Tuesday, October 20, 2020

DKT. NYENZI ATOA RAI KWA WADAU KUSHIRIKIANA NA TMA KATIKA KUELIMISHA WANANCHI, UMUHIMU WA MATUMIZI YA TAARIFA ZA HALI YA HEWA.

Dar es Salaam, Tarehe; 19/10/2020. Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ambaye pia alikuwa ni mgeni rasmi katika mkutano wa wadau wa maandalizi ya kutoa utabiri wa mvua za msimu wa vuli kwa maeneo yanayopata mvua mara moja kwa mwaka Dkt. Buruhani Nyenzi ametoa rai kwa wadau kutoka sekta mbalimbali kushirikiana na TMA katika kuelimisha wananchi ikiwemo watendaji kutoka katika sekta zao juu ya umuhimu wa matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika shughuli zao za kila siku, aliyasema hayo alipokuwa akifungua mkutano huo uliofanyika katika Ukumbi wa mikutano wa TMA, Makao Makuu - Ubungo Plaza, Dar es salaam, Tarehe 19 Oktoba 2020. “Ninatoa rai kwenu wadau kushirikiana na TMA katika kuelimisha wananchi ikiwemo watendaji kutoka katika sekta zenu, juu ya umuhimu wa matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika shughuli zao za kila siku ili kuepusha au kupunguza athari zitokanazo na hali mbaya ya hewa sambamba na kulinda mafanikio ya uwekezaji na miundombinu iliyofanywa na Serikali”. Alisisitiza Dkt. Nyenzi. Katika hotuba yake Dkt. Nyenzi aliwakumbusha wadau kuwa maboresho yaliyofanywa na TMA yamesababisha kutoa utabiri wenye viwango vya usahihi uliofikia asilimia 94.4% kwa msimu wa mvua za Novemba 2019 hadi Aprili 2020, kiwango ambacho kimezidi kiwango kinachokubalika na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) cha asilimia 70%, ambapo aliishukuru sana Serikali kwa kuendelea kuiwezesha TMA mpaka kufikia mafanikio hayo. Pia katika hotuba yake alitoa pole kwa wananchi wote walioguswa na maafa yaliyotokana na mvua kubwa iliyotokea Tarehe 13 na 15 Oktoba, 2020 na kuomba washiriki kusimama kwa dakika moja kama ishara ya kuwakumbuka wale waliofariki kutokana na maafa hayo. Pia alieleza kuwa kwa hivi sasa taarifa za hali ya hewa zikitumika ipasavyo katika sekta mbalimbali itasaidia upatikanaji wa malighafi zitakazotosheleza uendeshaji wa viwanda vyetu, hivyo kusaidia kufikia malengo ya Taifa ya kujenga uchumi wa viwanda. Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Dkt. Agnes Kijazi aliwashukuru wadau kwa ushirikiano mkubwa wanaotoa katika kuhakikisha huduma za hali ya hewa zinatumika katika sekta zao na kuwashukuru kwa kushiriki vikao vya wadau ambavyo vinafanyika kila mara unapotolewa utabiri wa msimu. Aidha, wadau walioudhuria mkutano huo, waliipongeza TMA kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kutoa utabiri ambao kwa kiwango kikubwa umekuwa na uhalisia na kuahidi kuendelea kutumia utabiri unaotolewa na TMA katika kupanga mipango yao ya kiutendaji na ya maendeleo katika sekta zao. Walisema utabiri uliopita ulikuwa wa manufaa sana katika sekta zao na umesaidia kupunguza hasara ambazo zingetokea endapo utabiri usingetumika.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...