Monday, July 4, 2022

TAARIFA YA UTENDAJI WA JOPO LA WMO LINALOSIMAMIWA NA DKT. KIJAZI YAWASILISHWA.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi (wa pili kutoka kulia kwa walioketi) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wengine wa Baraza Kuu la Utendaji wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) wakati wa mkutano wa sabini na tano wa Baraza Kuu la WMO (WMO Executive Council-Seventy Fifth Session) uliofanyika tarehe 20 hadi 24 Juni, 2022, Geneva, Uswisi

Geneva, Uswisi; Tarehe 24/06/2022 

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) Dkt. Agnes Kijazi, Mwenyekiti wa Jopo la WMO la kujenga uwezo wa Nchi Wanachama wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) “WMO Capacity Development Panel (CDP)”, ambaye pia ni Makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), ameshiriki na kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya jopo hilo wakati wa Mkutano wa 75 wa Baraza Kuu la WMO “Seventy-Fifth Session of the WMO Executive Council (EC-75)” uliofanyika katika Makao Makuu ya WMO, Geneva, Uswisi kuanzia tarehe 20 hadi 24 Juni, 2022. Mkutano huo ulikuwa na lengo la kujadili utekelezaji wa maamuzi na maelekezo ya mikutano iliyotangulia ya WMO ambayo ni pamoja na Mkutano Mkuu wa 18 wa WMO “Seventeenth WMO Congress (Cg-18)” uliofanyika 2019, Mkutano Mkuu Maalum wa WMO wa 2021 (WMO Extraordinary Congress-2021) na mkutano wa 74 wa Baraza Kuu la WMO “Seventy-Fourth Session of the WMO Executive Council (EC-74)” uliofanyika 2021. Aidha, Mkutano huo wa 75 wa Baraza la WMO umetoa mapendekezo ya masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya hali ya hewa na maji yanayotakiwa kutolewa maamuzi na Mkutano Mkuu wa 19 wa WMO “Nineteenth WMO Congress (Cg-19) utakaofanyika mwezi Mei, 2023. 

Akiwasilisha ripoti ya jopo la WMO la kujenga uwezo “WMO Capacity Development Panel (CDP)”, Dkt. Kijazi aliainisha mafanikio yaliyofikiwa kupitia kazi za Jopo hilo ambazo ni pamoja na hatua zilizofikiwa za mapitio ya miongozo ya mafunzo ya wataalamu wa hali ya hewa “Status of the review of Basic Instructional Packages(BIPs)”; Uundwaji wa chombo kitakachowaunganisha wadau wote wanaotoa elimu ya hali ya hewa na maji “Consortium of WMO Education and Training Partners (CONECT)”; Mapitio ya mpango mkakati wa mafunzo wa WMO “Review the WMO Capacity Development Strategy (CDS)”; Maandalizi ya mwongozo wa kuhakikisha kuwa kazi za utoaji wa taarifa za hali ya hewa zinaendelea hata kipindi ambacho majanga kama UVIKO-19 yanapojitokeza, “Business Continuity and Contingency Planning Guidance”; Chapisho jipya la WMO la kisera na uongozi hasa likilenga taasisi za hali ya hewa “New publication on Public Policy and Management with focus on NMHSs”; Pamoja na ushirikiano kati ya sekta za hali ya hewa na maji kupitia Jopo la uratibu wa sekta za WMO, “Collaborations with the Hydrological Coordination Panel” 

 Aidha, Dkt. Kijazi alishiriki katika mkutano wa wa tatu wa Jukwaa la WMO la Kutoa Maoni “Third High-Level Session of Open Consultative Platform (OCP-HL-3)”), uliofanyika tarehe 20 Juni 2022 ambapo alikuwa Mwanajopo “Panelist”. Wakati akitoa mada na kujibu hoja kuhusiana na vipengele muhimu vya kisera na kisheria vya kuzingatiwa ili kukidhi mahitaji na majukumu ya taasisi za hali ya hewa kuendana na wakati, Dkt.Kijazi alisema “TMA ipo kisheria na kazi zake zimeainishwa katika Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya mwaka 2019, kifungu namba 5, ambapo TMA imepewa dhamana ya kutoa huduma za hali ya hewa ikijumuisha za kibiashara na zisizo za kibiashara pamoja na kudhibiti (regulate) huduma hizo katika eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania” 

Aidha, akiendelea kufafanua juu ya matakwa ya sheria hiyo alisema kuwa, sheria inawataka wadau wanaotumia huduma za hali ya hewa kwa shughuli za biashara kuchangia gharama kidogo ili ziwe endelevu kwa kuboresha miundo mbinu ambayo kwa hivi sasa kwa kiasi kikubwa inagharamiwa na serikali. Kwa kuongezea, Dkt.Kijazi alitoa wito kwa WMO kuongeza juhudi na rasilimali katika kuzisaidia taasisi za hali ya hewa za nchi wanachama wenye uwezo mdogo hususan katika Bara la Afrika na Asia ili ziweze kutoa huduma za hali ya hewa kwa viwango vinavyokubaliwa na WMO. Mkutano wa WMO EC-75 ulitanguliwa na Mkutano wa 41 wa Kamati ya Ushauri ya WMO katika Masuala ya Fedha “WMO Financial Advisory Committee (FINAC- 41) ambao pia Dkt. Kijazi ni mjumbe uliofanyika tarehe 16 na 17 Juni 2022, Geneva- Uswisi. 

Baraza Kuu la WMO ni chombo chenye jukumu la kusimamia utekelezaji wa maamuzi na maelekezo ya Mkutano Mkuu wa WMO (WMO Congress). Baraza hili linaundwa na wajumbe 37 wawakilishi kutoka mabara yote ya Dunia kwa uwiano uliopitishwa na Mkutano Mkuu wa WMO. Hivyo Baraza Kuu la WMO linaundwa na Rais wa WMO, Makamu wa Kwanza wa Rais; Makamu wa Pili wa Rais, Makamu wa Tatu wa Rais, Marais wa kanda sita(6) za WMO (WMO Regional Associations), na wajumbe 27 ambao ni Wakuu wa taasisi mbalimbali za hali ya hewa. Wawakilishi kutoka Kanda ya Afrika “WMO Regional Association 1(RA 1) kwa sasa ni: Makamu wa Tatu wa Rais, Dkt. Agnes Kijazi (Tanzania), Rais wa RA I, Dkt. Daouda Konate (Cote d'Ivoire) na wajumbe saba (7) kutoka nchi za Msumbiji, Chad, Morocco, Nigeria, Cameroon, Ethiopia na Namibia.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...