Friday, February 28, 2020

TANZANIA YAISHUKURU JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI KWA USHIRIKIANO WALIOTOA KUMUUNGA MKONO MKURUGENZI MKUU WA TMA KATIKA KINYANG’ANYIRO CHA NAFASI YA MAKAMU WA TATU WA RAIS WA WMO.



Kigali, Rwanda; Tarehe 08 Februari, 2020;
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ambaye pia ni Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Lawrence Kijazi amewashukuru wakuu wa Taasisi za Hali ya Hewa katika Jumuia ya Afrika Mashariki kwa ushirikiano mkubwa waliompatia katika kuwania nafasi ya Makamu Watatu wa Rais wa WMO
 
“Naomba ushirikiano huu (teamwork) tulio uonyesha katika kipindi cha uchaguzi uendelee pia katika utekelezaji wa majukumu ya Kikanda kwenye uboreshaji na utoaji huduma za hali ya hewa”. Alizungumza Dkt. Kijazi wakati akitoa shukrani hizo kwa niaba ya nchi katika Mkutano wa Wakuu wa Taasisi za Hali ya Hewa za Afrika Mashariki (Heads of EAC Meteorological Service Meeting), uliofanyika tarehe 7 hadi 8 Februari, 2020, Kigali, Rwanda.
 
Dkt. Kijazi  alisisitiza umuhimu wa kufanya vikao  kazi vya pamoja ili kuhakikisha masuala muhimu yanayohusiana na utoaji huduma ikiwa ni pamoja na kubadilishana taarifa za hali ya hewa yanapewa kipaombele.
 
“Kwa kutambua kuwa hali ya hewa haina mipaka ya nchi, hivyo ni wakati muafaka kwa Taasisi zetu kuwa na vikao vya kujadili masuala mbalimbali ya kuboresha huduma, tukichukua mfano wa hali ya hatari iliyopo kwa sasa ya uvamizi wa nzige na mlipuko wa virusi vya corona ambapo kwa kiasi kikubwa hali hizo zinauhusiano na hali ya hewa”. Alisisitiza Dkt. Kijazi.
 
Masuala muhimu yaliyojadiliwa katika mkutano huo ni pamoja na nchi wanachama wa EAC kuendelea kuboresha utoaji wa huduma za hali ya hewa kwa viwango vya kimataifa ikiwa pamoja na kupata cheti cha ubora cha utoaji wa huduma za hali ya hewa yaani ISO 9001:2015 (Tanzania kupitia TMA imeshapata cheti hicho cha ubora cha utoaji wa huduma za hali ya hewa katika sekta ya usafiri wa anga). Vile vile nchi wanachama wa EAC kuongeza kasi katika upanuaji wa mtandao wa vituo vya upimaji wa hali ya hewa na mawasiliano ya data hizo na ubadilishanaji wa ujuzi kuhusu matumizi ya teknolojia mpya za upimaji wa hali ya hewa katika eneo la Jumuia ya Afrika Mashariki.

Aidha, suala la uchangiaji wa huduma za hali ya hewa kwa sekta zinazotumia huduma za hali ya hewa kibiashara (cost recovery) lilipewa kipaombele pamoja na taasisi za hali ya hewa kuendelea kuhifadhi data za hali ya hewa kwa kutumia kanzi data ambazo ni imara kutokana na uhitaji wa matumizi ya data hizi katika maendeleo endelevu ya nchi za Jumuia ya Afrika Mashariki.

Kutokana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa yanayosababisha mabadiliko makubwa katika mifumo ya hali ya hewa mkutano huo umefikia makubaliano kwamba nchi wanachama waendelee kufanya tafiti na kushiriki katika mijadala ya kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa kimataifa kwa maendeleo endelevu ya nchi hizo.  Tanzania imeng’ara katika mkutano huo kwa kuonekana kwamba imetekeleza makubaliano yaliyofikiwa katika mkutano wa awali kwa kiwango cha kuridhisha na hiyo imepelekea TMA kupewa jukumu la kuzisaidia taasis zingine za Hali ya Hewa katika Jumuia ya Afrika Mashariki zenye changamoto katika utoaji wa huduma ikiwemo Burundi na Sudan ya kusini.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...