Friday, December 30, 2022

TMA YATOA MSAADA WA VIFAA TIBA KATIKA KITUO CHA AFYA TANDALE.

 

Dar es Salaam, Tarehe 28/12/2022.

Tunapoelekea katika sherehe za kumaliza mwaka 2022 na kuukaribisha mwaka 2023, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ilitembelea kituo cha afya cha Tandale, Tarehe 28/12/2022 na kutoa msaada wa vifaa tiba ambavyo viliwasilishwa rasmi  na Kaimu Meneja wa Masoko wa TMA Bi Monica Mutoni kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Ladislaus Chang’a.

Akizungungumza wakati wa kukabidhi vifaa hivyo, Bi. Monica Mutoni alisema msaada wa vifaa tiba hivyo ni matokeo ya Kongamano la 15 la  EUMETSAT lililofanyika mwezi Septemba 2022 kwa lengo la kutoa huduma ya kwanza kwa wadau wa Kongamano hilo kutoka nchi zote za Afrika na baadhi ya nchi za nje ya Afrika.

“vifaa hivyo vilikabidhiwa TMA na wataalamu wa afya kutoka hospitali ya Taifa ya Muhimbili, vipo takribani 25, hivyo basi kwa upendo wetu kwenu na kwa kuwa moja ya majukumu ya TMA ni kurudisha kwa jamii, Kaimu Mkurugenzi Mkuu ametuagiza kutoa msaada wa hivi ili kuweza kusaidia jamii na wahitaji wote wanaotumia kituo hiki”. Alisisitiza Bi. Monica Mutoni

Aidha, vifaa hivyo vilipokelewa na Kaimu Mganga Mfawidhi wa kituo cha afya cha Tandale, Dkt. Merina Kulwa, ambaye aliishukuru TMA na kusema kuwa msaada huo utasaidia katika kuboresha utoaji huduma kituoni hapo.


Thursday, December 22, 2022

TMA YAWAHAKIKISHIA HUDUMA BORA NA UFANISI WADAU WA USAFIRI WA ANGA










Matukio mbalimbali katika picha wakati mkutano na wadau wa usafiri wa Anga ukiendelea katika ukumbi wa TAA, Dodoma tarehe 21 Disemba 2022.


Dodoma; Tarehe 21 Disemba, 2022;

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imekutana na wadau  wa usafiri wa  Anga wa jijini Dodoma katika ukumbi wa TAA,Dodoma tarehe 21 Disemba, 2022,ili  kujadili maendeleo na mahitaji ya huduma za Hali ya Hewa kwa usafiri wa Anga.


Akifungua mkutano huo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu, TMA, Dkt. Ladislaus Chang’a alisema “Kusudi la mkutano huu ni kutathimini maendeleo na mahitaji ya utoaji wa huduma za Hali ya Hewa kwa ajili ya usafiri wa Anga ili kuongeza tija na ufanisi katika shughuli na kuhakikisha  usalama wa usafiri wa  Anga ”.Alisema Dkt. Ladislaus Chang’a.


“TMA imeendelea kutambua umuhimu wa mikutano hii kwani imesaidia kuboresha sio tu ubora wa bidhaa zetu  bali pia taratibu za utoaji wa huduma katika sekta ya usafiri wa  Anga. Nakumbuka, miaka ya nyuma kulikuwa na malalamiko kadhaa juu ya kutafuta njia bora ya kuhakikisha taarifa za Hali ya Hewa kwa marubani zinapatikana kwa njia ya mtandao yaani (online), TMA tulifanyia kazi malalamiko hayo na kuweza kutengeneza mfumo wa Tehama wa usambazaji wa taarifa hizo unaoitwa MAIS na kuanza kufanya kazi rasmi mwaka 2012.” Aliongeza Dkt. Ladislaus Chang’a.


Dkt. Chang’a alisisitiza kuwa TMA inafanya kazi kwa kuzingatia taratibu za Kitaifa na Kimataifa. Akizungumzia kuhusu taratibu za Kimataifa, alieleza kuwa TMA imeendelea kukaguliwa kila mwaka na kuendelea kushikilia cheti cha ubora ISO 9001: 2015 na hivyo kuhakikishia ubora wa huduma zitolewazo kukidhi viwango vya Kimataifa.

Na kuhusu mabadiliko ya tabia ya Nchi, TMA imeendelea kufuatilia kwa karibu changamoto ya mabadiliko ya Hali ya Hewa hususan ongezeko la joto na matukio ya hali mbaya ya Hewa ambayo pia yanaendelea kuathiri huduma katika sekta ya usafiri wa Anga na hivyo kuhitaji uimarishaji wa utoaji na matumizi ya taarifa za Hali ya Hewa.


Awali wakati akifungua Mkutano huo, aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuboresha miundo mbinu ya Hali ya Hewa kwa kufanya ununuzi wa vifaa mbalimbali vya kisasa vya hali ya hewa ikiwemo Rada.



Monday, December 19, 2022

KIKAO CHA MWAKA 2022, TUGHE - TMA

 







Matukio mbalimbali katika picha wakati kikao cha mwaka 2022, TUGHE - TMA kikiendelea.

Thursday, November 17, 2022

HALI YA JOTO NCHINI


 Dar es Salaam, 17 Novemba 2022:

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inatoa taarifa juu ya uwepo wa ongezeko la joto katika maeneo mbalimbali nchini.

Kumekuwepo na ongezeko la joto katika baadhi ya maeneo nchini. Hali hii imesababishwa na kusogea kwa jua la utosi sambamba na upungufu wa mvua katika maeneo mengi hapa nchini kama ilivyotabiriwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania. Kwa kawaida vipindi vya jua la utosi nchini hufikia kilele mwishoni mwa mwezi Novemba wakati jua la utosi likiwa linaelekea kusini (Tropiki ya Kaprikoni) na hali hiyo hujirudia tena mwezi Februari wakati jua la utosi likiwa linaelekea kaskazini (Tropiki ya Kansa). Jua la utosi huambatana na hali ya ongezeko la joto kwa sababu uso wa dunia katika eneo tajwa huwa karibu zaidi na jua kuliko maeneo mengine.

Katika kipindi cha mwezi Oktoba, 2022, hali ya joto iliongezeka katika maeneo mbali mbali nchini. Kiwango cha juu zaidi cha joto cha nyuzi joto 36.9 0C kiliripotiwa katika kituo cha Mpanda, Katavi mnamo tarehe 26 Oktoba, 2022. Kiwango hiki ni sawa na ongezeko la nyuzi joto 4.0 0C ukilinganisha na wastani wa muda mrefu kwa mwezi Oktoba. Aidha, baadhi ya maeneo mengine yaliyokuwa na ongezeko la joto kwa mwezi Oktoba, 2022 ni pamoja na mkoa wa Tabora nyuzi joto 35.7 (ongezeko la nyuzi joto 3.0), Moshi nyuzi joto 34.1 (ongezeko la nyuzi joto 3.2) na Dar es Salaam nyuzi joto 32.8 (ongezeko la nyuzi joto 1.4).

Aidha, katika wiki mbili za mwanzo za mwezi Novemba, 2022; hali ya ongezeko la joto iliendelea kujitokeza katika baadhi ya maeneo ambapo kituo cha Mpanda kiliripoti nyuzi joto 35.4 0C mnamo tarehe 2 Novemba, 2022 ikiwa ni ongezeko la nyuzi joto 4.7 ukilinganisha na wastani wa muda mrefu kwa mwezi Novemba. Kituo cha Tabora kiliripoti nyuzi joto 34.8 (ongezeko la nyuzi joto 3.7), Dar es Salaam nyuzi joto 33.7 (ongezeko la nyuzi joto 2.1) pamoja na Kilimanjaro nyuzi joto 34.3 (ongezeko la nyuzi joto 2.4).

Vipindi vya ongezeko la joto vinatarajiwa kuendelea kujitokeza katika mwezi Novemba, 2022 hususan katika maeneo yanayotarajiwa kuendelea kuwa na upungufu wa mvua na kupungua kidogo ifikapo mwezi Disemba, 2022 ambapo ongezeko la mtawanyiko wa mvua unatarajiwa.

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania inaendelea kutoa wito kwa wananchi kufuatilia taarifa za mwenendo wa hali ya hewa zinazotolewa pamoja na kutafuta, kupata na kutumia ushauri wa wataalamu wa kisekta ili kuepuka au kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na hali mbaya ya hewa ikiwemo ongezeko la joto.

Wednesday, November 16, 2022

MHE. MBARAWA ATEMBELEA BANDA LA TMA NA KUPATA MAELEZO YA HUDUMA ZA HALI YA HEWA KATIKA SEKTA YA UCHUKUZI.

 
 


Dar es Salaam, Tarehe 16/11/2022.

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhe. Profesa Makame Mnyaa Mbarawa (MB) ametembelea banda la Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) lililopo katika maonesho yaliyoandaliwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa lengo la kutangaza kazi za taasis mbalimbali zilizopo chini ya wizara hiyo kupitia mkutano wa 15 wa wadau wa kutathmini utendaji kazi wa sekta ya uchukuzi kwa mwaka mmoja, uliofanyika katika ukumbi wa Kisenga LAPF - Dar es salaam, Tarehe 16 Novemba, 2022.

Mhe. Mbarawa akiambatana na Mkurugenzi wa Benki ya Maendeleo ya Africa (AFDO) Dkt. Patricia Laverley, walielezwa umuhimu wa huduma za hali ya hewa kwa sekta ya ujenzi na uchukuzi ikiwa ni pamoja na huduma mahususi za usafiri wa barabara, maji na anga.

Aidha, kupitia maonesho hayo Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Ndg. Wilbert Muruke alizungumza na vyombo vya habari na kuelezea umuhimu wa huduma za hali ya hewa katika sekta ya uchukuzi jinsi zinavyosaidia katika kutekeleza majukumu ya sekta vilevile kukabiliana na athari zitokanazo na hali mbaya ya hewa.

“Kama mnavyoelewa huduma za hali ya hewa ni mtambuka kwa sekta mbalimbali mojawapo ya sekta ambayo tunaihudumia ni sekta ya usafirishaji ambapo katika ujenzi wa miundombinu mbalimbali ikiwemo viwanja vya ndege, reli, barabara na madaraja moja ya taarifa muhimu katika mipango yao ni taarifa za hali ya hewa zitakazowawezesha kupanga vyema mipango yao na hivyo kusaidia kuepusha hasara zitakazojitokeza kutokana na majanga yatokanayo na hali mbaya ya hewa”. Alisema Ndg. Muruke.

Ndg. Muruke aliongezea kwa kuwataka wadau kuendelea kufuatilia taarifa mbalimbali za hali ya hewa zinazotolewa mara kwa mara na TMA hususani katika kipindi hiki ambacho dunia imeendelea kukumbwa na mabadiliko ya hali ya hewa. Hii itasaidia kupunguza au kuepusha hasara zinazoweza kujitokeza  kutokana na hali mbaya ya hewa.

Thursday, November 3, 2022

MSEMAJI MKUU WA SERIKALI ATOA WITO KWA WANANCHI KUFUATILIA TAARIFA ZA HALI YA HEWA.




 

Dar es Salaam; Tarehe 02 Novemba, 2022;

Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa ametoa wito kwa wananchi kufuatilia taarifa za hali za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA). Amesema matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa yainasaidia kutambua hali ikoje katika siku zijazo na hivyo kusaidia kupanga shughuli mbalimbali kwa kushirikiana na wataalam kutoka sekta husika.

“Natoa wito kwa watanzania kutumia taarifa sahihi kutoka TMA ili kuweza kutambua hali ikoje katika shughuli zetu kwa kushirikiana na wataalamu kutoka sekta husika”. Alisema Msigwa wakati wa uwasilishwaji wa taarifa ya utekelezaji wa majukumu na mafanikio ya TMA kwa mwaka wa fedha 2021/22 na mwelekeo wa utekelezaji kwa mwaka 2022/23, katika Ukumbi wa Idara ya Habari-MAELEZO, Dodoma.

 

Awali wakati akiwasilisha taarifa hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri, Dkt. Hamza Kabelwa alisema katika kipindi husika, TMA imefanikiwa kutekeleza  miradi ya rada, vifaa na miundo mbinu ya hali ya hewa ambapo hatua zilizofikiwa  ni asilimia 90 ya utengenezaji wa  mtambo wa rada mbili za Mbeya na Kigoma ambapo malipo ya  asilimia 90 yamefanyika pamoja mitambo miwiili ya kupima hali ya hewa inayohamishika na ununuzi wa kompyuta maalum ‘cluster computer ilinunuliwa.

“Aidha, Mamlaka ilizinduwa mfumo mpya wa uangazi wa hali ya hewa ya anga za juu katika kituo cha kupima hali ya hewa ya anga ya juu kilichopo JNIA, Mamlaka iliendelea na jukumu lake la kutoa utabiri kwa usahihi, kwa  mfano utabiri wa mvua za msimu ulioanza Novemba 2021 hadi Aprili 2022 ulikuwa una usahihi wa asilimia 93.8 ukiwa juu ya kiwango cha usahihi kinachokubalika kimataifa”.

Akielezea matarajio katika mwaka wa fedha 2022/23, Dkt. Kabelwa alisema, matarajio yaliyopo ni pamoja na kupanua wigo wa utoaji wa elimu kwa wananchi na wadau juu ya umuhimu wa huduma za hali ya hewa,kuimariasha uangazi wa hali ya hewa katika Bahari na Maziwa makuu, kuedelea na utekelezaji wa sheria Na. 2 ya mwaka 2019 na kanuni zake pamoja kuboresha miundo mbinu ya Chuo cha taifa cha Hali ya Hewa.

Saturday, October 29, 2022

MWENYEKITI WA BODI TMA APONGEZA UTEKELEZAJI WA MKATABA WA BARAZA LA WAFANYAKAZI





























Kibaha, Pwani; Tarehe 29 Oktoba, 2022;

Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Buruhani Nyenzi ameipongeza TMA kwa kutekeleza Mkataba wa Baraza kwa kuhakikisha wajumbe wa Baraza wanakutana mara mbili kwa mwaka. Alieleza hayo wakati akifungua rasmi Baraza la Wafanyakazi wa TMA la pili kwa mwaka 2022 katika Ukumbi wa Manesi na Wakunga,Kibaha, Pwani, tarehe 29/10/2022.

“Kupitia taarifa ya Mwenyekiti wa Baraza, nimeelezwa kuwa hiki ni kikao cha pili, hivyo naipongeza Mamlaka kwa kuwa na mabaraza mawili kwa mwaka kulingana na Mkataba. Aidha, niendelee kuwapongeza kwa uwakilishi mzuri kwa kuwa na wajumbe tisini na nane kutoka maeneo mbalimbali nchini”. Alisema Dkt. Nyenzi.

Dkt. Nyenzi aliendelea kwa kuipongeza Mamlaka kwa utekelezaji mzuri wa miradi mikubwa na mafanikio yaliyopatikana hususani fanikio la kuboresha miundo mbinu ya hali ya hewa sambamba na kutekeleza agizo la Serikali la kuhamia Dodoma, Makao Makuu ya nchi. Vilevile, aliishukuru Bodi kwa kazi nzuri ya usimamizi wa Taasisi uliochangia mafanikio hayo.

“Nitumie fursa hii kuwashuruku wajumbe wa Bodi ambao nimefanya nao kazi kwa kipindi cha miaka mitatu kwa utumishi wao uliotukuka uliopelekea mafanikio yote haya yaliyoainishwa na Mwenyekiti wa Baraza hili, ikiwa ni pamoja na uboreshaji wa maslahi ya wafanyakazi”. Alieleza Dkt. Nyenzi. 

Awali, Mkurugenzi wa Utafiti na Matumizi Dkt. Ladislaus Chang’a, akisoma taarifa ya Mwenyekiti wa Baraza kwa niaba ya Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), alishukuru Serikali kupitia Wizara na Bodi ya TMA kwa ushirikiano na kazi kubwa iliyofanyika ya kufanikisha malengo ya Taasisi, ambapo viwango vya usahihi wa utabiri vimeendelea kuongezeka, nakutoa wito kwa watanzania kutumia taarifa hizo za hali ya hewa. 

Katika taarifa hiyo, Dkt. Kijazi aliendelea kueleza kuwa “Dhumuni kuu la Baraza hili ni kufanya tathmini ya utendaji wa Mamlaka ambao utasaidia kuongeza ubora na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa umma kwa lengo la kupunguza athari za mabadiliko ya hali ya hewa na tabia nchi”.

Akielezea baadhi ya mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha Baraza lililopita na Baraza la sasa, Mwenyekiti wa Baraza alisema mafanikio hayo  ni pamoja na “ufanisi wa utekelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa na Kanuni zake, ununuzi wa rada na miundo mbinu kwa ujumla, uboreshaji wa maslahi ya wafanyaki kwa kuendelea kupandishwa vyeo,kubadilishwa kada,ongezeko la mishahara na kuhuishwa kwa miundo ya kada kwa watumishi kufuatia mabadiliko ya Miundo ya Maendeleo ya Watumishi”.







Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...