Tuesday, July 12, 2022

DKT. KIJAZI: TUTUMIE SHERIA YA MAMLAKA KATIKA UKUSANYAJI WA MAPATO.


 


Dar es Salaam; Tarehe 30/06/2022

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) Dkt. Agnes Kijazi, ambaye pia ni Makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) amewataka wafanyakazi wanaofanya kazi katika ofisi za TMA zilizopo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa  Mwalimu Julius Nyerere (JNIA), kutumia sheria ya Mamlaka katika kukusanya mapato yatakayochangia katika uboreshaji wa huduma za hali ya hewa nchini. Aliyasema hayo alipokuwa akifunga rasmi mafunzo ya siku nne yanayohusiana na uangazi wa anga la juu pamoja na taratibu za udhibiti wa ubora “Quality Management Systsem (QMS) procedures”, katika ofisi za TMA - JNIA, tarehe 30 Juni 2022.

 

“Nimekuwa nasisitiza muda mrefu juu ya kufanya kazi kwa ushirikiano yaani “Team work” hali iliyotuwezesha kutufikisha mpaka tukapata sheria yetu ya Mamlaka, lakini sasa siongelei tena “Team work” kwani najua hiyo ipo tayari katika utendaji kazi wetu wa kila siku, lakini hivi sasa nazungumzia suala la mapato, tunatakiwa tuitumie sheria yetu ya Mamlaka vizuri katika ukusanyaji wa mapato yatakayochangia kuboresha zaidi huduma za hali ya hewa nchini”. Alisisitiza Dkt. Kijazi. 

 

Aidha, Dkt. Kijazi aliwapongeza wafanyakazi kwa kupata mafunzo hayo kwani yatawaongezea uelewa katika utendaji kazi wao wa kila siku sambamba na kupata nafasi ya kujikumbusha masuala ya QMS, kwa lengo hilo hilo la kuboresha huduma za hali ya hewa hususan kwa usalama wa usafiri wa anga.

 

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Meneja wa TMA, Kituo cha Hali ya Hewa JNIA Bw. John Mayunga alimshukuru Mkurugenzi Mkuu wa TMA Dkt. Agnes Kijazi pamoja na menejiment yake kwa ujumla kwa kuwezesha kufanyika kwa mafunzo hayo muhimu ya siku nne, ambapo yalijumuisha kujifunza namna ya kutafsiri taarifa zinazotokana na uangazi wa anga za juu pamoja na namna ya kufanya kazi kwa kufuata taratibu za QMS. Aidha, kwa upande wa wafanyakazi wa TMA wa JNIA walimpongeza Dkt. Kijazi kwa utendajikazi wake mzuri kitaifa na kimataifa.


No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...