Tuesday, January 7, 2020

ONGEZEKO LA HALI YA JOTO KWA BAADHI YA MAENEO NCHINI



Dar es Salaam, 06 Januari 2020:
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inatoa taarifa juu ya hali ya ongezekeo la joto katika baadhi ya maeneo hapa nchini.

Kwa kawaida kipindi cha miezi ya Oktoba hadi Machi kila mwaka jua la utosi linakuwa katika maeneo ya kizio cha kusini mwa dunia. Tanzania ikiwa ni moja ya nchi zilizopo katika kizio cha kusini, huwa na hali ya joto kali katika maeneo mengi ikilinganishwa na miezi mingine. Hapa nchini, vipindi vya jua la utosi vinafikia kilele kati ya mwishoni mwa mwezi Novemba wakati jua la utosi likiwa linaelekea kusini (Tropiki ya Kaprikoni) na hali hiyo hujirudia tena mwezi Februari wakati jua la utosi likiwa linaelekea kaskazini (Tropiki ya Kansa). Jua la utosi huambatana na hali ya Joto kali kwa sababu kipindi hicho ndipo uso wa dunia katika eneo tajwa huwa karibu zaidi na jua kuliko maeneo mengine. Hali hii hujitokeza zaidi kunapokuwepo na upungufu wa mawingu na mvua ambazo husaidia katika kupunguza hali ya joto katika kipindi husika.

Nyakati za usiku pia kunaonekana kuwa na hali ya joto kutokana na kuwepo na kiwango kikubwa cha unyevunyevu angani kinachofika asilimia themanini na zaidi kwa baadhi ya maeneo. Unyevunyevu huo hutunza hali ya joto litokanalo mionzi ya jua na hivyo kuleta hali ya fukuto.

Kwa sasa msimu wa mvua za Vuli umeisha katika maeneo mengi hususan  yale yaliyoko ukanda wa Pwani, Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki na baadhi ya maeneo ya mikoa ya Simiyu, Shinyanga hivyo kuwa na joto kali. Pamoja na maeneo hayo mkoa wa Tabora nao unatarajiwa kuendelea kupata  vipindi vya joto kali. Vipindi hivi vya joto kali vinatarajiwa kuendelea kuongezeka katika mwezi Februari 2020 ambapo jua litakuwa la utosi hapa nchini. Baada ya kipindi hicho  hali ya joto inatarajiwa kuanza kupungua hasa kuelekea mwezi Machi ambapo mtawanyiko wa mvua unatarajiwa kuongezeka katika maeneo yanayopata mvua za msimu na kuanza kwa msimu wa mvua za masika  na hivyo kupunguza hali ya joto kali.

Hata hivyo, taarifa za mwenendo wa joto, zinaendelea kutolewa katika utabiri wa kila siku na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, hivyo tunatoa wito kwa wananchi kuendelea kufuatilia taarifa hizo na kuchukua hatua stahiki  kila inapobidi.


No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...