Thursday, February 13, 2020

TMA YATOA UTABIRI WA MSIMU WA MVUA ZA MASIKA KWA MAENEO YANAYOPATA MVUA MARA MBILI KWA MWAKA.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania(TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Dkt. Agnes Kijazi, mbele ya waandishi wa habari  akichambua  mwenendo wa mifumo ya hali ya hewa na mwelekeo wa mvua za msimu wa Masika (Machi – Mei 2020) katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya tatu, Ubungo Plaza – Dar es Salaam, Tanzania.

Mtaalamu wa hali ya hewa kutoka TMA, Bi. Rosemary Senyagwa akitoa tathmini ya mvua za msimu wa Vuli (Novemba 2019 hadi Aprili 2020), kabla ya kutolewa rasmi mwelekeo wa msimu wa mvua za MASIKA kwa kipindi cha mwezi Machi hadi Mei 2020

Mwandishi wa Habari kutoka Idhaa ya Kiswahili ya Deutsche Welle (DW) Bi. Hawa Bihoga akiuliza swali katika mkutano wa wanahabari wa kutoa mwelekeo wa mvua za Msimu wa Masika (Machi – Mei 2020) katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya tatu, Ubungo Plaza – Dar es Salaam, Tanzania.



Vyombo mbalimbali vya habari vikichukua taarifa wakati wa mkutano wa wanahabari wa kutoa mwelekeo wa mvua za Msimu wa Masika (Machi – Mei 2020) katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya tatu, Ubungo Plaza – Dar es Salaam, Tanzania.

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa utabiri wa msimu wa mvua za Masika kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka. Akizungumza wakati wa mkutano na vyombo vya habari, Mkurugenzi Mkuu Dkt. Agnes Kijazi alisema maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka ni  Mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro, Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani ikijumuisha kisiwa cha Mafia Tanga na maeneo ya kaskazini mwa mkoa wa Morogoro pamoja na  visiwa vya Unguja na Pemba, Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Mara  pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma. 
 
Mvua za Masika kwa kipindi cha Machi hadi Mei, 2020 zinatarajiwa kuwa za wastani hadi juu ya wastani katika maeneo ya mkoa wa Tanga, visiwa vya Unguja na Pemba, maeneo mengi ya mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro, mashariki mwa mkoa wa Geita pamoja na mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Mara”. Alisema Dkt. Kijazi

Aliendelea kwa kuyataja maeneo ya mkoa wa Kagera, magharibi mwa mkoa wa Geita, kaskazini mwa mkoa wa Kigoma, Dar es Salaam, Pwani ikijumuisha kisiwa cha Mafia pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Morogoro kuwa yanatarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani. Aidha, Dkt. Kijazi alifafanua kuhusu mvua za nje ya msimu zinazoendelea katika maeneo yanayopata mvua za Masika hususan maeneo yaliyopo katika pwani ya kaskazini, mvua hizo zinatarajiwa kuendelea na kuungana na msimu wa mvua wa Masika 2020.

Akizungumzia athari zinazoweza kujitokeza, Dkt. Kijazi alisema vipindi vifupi vya mvua kubwa vinaweza kujitokeza hata katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani, hivyo jamii inashauriwa kuchukua hatua stahiki kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.


No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...