Friday, June 26, 2020

WATAALAMU WA HALI YA HEWA WATAKIWA KUJENGEWA UWEZO KATIKA UTOAJI WA HUDUMA ZA HALI YA HEWA KWA WATUMIAJI WA BAHARI

Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO, Dkt. Agnes Kijazi akichangia katika mjadala kwenye mkutano wa “WMO-IOC Joint Collaborative Board” uliofanyika tarehe 16 Juni, 2020  kuhusiana na vipaumbele vya maeneo ya ushirikiano kati ya WMO na IOC.

Baadhi ya washiriki wa mkutano wa “WMO-IOC Joint Collaborative Board” uliofanyika tarehe 16 Juni, 2020 wakichangia mijadala katika mkutano huo. Washiriki walio pichani kutoka upande wa kushoto ni mratibu wa Mkutano Bi. Sarah Grimes kutoka Sekretarieti ya  Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Mwenyekiti Mwenza wa WMO-IOC Joint Collaborative Board”, Dkt. Louis Uccellin, ambaye pia ni Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Hali ya Hewa ya Marekani na Bi. Monika Breuch-Moritz, ambaye ni Afisa kutoka Sekretarieti ya IOC.

Dar es Salaam; 

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi amesisitiza  kwamba suala la kuwajengea uwezo wataalamu wa hali ya hewa wanaotoa huduma kwa watumiaji wa bahari ni la umuhimu wa kipekee ili kuweza kukidhi mahitaji ya wadau hao wa bahari. 


Amezungumza hayo wakati akishiriki katika mkutano wa Bodi ya Mashirikiano kati ya WMO na Kamisheni ya Kimataifa ya Masuala ya Huduma za Hali ya Hewa kwa watumiaji wa Bahari (WMO-Intergovernmental Oceanographic Commission Collaborative Board (WMO-IOC JCB)) uliofanyika tarehe 16 Juni, 2020 kwa njia ya mtandao (videoconference). 


“Taasisi nyingi za Hali ya Hewa zina vituo vya kufuatilia hali ya bahari na kutoa huduma kwa wadau, lakini wataalamu bado hawajapewa ujuzi wa kutosha kuhusiana na mahitaji ya wadau. Hivyo tunahitaji kushughulikia masuala muhimu ya kisera na kimkakati yatakayowezesha kujenga uwezo kwa wataalamu katika ngazi ya nchi, kwani wataalamu hao bado hawajapewa elimu na ujuzi wa kutosha kukidhi mahitaji ya wadau wa bahari wanaowahudumia”. Alisema Dkt. Kijazi.


Aidha, Dkt. Kijazi alitaja kipaumbele kingine kuwa ni kuimarishwa kwa miundombinu ya upimaji na ufuatiliaji katika maeneo ya bahari ili kuwezesha upatikanaji wa takwimu ambazo ni muhimu katika utoaji wa huduma katika sekta hii, pamoja na ushirikiano kati ya taasisi husika kuanzia ngazi ya nchi.


Bodi ya mashirikiano katika ya WMO na IOC (WMO-IOC Joint Collaborative Board) huratibu maeneo ya mashirikiano kati ya WMO na IOC, na kwa sasa pamoja na masuala mengine itashughulikia pia suala la kujenga uwezo katika maeneo ya mashirikiano. Miongoni mwa masuala yaliyojadiliwa katika mkutano huo ni pamoja rasimu ya mkakati wa miaka kumi (10) wa kujenga uwezo, ambao utahusisha utaratibu wa kufanya kazi pamoja; utaratibu wa kushirikiana na washirika wengine; na uendelevu katika shughuli za kujenga uwezo. 


Bodi hiyo ilikutana kwa lengo la kujadili vipaumbele vya maeneo ya ushirikiano yanayohitaji kujengewa uwezo, ambayo yatashughulikiwa na majopo ya kujenga uwezo ya WMO na IOC. Dkt. Kijazi ni  Mwenyekiti wa Jopo la WMO la kujenga uwezo (WMO Capacity Development Panel).

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...