Thursday, November 17, 2022

HALI YA JOTO NCHINI


 Dar es Salaam, 17 Novemba 2022:

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inatoa taarifa juu ya uwepo wa ongezeko la joto katika maeneo mbalimbali nchini.

Kumekuwepo na ongezeko la joto katika baadhi ya maeneo nchini. Hali hii imesababishwa na kusogea kwa jua la utosi sambamba na upungufu wa mvua katika maeneo mengi hapa nchini kama ilivyotabiriwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania. Kwa kawaida vipindi vya jua la utosi nchini hufikia kilele mwishoni mwa mwezi Novemba wakati jua la utosi likiwa linaelekea kusini (Tropiki ya Kaprikoni) na hali hiyo hujirudia tena mwezi Februari wakati jua la utosi likiwa linaelekea kaskazini (Tropiki ya Kansa). Jua la utosi huambatana na hali ya ongezeko la joto kwa sababu uso wa dunia katika eneo tajwa huwa karibu zaidi na jua kuliko maeneo mengine.

Katika kipindi cha mwezi Oktoba, 2022, hali ya joto iliongezeka katika maeneo mbali mbali nchini. Kiwango cha juu zaidi cha joto cha nyuzi joto 36.9 0C kiliripotiwa katika kituo cha Mpanda, Katavi mnamo tarehe 26 Oktoba, 2022. Kiwango hiki ni sawa na ongezeko la nyuzi joto 4.0 0C ukilinganisha na wastani wa muda mrefu kwa mwezi Oktoba. Aidha, baadhi ya maeneo mengine yaliyokuwa na ongezeko la joto kwa mwezi Oktoba, 2022 ni pamoja na mkoa wa Tabora nyuzi joto 35.7 (ongezeko la nyuzi joto 3.0), Moshi nyuzi joto 34.1 (ongezeko la nyuzi joto 3.2) na Dar es Salaam nyuzi joto 32.8 (ongezeko la nyuzi joto 1.4).

Aidha, katika wiki mbili za mwanzo za mwezi Novemba, 2022; hali ya ongezeko la joto iliendelea kujitokeza katika baadhi ya maeneo ambapo kituo cha Mpanda kiliripoti nyuzi joto 35.4 0C mnamo tarehe 2 Novemba, 2022 ikiwa ni ongezeko la nyuzi joto 4.7 ukilinganisha na wastani wa muda mrefu kwa mwezi Novemba. Kituo cha Tabora kiliripoti nyuzi joto 34.8 (ongezeko la nyuzi joto 3.7), Dar es Salaam nyuzi joto 33.7 (ongezeko la nyuzi joto 2.1) pamoja na Kilimanjaro nyuzi joto 34.3 (ongezeko la nyuzi joto 2.4).

Vipindi vya ongezeko la joto vinatarajiwa kuendelea kujitokeza katika mwezi Novemba, 2022 hususan katika maeneo yanayotarajiwa kuendelea kuwa na upungufu wa mvua na kupungua kidogo ifikapo mwezi Disemba, 2022 ambapo ongezeko la mtawanyiko wa mvua unatarajiwa.

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania inaendelea kutoa wito kwa wananchi kufuatilia taarifa za mwenendo wa hali ya hewa zinazotolewa pamoja na kutafuta, kupata na kutumia ushauri wa wataalamu wa kisekta ili kuepuka au kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na hali mbaya ya hewa ikiwemo ongezeko la joto.

Wednesday, November 16, 2022

MHE. MBARAWA ATEMBELEA BANDA LA TMA NA KUPATA MAELEZO YA HUDUMA ZA HALI YA HEWA KATIKA SEKTA YA UCHUKUZI.

 
 


Dar es Salaam, Tarehe 16/11/2022.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhe. Profesa Makame Mnyaa Mbarawa (MB) ametembelea banda la Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) lililopo katika maonesho yaliyoandaliwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa lengo la kutangaza kazi za taasis mbalimbali zilizopo chini ya wizara hiyo kupitia mkutano wa 15 wa wadau wa kutathmini utendaji kazi wa sekta ya uchukuzi kwa mwaka mmoja, uliofanyika katika ukumbi wa Kisenga LAPF - Dar es salaam, Tarehe 16 Novemba, 2022.

Mhe. Mbarawa akiambatana na Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Africa (AFDO) Dkt. Patricia Laverley, walielezwa umuhimu wa huduma za hali ya hewa kwa sekta ya ujenzi na uchukuzi ikiwa ni pamoja na huduma mahususi za usafiri wa barabara, maji na anga.

Aidha, kupitia maonesho hayo Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Ndg. Wilbert Muruke alizungumza na vyombo vya habari na kuelezea umuhimu wa huduma za hali ya hewa katika sekta ya uchukuzi jinsi zinavyosaidia katika kutekeleza majukumu ya sekta vilevile kukabiliana na athari zitokanazo na hali mbaya ya hewa.

“Kama mnavyoelewa huduma za hali ya hewa ni mtambuka kwa sekta mbalimbali mojawapo ya sekta ambayo tunaihudumia ni sekta ya usafirishaji ambapo katika ujenzi wa miundombinu mbalimbali ikiwemo viwanja vya ndege, reli, barabara na madaraja moja ya taarifa muhimu katika mipango yao ni taarifa za hali ya hewa zitakazowawezesha kupanga vyema mipango yao na hivyo kusaidia kuepusha hasara zitakazojitokeza kutokana na majanga yatokanayo na hali mbaya ya hewa”. Alisema Ndg. Muruke.

Ndg. Muruke aliongezea kwa kuwataka wadau kuendelea kufuatilia taarifa mbalimbali za hali ya hewa zinazotolewa mara kwa mara na TMA hususani katika kipindi hiki ambacho dunia imeendelea kukumbwa na mabadiliko ya hali ya hewa. Hii itasaidia kupunguza au kuepusha hasara zinazoweza kujitokeza  kutokana na hali mbaya ya hewa.

Thursday, November 3, 2022

MSEMAJI MKUU WA SERIKALI ATOA WITO KWA WANANCHI KUFUATILIA TAARIFA ZA HALI YA HEWA.




 

Dar es Salaam; Tarehe 02 Novemba, 2022;

Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa ametoa wito kwa wananchi kufuatilia taarifa za hali za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA). Amesema matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa yainasaidia kutambua hali ikoje katika siku zijazo na hivyo kusaidia kupanga shughuli mbalimbali kwa kushirikiana na wataalam kutoka sekta husika.

“Natoa wito kwa watanzania kutumia taarifa sahihi kutoka TMA ili kuweza kutambua hali ikoje katika shughuli zetu kwa kushirikiana na wataalamu kutoka sekta husika”. Alisema Msigwa wakati wa uwasilishwaji wa taarifa ya utekelezaji wa majukumu na mafanikio ya TMA kwa mwaka wa fedha 2021/22 na mwelekeo wa utekelezaji kwa mwaka 2022/23, katika Ukumbi wa Idara ya Habari-MAELEZO, Dodoma.

 

Awali wakati akiwasilisha taarifa hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri, Dkt. Hamza Kabelwa alisema katika kipindi husika, TMA imefanikiwa kutekeleza  miradi ya rada, vifaa na miundo mbinu ya hali ya hewa ambapo hatua zilizofikiwa  ni asilimia 90 ya utengenezaji wa  mtambo wa rada mbili za Mbeya na Kigoma ambapo malipo ya  asilimia 90 yamefanyika pamoja mitambo miwiili ya kupima hali ya hewa inayohamishika na ununuzi wa kompyuta maalum ‘cluster computer ilinunuliwa.

“Aidha, Mamlaka ilizinduwa mfumo mpya wa uangazi wa hali ya hewa ya anga za juu katika kituo cha kupima hali ya hewa ya anga ya juu kilichopo JNIA, Mamlaka iliendelea na jukumu lake la kutoa utabiri kwa usahihi, kwa  mfano utabiri wa mvua za msimu ulioanza Novemba 2021 hadi Aprili 2022 ulikuwa una usahihi wa asilimia 93.8 ukiwa juu ya kiwango cha usahihi kinachokubalika kimataifa”.

Akielezea matarajio katika mwaka wa fedha 2022/23, Dkt. Kabelwa alisema, matarajio yaliyopo ni pamoja na kupanua wigo wa utoaji wa elimu kwa wananchi na wadau juu ya umuhimu wa huduma za hali ya hewa,kuimariasha uangazi wa hali ya hewa katika Bahari na Maziwa makuu, kuedelea na utekelezaji wa sheria Na. 2 ya mwaka 2019 na kanuni zake pamoja kuboresha miundo mbinu ya Chuo cha taifa cha Hali ya Hewa.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...