Wednesday, February 22, 2023

TMA YATOA UTABIRI WA MSIMU WA MVUA ZA MASIKA 2023 KWA MAENEO YANAYOPATA MVUA MARA MBILI KWA MWAKA.


Dar es Salaam, Tarehe 22/02/2023;

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2023 kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka. Akizungumza wakati wa mkutano na vyombo vya habari katika Ofisi za TMA-Dar es Salaam, Ubungo Plaza, tarehe 22/02/2023, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dkt. Ladislaus Chang’a alisema maeneo mengi ya nchi yanayopata misimu miwili ya mvua yanatarajiwa kupata mvua za wastani hadi chini ya wastani.

 

“Mvua za wastani hadi chini ya wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya nchi yayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka isipokuwa maeneo machache ya mikoa ya Dar es Salaam, pwani (ikijumuisha mafia),kaskazini mwa Morogoro pamoja na Kisiwa cha Unguja ambapo mvua za wastani hadi juu ya wastani zinatarajiwa”. Alisema Dkt. Chang’a.

 

Aidha, aliongezea kuwa “Ongezeko la mvua linatarajiwa katika kipindi cha mwezi Mei 2023, hususan katika maeneo ya pwani ya kaskazini”.Alisema Dkt. Chang’a.

 

Mvua za Masika zinatarajiwa kuanza mwezi Machi 2023 katika maeneo mengi na zinatarajiwa kuisha katika wiki ya nne ya Mwezi Mei 2023, katika maeneo mengi ingawa mwendelezo wa mvua za nje ya msimu unatarajiwa mwezi Juni 2023 katika maeneo machache ya mikoa ya Tanga, Dar es Salaam, Morogoro kaskazini, Pwani, Kisiwa cha Mafia, kisiwa cha unguja na Pemba.

 

Akizungumzia athari zinazoweza kujitokeza, Dkt. Chang’a alisema vipindi vifupi vya mvua kubwa vinaweza kujitokeza hivyo kuweza kusababisha mafuriko, uharibifu wa miundombinu, upotevu wa mali na maisha, milipuko ya magonjwa pamoja na athari nyingine zitokanazo na mvua nyingi.

 

Kwa taarifa zaidi tembelea; www.meteo.go.tz https://www.meteo.go.tz/weather_forecasts/seasonal-weather-forecast

 

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...