kutafuta, kupata na kutumia ushauri wa wataalamu wa kisekta ili kujiepusha na madhara yanayoweza kusababishwa na hali mbaya ya hewa ikiwemo joto kali.


Friday, November 5, 2021

Dkt. Kijazi aongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano mkuu maalumu wa Kidunia wa hali ya hewa “Extra-ordinary session of the World Meteorological Congress (Cg-Ext (2021)

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi akiwasilisha mapendekezo ya Kikosi kazi cha WMO cha kufanya mapitio ya muundo na utendaji kazi wa kanda za WMO (Executive Council Task Force on the Comprehensive Review of the WMO Regional Concept and Approaches) kuhusiana na maboresho ya kimuundo na utendaji kazi wa kanda za WMO, Dkt. Kijazi aliwasilisha mapendekezo hayo katika mkutano mkuu maalumu wa Kidunia wa hali ya hewa “Extra-ordinary session of the World Meteorological Congress (Cg-Ext (2021), tarehe 11 Oktoba, 2021. Kulia kwake ni Meneja wa Ushirikiano wa masuala ya hali ya hewa Kikanda na Kimataifa na Mshauri wa  Makamu wa Tatu wa Rais, Bw. Wilbert Muruke  akifuatilia mkutano na kumsaidia  Dkt. Kijazi. 


Washiriki wa TMA katika Mkutano wa 74 wa Baraza Kuu la Utendaji la WMO “Seventy- Second Session of the WMO Executive Council (EC-74) wakifuatilia mkutano huo uliofanyika kwa njia ya mtandao kuanzia tarehe 25 hadi 29 Oktoba, 2021, wakiongozwa na Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO, Dkt. Agnes Kijazi. Mkutano wa EC-74 ulifanyika kwa lengo la kujadili utekelezaji wa maamuzi ya mkutano mkuu maalumu wa Kidunia wa hali ya hewa “Extra-ordinary session of the World Meteorological Congress (Cg-Ext (2021). Aliyeko kwenye runinga ni Rais wa WMO, Prof. Gerhard Adrian akiongoza mkutano wa EC-74.




 Dar es Salaam; Tarehe 22/10/2021

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi ameongoza ujumbe wa Tanzania katika mkutano mkuu maalumu wa Kidunia wa hali ya hewa “Extra-ordinary session of the World Meteorological Congress (Cg-Ext (2021), uliofanyika kwa njia ya mtandao kuanzia tarehe 11 hadi 22 Oktoba, 2021. 

Lengo la mkutano huo lilikuwa ni kujadili utekelezaji wa maamuzi ya mkutano mkuu wa 18 wa Kidunia wa hali ya hewa “Eighteenth Session of the World Meteorological Congress (Cg-18)” uliofanyika mwaka 2019, pamoja na mapendekezo mapya ya kuboresha zaidi huduma za hali ya hewa ili ziweze kuleta tija zaidi kwa jamii. Mkutano mkuu huo maalumu ulijielekeza zaidi katika maeneo makuu matatu, ambayo ni: 

·       Tathmini ya utekelezaji wa mabadiliko ya muundo wa WMO “(WMO reform)”;

·       Mchango wa WMO katika maendeleo ya sekta ya maji (WMO support to the global water agenda); na 

·       Maboresho ya sera ya WMO ya ubadilishanaji wa data za hali ya hewa (WMO Unified Policy on International Data Exchange).

Mkutano huo ulipokea na kujadili taarifa na mapendekezo ya kamati na vikosikazi mbalimbali vya WMO vinavyoshughulikia maeneo hayo. 

Miongoni mwa masuala yaliyojadiliwa ni mapendekezo ya Kikosi kazi cha WMO kilichopewa jukumu la kufanya mapitio ya muundo na utendaji kazi wa kanda za WMO (Executive Council Task Force on the Comprehensive Review of the WMO Regional Concept and Approaches). Dkt. Kijazi ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kikosikazi, aliwasilisha maapendekezo ya Kikosikazi hicho kuhusiana na maboresho ya kimuundo na utendaji kazi wa kanda za WMO, ili ziweze kushiriki ipasavyo  katika uboreshaji wa huduma za hali ya hewa kwa Nchi Wanachama wa WMO zilizomo katika kanda husika. Mkutano ulipitisha mapendekezo yaliyowasilishwa na kumwomba Katibu Mkuu wa WMO kusimamia utekelezaji wa maamuzi hayo.

Ujumbe wa Tanzania katika mkutano mkuu huo maalumu wa Kidunia wa hali ya hewa ulijumuisha washiriki kutoka TMA, Wizara ya Maji, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, na mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika Ofisi ya Umoja wa Mataifa,  Geneva – Uswisi. 

Mkutano mkuu huo maalumu ulifuatiwa na Mkutano wa 74 wa Baraza Kuu la Utendaji la WMO “Seventy- Second Session of the WMO Executive Council (EC-74) uliofanyika pia kwa njia ya mtandao kuanzia tarehe 25 hadi 29 Oktoba, 2021 kwa lengo la kujadili utekelezaji wa maamuzi ya mkutano mkuu maalumu wa Kidunia wa hali ya hewa.Mikutano yote miwili iliongozwa na Rais wa WMO, Prof. Gerhard Adrian, ambaye ni raia wa Ujerumani.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...