Friday, October 30, 2020

TMA YAENDELEA KUJIPANGA KUTOA UTABIRI KWA MAENEO MADOGO MADOGO YA NCHI.

Dar es salaam, Tarehe 23/10/2020 “Tunaendelea kujipanga ili tuje kutoa utabiri wa maeneo madogo madogo, katika ngazi ya Wilaya, Tarafa na hata Kata”, aliongea hayo Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Dkt. Agnes Kijazi alipokuwa akifungua kikao kazi kilichowakutanisha wataalam wa TMA pamoja na maafisa Ugani kutoka katika wilaya ya Kilolo – Iringa, Kongwa – Dodoma, Ruangwa – Lindi na Uyui – Tabora ili kujadili utabiri wa msimu wa mvua za Novemba 2020 – Aprili 2021 kwa maeneo madogomadogo katika ngazi ya Wilaya kilichofanyikia Tarehe 23 Oktoba 2020 katika ukumbi wa mikutano wa TMA, Ghorofa ya Tatu- Ubungo plaza. Aidha, Dkt. Kijazi aliwasisitiza maafisa ugani mara watakaporudi katika maeneo yao ya kazi kupeleka elimu hiyo ya hali ya hewa waliyoipata kwa wananchi ili waweze kutumia vyema utabiri wa hali ya hewa katika shughuli zao za kilimo. Alieleza kwamba wapo baadhi ya wananchi wanaotumia utabiri wa asili (Indigenous knowledge), hata hivyo utabiri huo katika kipindi hiki ambacho dunia imekumbwa na mabadiliko ya tabia nchi unakuwa si wa kutegemea, ni vyema kufuatilia utabiri unaotolewa na TMA ambao umejikita katika uchambuzi wa mifumo ya kisayansi. Kwa upande wa wadau wakitoa mrejeo wa utabiri wa msimu wa mvua za Novemba 2019 – Aprili 2020 kwa maeneo madogomadogo katika ngazi ya Wilaya, waliipongeza TMA kutokana na utabiri kwenda sawa na kile kilichotokea katika maeneo yao. Aidha waliishukuru TMA kwa elimu muhimu waliyopata kupitia kikao kazi hicho, ambayo wameahidi kuifikisha kwa wananchi katika maeneo yao ya kazi ili kusaidia kuongeza uzalishaji katika shughuli za kilimo.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...