Tuesday, June 9, 2020

TANZANIA YAONGOZA MKUTANO WA KUWIANISHA SHUGHULI ZA UTOAJI HUDUMA ZA HALI YA HEWA KATIKA UKANDA WA SADC.

Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO, Dkt. Agnes Kijazi akiongoza Mkutano wa SADC Sekta ya Hali ya Hewa uliofanyika kwa njia ya mtandao katika katika kituo cha kimataifa cha mikutano cha Mwalimu Julius Nyerere (JNICC), Jijini, Dar es Salaam. Aliyekaa kulia kwake ni Meneja Ushirikiano wa Hali ya Hewa Kimataifa wa TMA, Bw. Wibert Muruke akifuatilia majadiliano ya kikao.

Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO, Dkt. Agnes Kijazi akijibu hoja za wajumbe wa mkutano wa SADC Sekta ya Hali ya Hewa. Aliyekaa kulia kwake  ni Meneja Ushirikiano wa Hali ya Hewa Kimataifa wa TMA, Bw. Wibert Muruke akiandika muhtasari wa kikao.


Dar es Salaam; Tarehe 04/06/2020
Wakuu wa Taasisi za Hali ya Hewa za Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamefanya mkutano wa kuwianisha shughuli za utoaji wa huduma za hali ya hewa katika Ukanda wa SADC (Harmonizing SADC Strategy and Action Plan on Meteorology).

Mkutano huo ulifanyika tarehe 4 Juni 2020 kwa njia ya mtandao (videoconference) chini ya Uenyekiti wa Tanzania kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), ambapo  Mkurugenzi Mkuu wa  TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi aliongoza mkutano huo.

Akiwasilisha hotuba yake fupi ya ufunguzi, Dkt. Kijazi alisema kuwa dhumuni kuu la mkutano huo ni kuwianisha shughuli  za  utoaji wa huduma za hali ya hewa katika Ukanda wa SADC ili zichangie ipasavyo katika kutatua changamoto za  sekta ya hali ya hewa katika Ukanda wa SADC kwa maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii katika Nchi Wanachama. Dkt. Kijazi alizitaja baadhi ya changamoto zinazokabili sekta ya hali ya hewa kuwa ni pamoja na uhaba wa miundombinu ya kupima hali ya hewa; kuchakata takwimu za hali ya hewa; na kubadilishana takwimu za hali ya hewa.
Dkt. Kijazi aliendelea kueleza kwamba, licha ya jitihada kubwa zinazofanywa na Nchi Wanachama kuboresha huduma za hali ya hewa, utatuzi wa changamoto hizo unahitaji pia juhudi za pamoja za wadau na taasisi zote husika ili kuwianisha shughuli za huduma ya hali ya hewa za Kikanda.
 “Licha ya jitihada zilizofanywa na Nchi wanachama katika uboreshaji wa huduma za hali ya hewa, bado kuna changamoto nyingi.  Kama sehemu ya utatuzi  wa changamoto hizi, mkutano huu utajadili namna ya kuwianisha shughuli za huduma za hali ya hewa za Kikanda” alisema Dkt. Kijazi na kuwaomba wajumbe kushiriki kikamilifu na kutoa maoni  yatakayofanikisha  uwianishaji wa shughuli hizo.

Akitoa maelezo ya awali kuhusiana na mkutano huo, Afisa Mwandamizi wa Programu ya Hali ya Hewa katika Secretarieti ya SADC, Dkt. Prithiviraj Booneeady, alisema hatua ya kuwianisha shughuli za huduma za hali ya hewa ni takwa la  Itifaki ya SADC ya Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa (SADC Protocol on Transport, Communication and Meteorology) unaozitaka Nchi Wanachama kuwianisha shughuli za huduma za hali ya hewa ili kuwezesha ushirikiano wa Kikanda na kuimarisha uwezo wa Nchi Wanachama katika utoaji wa huduma za hali ya hewa.  Kwa mujibu wa Dkt. Booneeady, hatua hiyo itasaidia juhudi za pamoja katika kuimarisha uwezo wa Nchi Wanachama katika kukabiliana na majanga yanayotokana na hali mbaya ya hewa.
Mada zilizowasilisha katika mkutano huo ni pamoja na zinazohusiana na programu za Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) katika ukanda wa SADC; Programu za Secretarieti ya SADC zinazohusiana na sekta ya hali ya hewa;  Programu za Umoja wa Taasisi za Hali ya Hewa Kusini mwa Afrika (SADC MASA). Mkutano ulijadili shughuli hizo na kutoa mapendekezo. Mapendekezo yaliyotolewa ni pamoja na kurejewa upya kwa Itifaki ya Uchukuzi, Mawasiliano na Hali ya Hewa (SADC Protocol on Transport, Communication and Meteorology) ili ukidhi mahitaji ya sasa ya sekta ya hali ya hewa.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...