Monday, August 26, 2019

WAZIRI KAMWELWE AHIMIZA MIPANGO MADHUBUTU YA KUKABILIA NA ATHARI ZA MABADILIKO YA HALI YA HEWA

 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe akifungua  mkutano wa 53 wa utabiri wa msimu wa vuli kwa nchi 11 za pembe ya Afrika unaofanyika kwenye hoteli ya Hyatt Regency jijini Dar es salaam.
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dk. Agnes Kijazi akizungumza katika mkutano huo unaofanyika kwenye hoteli ya Hyatt Regency jijini Dar es salaam leo.
Meza Kuu




‘Tarehe 26/08/2019: Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mh. Mhandisi Isaack Kamwelwe amehimiza wanasayansi na wataalam wa sekta mbalimbali kuhakikisha wanafanikisha upatikanaji wa mipango madhubuti ya kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa. Alizungumza hayo wakati akifungua rasmi mkutano wa 53 wa utoaji wa utabiri wa Hali ya Hewa wa Msimu wa Mvua za Vuli 2019 "Fifty Third Greater Horn of Africa Climate Outlook Forum" (GHACOF 53) unaofanyika katika Hotel ya Kilimanjaro (Hyatt Regency) kuanzia tarehe 26 hadi 28 Agosti 2019 Dar es Salaam.

'Naamini baada ya mkutano huu wataalamu mliopo kwenye mkutano huu mtakuja na mpango madhubuti wa kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa ili kuweza kupunguza athari zitokanazo na mabadiliko hayo’, alizungumza Mhe. Kamwelwe. 
 
Aidha, Mheshimiwa Kamwele aliwakumbusha wataalam hao kutoka nchi kumi na moja za pembe ya Afrika umuhimu wa kuhusisha utabiri wa jadi (Indigenous knowledge) katika kuboresha utabiri. Alisema kuna wadudu ambao wakionekana inaashiria kuanza kwa mvua na kuna ambao wakionekana inaashiria mvua si za kuridhisha, aliwataka wanasayansi hao kufanya uchambuzi wa kina. 
 
Sambamba na maelekezo hayo, Mheshimiwa Kamwele aliwakaribisha washiriki wa kongamano hilo kutembelea sehemu za vivutio vya utalii vilivyopo hapa nchini na aliwataka kujifunza maneno machache ya Kiswahili. 
 
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani, Dkt.Agnes Kijazi alimweleza mhe. Waziri kuwa kupitia mikutano hiyo kumekuwa na maboresho makubwa kwenye mfumo wa mawasiliano kati ya wanasayansi na wataalamu kutoka sekta mbalimbali hivyo kusaidia matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa zitolewazo na taasisi za hali ya hewa za nchi za Pembe ya Afrika. 
 
Pia, Dkt. Kijazi aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Rais John Joseph Pombe Magufuli kwa kutoa kipaombele katika uboreshaji wa huduma za hali ya hewa hapa nchini. 
 
Aliendelea kwa kusema kuwa uwekezaji unaofanywa na Serikali katika miundombinu ya hali ya hewa ukiwemo mtandao wa rada za hali ya hewa ni kielelezo tosha cha umakini wa serikali kuboresha sekta ya hali ya hewa ambayo ni ya muhimu sana katika kufikia maendeleo endelevu. 
 
Akizungumza kwa niaba ya wakuu wa taasis za hali ya hewa katika nchi za pembe ya Afrika Dkt. Kijazi aliziomba serikali za nchi hizo kuendelea kuboresha huduma za hali ya hewa na pia aliwashukuru ICPAC kwa kuendelea kuendesha makongamano hayo ambayo alisema yameendelea kuwa chachu ya uboreshaji wa utabiri wa msimu katika nchi za pembe ya Afrika. 
 
Kwa upande wa Mkurugenzi wa Taasis inayosimamia Masuala ya Hali ya Hewa kwa Nchi za Pembe ya Afrika (IGAD Climate Prediction and Application Centre (ICPAC)) Dkt. Guleid Artan alielezea lengo la kongamano hilo kuwa ni kujadili na kuandaa kwa pamoja utabiri wa msimu wa mvua za vuli za mwezi Oktoba hadi Desemba 2019, pamoja na kuandaa mikakati ya kukubaliana na hali mbaya ya hewa kwa msimu huo kwa kulenga sekta muhimu za kijamii na kiuchumi ambazo ni pamoja na afya, kilimo na usalama wa chakula, maji, nishati n.k. 
 
Mwakilishi wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani, Dkt. Afiesimama aliwajulisha washiriki wa kongamano hilo kwamba katika mkutano wa WMO Congress uliomalizika hivi karibuni Afrika ilifanikiwa kuwa na mwakilishi katika ngazi za juu za uongozi wa Shirika hilo kupitia Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ambaye alichaguliwa katika nafasi ya Makamu wa tatu wa Rais wa WMO. Aidha, aliahidi kwamba WMO itaendelea kuzisaidia nchi wanachama kuboresha huduma zikiwemo nchi za pembe ya Afrika. 
 
Wengine waliozungumza katika ufunguzi wa Kongamano hilo ni mwakilishi wa Bank ya maendeleo ya Afrika Dkt. Solomon Ngoze ambae alielezea misaada mbali mbali iliyotolewa na Bank hiyo katika kuboresha huduma za hali ya hewa kwenye nchi za pembe ya Afrika.  Mwakilishi wa programu ya WISER Mr. Adam Curtis alielezea mafanikio yaliyofikiwa katika kutekeleza programu hiyo. Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Dkt. Buruhani Nyenzi aliwakumbusha washiriki hao kwamba kongamano la kwanza lilifanyika nchini Zimbabwe mwaka 1996 ambapo yeye binafsi alikuwa kiongozi wa taasisi iliyohusika na ukame kusini mwa Afrika ambayo ndiyo iliendesha kongamano hilo. Alionyesha furaha yake kuona kwamba makongamano hayo yanaendelea kwa ufanisi mkubwa. 
 

GHACOF ni Mkutano unaojumuisha nchi za Pembe ya Afrika ambazo ni Tanzania, Kenya, Somalia, Ethiopia, Sudan, Sudan ya Kusini, Uganda, Burundi, Rwanda, Djibouti na Eritrea pamoja na mashirika ya Kimataifa ikiwemo Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO). 
 

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...