Friday, June 28, 2019

BODI YAMPONGEZA DKT. KIJAZI KUCHAGULIWA MAKAMU WA TATU WA RAIS WA WMO







Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) imempongeza Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na katibu wa hiyo kwa kuchaguliwa kwa kishindo kuwa makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO).

Akizungumzia pongezi hizo na ushindi uliopatikana wakati wa kikao cha 55 cha Bodi, mwenyekiti wa Bodi Dkt. Buruhani Nyenzi aliwasilisha pongezi za dhati kutoka kwa wajumbe wote na kukiri kuwa nafasi iliyopatikana ni moja ya njia za kuzidi kuipandisha Tanzania juu katika anga za kimataifa.

‘Bodi inatoa pongezi za dhati kwa Dkt. Kijazi kwa kuchaguliwa kushika nafasi ya juu WMO, kwa kuwa kupitia nafasi hiyo Tanzania inazidi kupanda juu katika anga za kimataifa’. Aliongea Dkt. Nyenzi

Mwenyekiti huyo aliendelea kuwakumbusha washiriki wa kikao hicho kuwa mafanikio ambayo Tanzania imeyapata yanachangiwa na mambo mengi. Alisema jambo la kwanza na la muhimu ni sifa za Dkt. Kijazi kama mgombea wa nafasi hiyo, pili kukubalika na kukua kwa diplomasia ya Tanzania nje ya nchi na tatu sifa nzuri za Watanzania ambao wamewahi kufanya kazi WMO akiwemo yeye mwenyewe.

Aidha, Dkt. Nyenzi alionesha furaha yake namna ambavyo TMA inafanya kazi kwa umoja na upendo baina ya wafanyakazi, akitolea mfano mapokezi yaliyofanywa na wafanyakazi kwa kiongozi wao ambaye ni Dkt. Kijazi.

Dkt. Kijazi alichaguliwa kuwa makamu wa tatu wa Rais wa WMO kwenye mkutano wa 18 wa shirika hilo uliofanyika jijini Geneva, Uswisi tarehe 03-14 Juni 2019 kwa kipindi cha miaka minne, akiwa mwanamke na makamu wa tatu wa Rais wa kwanza kutoka nchi zinazoendelea hususani nchi za Afrika zilizo kusini mwa jangwa la Sahara.

IMEANDALIWA NA;
OFISI YA UHUSIANO
MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA (TMA)

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...