Friday, November 8, 2019

MHE. MONGELA: TMA YAENDELEA NA UBORESHAJI WA HUDUMA ZA HALI YA HEWA ZIWA VIKTORIA

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. John Mongella (katikati) katika picha ya pamoja wakati wa warsha ya “Utoaji Elimu Kuhusiana na Huduma za Hali ya Hewa Zinazozingatia Athari (Impact Based Early Warning Services Awareness Raising Workshop)” katika Ukumbi wa Chuo cha Benki Kuu, Mwanza, Tarehe 06 hadi 09 Novemba 2019. Kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa TMA Dkt. Agnes Kijazi na kushoto ni Mkurugenzi wa Utafiti  na Matumizi ya Huduma za Hali ya Hewa wa TMA Dkt. Ladislaus Chang’a.


Baadhi ya washiriki wa warsha ya “Utoaji Elimu Kuhusiana na Huduma za Hali ya Hewa Zinazozingatia Athari (Impact Based Early Warning Services Awareness Raising Workshop)” wakishangilia jambo  


Kikundi cha ngoma ya Kisukuma Bujora kikiwasilisha ujumbe wa matumizi ya taarifa za hali ya hewa wakati wa ufunguzi wa  warsha ya “Utoaji Elimu Kuhusiana na Huduma za Hali ya Hewa Zinazozingatia Athari (Impact Based Early Warning Services Awareness Raising Workshop)”


Mwanza, 06/11/2019: Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe. John Mongela amesema kuwa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imeendelea kuboresha huduma za hali ya hewa katika Ziwa Viktoria ambazo zimewanufaisha wananchi wanaofanya shughuli za uvuvi ziwani na hivyo kuchangia kupunguza majanga yatokanayo na hali mbaya ya hewa.
Aidha, Mhe. Mongela aliendelea kwa kuipongeza TMA kwa kazi nzuri inayoifanya katika kufanikisha maboresho ya huduma hizo wakati akifungua rasmi, warsha ya “Utoaji Elimu Kuhusiana na Huduma za Hali ya Hewa Zinazozingatia Athari (Impact Based Early Warning Services Awareness Raising Workshop)” inayofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Benki Kuu, Mwanza, Tarehe 06 hadi 09 Novemba 2019.
 “Tunawapongeza sana TMA kwa kazi nzuri ya kuendelea kuboresha huduma za hali ya hewa katika  Ziwa Viktoria, ambazo zimenufaisha wananchi wanaofanya shughuli za uvuvi ziwani hivyo kuchangia kupunguza majanga yatokanayo na hali mbaya ya hewa”. Alisema Mhe. Mongela

Awali, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi alitoa taarifa kuwa warsha hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa WMO wa kuboresha huduma za hali ya hewa kwa watumiaji wa Ziwa Viktoria uitwao “High impact Weather lAke sYstems (HIGHWAY), ambao kwa hapa Tanzania unatekelezwa katika wilaya za Sengerema, Mwanza na Muleba, Kagera kwa ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Uingereza (DFID).

Katika upande mwengine, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza alimpongeza Mkurugenzi Mkuu wa TMA kwa kuchaguliwa kuwa Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO, na kusema kwamba mafanikio hayo yamekuja kutokana na utendaji kazi  mzuri wa Dkt. Kijazi na wafanyakazi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa, na kuchaguliwa kwake kumeliletea sifa na heshima kubwa Taifa la Tanzania.

Lengo la warsha hiyo ni  kuwajengea uwezo wadau wa huduma za hali ya hewa wa sekta ya uvuvi ili kuzielewa na kuzitumia au kuziwasilisha ipasavyo huduma hizo ambazo ni mahususi kwa sekta ya uvuvi.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...