Saturday, March 23, 2019

TAARIFA YA WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO NA MKURUGENZI MKUU WA TMA KATIKAKUADHIMISHA SIKU YA HALI YA HEWA DUNIANI 23 MACHI 2019

Mhehimiwa Mhandisi Isack Kamwelwe

Muhtasari wa Taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Mhandisi  Isack Kamwelwe kwenye kilele cha maadhimisho ya siku ya Hali ya Hewa Duniani “World Meteorological Day (WMD)”, Ukumbi wa Wizara, Dar es Salaam, 23 Machi 2019.

Ni heshima kubwa kwangu kuwepo nanyi kwenye kilele cha maadhimisho haya ya siku ya Hali ya Hewa Duniani “World Meteorological Day (WMD)” kwa mwaka 2019. Naipongeza Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kwa kuandaa maadhimisho haya. Haya ni maadhimisho ya 69 tangu kuanzishwa kwa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) mwaka 1950. Kauli mbiu ya mwaka  huu ni  “Jua, Dunia, na Hali ya Hewa (The Sun, The Earth, and the Weather)”,  ambayo imelenga kutoa elimu kwa jamii na kuongeza uelewa wa sayansi ya hali ya hewa, hususan maandalizi, usambazaji na matumizi ya taarifa za hali ya hewa.
Siku ya Hali ya Hewa Duniani ni muhimu sana kwani inatupa nafasi ya kutafakari mchango wa Tanzania, kama mwanachama wa WMO katika utoaji wa huduma za hali ya hewa hapa Tanzania na ulimwenguni kote.
Kwa upande wa Tanzania, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ndiyo taasisi iliyopewa jukumu la kusimamia na kutoa huduma za hali ya hewa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa minajili hii Serikali yetu inaendelea kuwekeza katika kuimarisha huduma za hali ya hewa ikiwa ni pamoja na kuimarisha miundombinu ya uangazi, kwa mfano ununuzi wa RADAR na vifaa vingine vya hali ya hewa ambavyo ni kipaumbele kama ilivyolekezwa katika Mpando wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa Taifa  (2016/2017-2020/2021) chini ya Serikali ya awamu ya Tano.  Mpaka sasa Serikali tayari imenunua RADAR mbili za hali ya hewa ambazo zimewekwa Dar es Salaam na Mwanza. RADAR nyingine tatu zinatarajiwa kuwekwa Mtwara, Mbeya na Kigoma na ziko katika hatua za ununuzi.
Ni dhahiri kwamba huduma zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania zimeendelea kuongezeka viwango vya ubora ikiwa ni pamoja na usahihi wa utabiri na hivyo zinafaa kutumika katika sekta mbali mbali za maendeleo hapa nchini. Ninatoa wito kwa wadau wote wa hali ya hewa kutoka sekta zote za kiuchumi na kijamii na wananchi kwa ujumla kuendelea kufuatilia na kutumia huduma za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kwa ajili ya kupanga na kufanya maamuzi katika shughuli za kiuchumi na kijamii kwa ajili ya ustawi wa Taifa letu.
Serikali imeendelea kuwekeza katika kuboresha huduma za hali ya hewa kwa matumizi ya sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya usafiri wa anga, ambapo katika mwaka 2019 Tanzania imekuwa miongoni mwa nchi tatu barani Afrika zilizopata cheti cha ubora wa huduma za hali ya hewa katika usafiri na usalama wa anga (ISO 9001:2015) kwa mujibu wa Shirika la Viwango Duniani (ISO). Katika kuboresha usambazaji wa huduma za hali ya hewa, TMA imebuni mfumo wa kusambaza taarifa za hali ya hewa kwa njia ya simu za mkononi uitwao FarmSMS ambao umerahisisha upatikanaji wa taarifa za hali ya hewa kwa wadau.
Haya ni mafanikio makubwa katika kutekeleza mkataba wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani na kauli mbiu ya siku ya hali ya hewa Duniani ya mwaka huu. Pamoja na mafanikio haya, bado kuna changamoto nyingi zikiwemo gharama kubwa za vifaa vya hali ya hewa, kuendana na mabadiliko ya kukua kwa teknolojia katika tasnia ya hali ya hewa na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi (Climate Change). Utatuzi wa changamoto hizi unahitaji jitihada za pamoja za wadau mbalimbali.
Hivyo napenda kutumia fursa hii kutoa wito kwa wadau mbalimbali wa huduma za hali ya hewa kushirikiana na Serikali katika kutekeleza Programu ya Kitaifa ya Huduma za Hali ya Hewa (National Framework for Climate Servives), ambayo ni mwongozo muhimu katika utoaji na utumiaji wa huduma za hali ya hewa hapa nchini.
Mwisho, napenda kuwashukuru tena na kuwapongeza TMA na WMO kwa maadhimisho haya ya siku ya hali ya hewa Duniani. Natoa wito kwa jamii yote, ambao kimsingi ndio watumiaji wa taarifa za hali ya hewa tusherehekee siku hii kwa kuendelea kufuatilia taarifa za hali ya hewa kwa usalama wetu na mali zetu.
Nawatakia maadhimisho mema ya Siku ya Hali ya Hewa Duniani 2019
“Jua, Dunia, na Hali ya Hewa
 
Dkt. Agnes Kijazi
UJUMBE WA MKURUGENZI MKUU WA MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA (TMA), DKT. AGNES KIJAZI KWENYE KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA HALI YA HEWA DUNIANI “WORLD METEOROLOGICAL DAY (WMD)”, 23 MACHI, 2019.
Leo ni siku ya Hali ya Hewa Duniani “the World Meteorological Day (WMD)”, siku ambayo dunia inaadhimisha kuanzishwa kwa Shirika la Hali Duniani (WMO) ambapo Mkataba wa kuanzishwa kwa Shirika hilo ulisainiwa mnamo tarehe 23 Machi 1950. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), ikiwa moja wapo ya Taasisi za Hali ya Hewa za nchi 192 wanachama wa WMO inaungana na Jumuiya ya Hali ya Hewa Ulimwenguni  kote kusheherekea  siku hii. Taasisi za Hali ya Hewa, hutumia siku hii kueleza huduma za hali ya hewa na umuhimu wa kuzingatia na kujumuisha taarifa za hali ya hewa, ikiwemo utabiri na tahadhari katika kupanga na kutekeleza shughuli mbalimbali za kiuchumi, kijamii na kimaendeleo kwa ujumla.

Kwa upande wa hapa nchini Tanzania, huduma za hali ya hewa hutolewa na kusimamiwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).  TMA ni taasisi ya serikali chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Mamlaka imepewa dhamana ya kutoa na kusimamia huduma za hali ya hewa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ili kusisitiza na kuhamasisha umuhimu wa matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika mipango na maamuzi ya shughuli za kiuchumi na kijamii katika sekta mbalimbali, Uadhimishaji wa sherehe za siku ya Hali ya Hewa Duniani unaambatana na kauli mbiu maalumu kwa kila mwaka. Kauli mbiu ya mwaka huu ni “Jua, Dunia na Hali ya hewa (The Sun, The Earth, and the Weather)”. Kauli mbiu hii imechaguliwa kwa kuzingatia ukweli kwamba jua ndicho chanzo kikuu cha nishati ambayo huwezesha maisha ya viumbe vyote hapa duniani na huendesha mifumo ya hali ya hewa, mikondo ya bahari na mzunguko wa maji (hydrological cycle) na kuchangia katika shughuli zetu za kila siku za kiuchumi na kijamii katika uso wa Dunia.

Jua ndio nyota iliyo karibu zaidi na Dunia, umbali upatao Kilometa milioni 150 kutoka uso wa Dunia. Jua ndicho kitovu cha Unajimu na chanzo kikuu cha joto lililopo katika uso wa dunia ambalo linahitajika na viumbe hai mbalimbali ili viweze kuishi. Bila mwanga na joto litolewalo na jua kusingekuwa na maisha yoyote katika uso wa Dunia. Hivyo, joto litokanalo na jua ndilo husababisha mzunguko wa maji (hydrological cycle), mvukizo wa maji angani (evaporation) ambayo huganda na kufanyika mawingu na kisha kurudi tena kwenye uso wa Dunia kwa njia ya mvua. Mbali na kuwa chanzo kikuu cha mifumo ya hali ya hewa tunayoipata na kuwezesha maisha ya viumbe hai, mwanga wa jua una mchango wa pekee katika afya na ustawi wa viumbe hai na masuala ya Nishati. Inatazamiwa kuwa mchango wa Nishati mbadala katika mahitaji ya nishati ya dunia utafikia asilimia 40% ifikapo mwaka 2040. Uimarishaji wa upatikanaji na matumizi ya Nishati mbadala, ikiwemo nishati ya Jua na nishati ya upepo unahitaji jitihada kubwa za kuimarisha shughuli za uangazi wa hali ya hewa, ambapo mchango na wajibu wa Taasisi za Hali ya Hewa ikiwemo TMA ni mkubwa. Utoaji wa taarifa za hali ya hewa mahsusi kwa ajili ya masuala ya nishati ni wa muhimu sana, ukizingatia mikakati ya jumuiya ya kimataifa ya kuimarisha matumizi ya nishati mbadala ili kukabiliana na changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa (climate change). Uelewa kuhusu hali ya klimatolojia ya eneo husika ikiwemo mwenendo wa jua na nguvu yake, pamoja na nishati ya upepo ni muhimu sana katika kutoa mwongozo na kuongeza ufanisi na tija kwa uwekezaji  unaolenga kuimarisha nishati mbadala.
Katika kuimarisha upatikanaji na utumiaji wa taarifa za hali ya hewa katika kupanga shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii na kufikia maendeleo endelevu jitihada mbalimbali za kuboresha huduma za hali ya hewa katika ngazi ya kidunia na kitaifa zinafanyika. Katika ngazi ya kidunia, Programu ya Kidunia ya Huduma za Hali ya Hewa “The Global Framework for Climate Services (GFCS)” ndiyo programu inayotoa mwongoza wa namna ya kuboresha utoaji na utumiaji wa  taarifa za hali ya hewa katika mipango na maamuzi kwenye sekta mbali mbali za kiuchumi na kijamii duniani. Katika kuendeleza jitihada za kidunia, Tanzania inatekeleza Programu ya Kitaifa ya Huduma za Hali ya Hewa “the National Framework for Climate Services (NFCS)”, ambayo ilizunduliwa rasmi mwezi julai, 2018 ikiwa na malengo ya kuboresha huduma za hali ya hewa hususan kwa sekta zilizo katika hatari ya kuathirika zaidi na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa na mabadiliko ya tabia nchi zikiwemo Kilimo na Usalama wa chakula, Maji, Afya, Nishati na Maafa. Utekelezaji wa mpango wa NFCS umejikita katika kuimairisha shughuli za uangazi, utabiri, utafiti, ushirikishwaji wa Wadau na kujenga uwezo wa wataalamu na watumiaji wa taarifa za hali ya hewa.

Utabiri utolewao na TMA ni pamoja na utabiri wa kila siku (masaa 24), siku tano, siku kumi, mwezi, msimu na taarifa za hali mbaya ya hewa (severe weather warnings and alerts). Tabiri hizi za hali ya hewa ni kwa jamii yote kwa ujumla, na kwa sekta maalumu kama vile sekta ya usafiri wa anga, usafiri wa kwenye maji na nchi kavu, kilimo (kilimo mazao, mifugo na uvuvi), nishati, maji, utalii, afya, na usimamizi wa majanga kwa kutaja maeneo machache.

Taarifa hizi husambazwa kwa njia mbalimbali zikiwemo tovuti ya TMA (www.meteo.go.tz), radio, runinga, mitandao ya kijamii (facebook, twitter and Youtube), magazeti na Mfumo wa Kusambaza taarifa za hali ya hewa kwa njia ya simu za mkononi (FarmSMS).

Katika kuadhimisha siku ya Hali ya Hewa Duniani kwa mwaka 2019, napenda kutoa wito kwa wadau wote kuzifuatilia na kuzitumia taarifa za hali ya hewa katika kupanga mipango ya kiuchumi na kijamii kwa ajili ya maendeleo endelevu ya  nchi yetu na hasa kuchangia katika azma ya nchi yetu kwenda katika uchumi wa kati na uchumi wa viwanda
Nawatakia maadhimisho mema ya Siku ya Hali ya Hewa Duniani “World Meteorological Day” (WMD).

“Jua, Dunia na Hali ya Hewa”.

Siku ya Hali ya Hewa Duniani 2019


2 comments:

  1. Tunafarijika kuona namna ambavyo TMA yetu inavyoendelea kuboresha huduma za hali ya hewa kwa jamii. Viva TMA

    ReplyDelete
  2. TMA ni taasisi inayoendelea kujipambanua vyema katika majukumu yake ya kuhakikisha usalama wa raia na malizao unatekelezwa ipasavyo katika kufikia nchi ya uchumi wa kati na maendeleo ya viwanda.

    ReplyDelete

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...