Wednesday, October 9, 2019

WANAHABARI WAKUMBUSHWA UMUHIMU WA KUFIKISHA HABARI ZA HALI MBAYA YA HEWA KWA WAKATI.

Wanahabari katika picha ya pamoja wakati wa warsha ya wanahabari ya kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 na athari zinazoweza kujitokeza.
Wadau katika picha ya pamoja wakati wa warsha ya wanahabari ya kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 na athari zinazoweza kujitokeza.
Mmoja wa wadau akichangia mada wakati wa warsha ya wanahabari ya kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 na athari zinazoweza kujitokeza.

Tarehe 09/10/2019: Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imekutana na wadau wa sekta mbalimbali na wanahabari ili kujadili mwelekeo wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 na athari zinazoweza kujitokeza.

Akiongea wakati wa ufunguzi wa warsha hiyo, mgeni rasmi ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO, Dkt. Agnes Kijazi alisisitiza umuhimu wa vyombo vya habari katika kusambaza taarifa za hali ya hewa ukiwemo utabiri wa hali ya hewa na tahadhari ya hali mbaya ya hewa, huku akitolea mfano wa athari zilizoanza kuonekana mwanzoni mwa msimu wa mvua za vuli za mwaka huu.

“Napenda kusisitiza umuhimu wa warsha hizi ni kuhakikisha jamii tunayoenda kuihudumia inapata taarifa sahihi, kwa wakati na kwa lugha inayoeleweka kirahisi, msimu wa vuli umeanza na matukio mengi ya upepo mkali, mawimbi makubwa na mvua kubwa hivyo taarifa hizi zinakuwa na manufaa pale ambapo zinatumika kwa wakati’, alisema Dkt. Kijazi. Aidha, alivishukuru vyombo vya habari nchini kwa kuendelea kusambaza kwa wakati taarifa za hali ya hewa ikiwa pamoja na tahadhari za hali mbaya ya hewa.  

Kwa upande mwingine, Dkt.Kijazi alifafanua kwa wadau wa sekta mbalimbali sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Na.2 ya 2019. Alisema lengo la Sheria hiyo ni kuboresha huduma za hali ya hewa hapa nchini na kutoa mwongozo wa ushiriki wa sekta mbalimbali  katika matumizi ya huduma hizo. Dkt. Kijazi alifafanua vipengele vya sheria hiyo vinavyowahusu wadau wa huduma za hali ya hewa alipokuwa anafunga mkutano huo wa wadau.

Aidha, wadau hao walipata fursa ya kutoa ushauri wa athari zinazoweza kujitokeza kulingana na utabiri wa msimu wa mwaka ulioandaliwa kwa mikoa inayopata mvua za msimu mara moja kwa mwaka ambayo ni  mikoa ya kanda ya magharibi, kati, nyanda za juu kusini magharibi, kusini mwa nchi, ukanda wa pwani ya kusini pamoja na maeneo yaliyoko kusini mwa mkoa wa Morogoro.

Kwa upande wa wanahabari waliahidi kuendelea kutoa taarifa sahihi za hali ya hewa kama zinavyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania na waliishukuru TMA kwa kuendesha warsha hizo ambazo zimeendelea kuwajengea uwezo wa kuelewa lugha inayotumika katika utabiri wa hali ya hewa.

 Warsha hizo zilifanyika tarehe 08/10/2019 kwa kuwakutanisha wadau wa sekta mbalimbali na tarehe 09/10/2019 kwa kuwakutanisha wanahabari. Utabiri wa msimu wa mvua za mwaka kwa kipindi cha mwezi Novemba 2019 hadi Aprili 2020 unatarajiwa kutolewa rasmi kwa umma kupitia vyombo vya habari siku ya Alhamisi, tarehe 10/10/2019,makao makuu ya ofisi za TMA, saa tano kamili asubuhi.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...