Friday, March 25, 2022

DKT. KIJAZI AELEZA MAFANIKIO YA UMOJA WA TAASISI ZA HALI YA HEWA ZA NCHI ZA SADC (MASA) YALIYOPATIKANA CHINI YA UENYEKITI WA TANZANIA


Picha Na 1: Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za  Umoja wa Taasisi za Hali ya Hewa za nchi za SADC “Meteorological Association of Southern Africa (MASA)” katika  kipindi cha Uenyekiti wa Tanzania ((Agosti 2019 hadi Machi 2022), kwenye mkutano Mkuu wa 14 wa MASA,  uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 17 Machi, 2022, ambapo Dkt. Kijazi aliongoza Mkutano huo akiwa Mwenyekiti anayemaliza muda wake.  Kulia kwake ni Meneja Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Wilbert Muruke akifuatilia majadiliano ya mkutano huo


Picha Na 2: Baadhi ya washiriki wa mkutano Mkuu wa 14 wa Umoja wa Taasisi za Hali ya Hewa za nchi za SADC “Meteorological Association of Southern Africa (MASA)” katika picha ya pamoja (kwa njia ya mtandao). 

 


 Mwanza: Tarehe 17/03/2022

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi, ameeleza mafanikio ambayo Umoja wa Taasisi za Hali ya Hewa za Nchi za SADC “Meteorological Association of Southern Africa (MASA)” umepata chini ya Uenyekiti wa Tanzania, katika kipindi cha Agosti 2019 hadi Machi 2022, licha ya changamoto ya ugonjwa wa UVIKO-19.

Dkt. Kijazi ambaye alikuwa Mwenyekiti wa MASA katika kipindi hicho cha miaka miwili na miezi 6, alieleza mafanikio hayo alipowasilisha taarifa ya utekelezaji wa shughuli za MASA katika kipindi cha uongozi wake, kwenye mkutano mkuu wa 14 wa Umoja huo “Fourteenth MASA Annual General Meeting (MASA AGM-14)” uliofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 17 Machi, 2022. Katika taarifa yake, Dkt. Kijazi alieleza kwamba licha ya changamoto ya ugonjwa wa UVIKO-19 iliyojitokeza katika kipindi hicho na kuathiri shughuli za MASA, mafanikio mbalimbali yalipatikana yaliyohusisha majukumu ya Bodi na Sekretarieti ya MASA.

“Tunafahamu kuwa changamojto ya ugonjwa wa UVIKO-19 iliathiri shughuli nyingi za MASA zilizokuwa zimepangwa kutekelezwa kutokana na masharti ya kusafiri na kufanya mikutano yaliyotolewa na Mamlaka za Afya. Hata hivyo, licha ya changamoto hiyo, napenda kuwajulisha kwamba Bodi ilijitahidi kutekeleza shughuli za MASA, ikiwa ni pamoja na maamuzi ya Waheshimiwa Mawaziri wa SADC, na kuna mafanikio kadha wa kadha ambayo ni muhimu Wanachama wa MASA kufahamishwa”. alisema Dkt. Kijazi na kuendelea kutaja mafanikio hayo.

Miongoni mwa mafanikio aliyoeleza Dkt. Kijazi ni pamoja na: Kukamilika kwa mpango wa kuhuisha kazi za MASA (MASA Rescue Plan); kuandaliwa kwa mpangokazi wa utekelezaji wa mpango huo (MASA Rescue Plan Programme of action); Tanzania kujitolea kuwa mwenyeji wa Sekretarieti ya MASA; na mikutano ya Bodi ya MASA kufanyika kwa njia ya mtandao. Aidha, Dkt. Kijazi alifafanua zaidi kwamba athari za ugonjwa wa UVIKO-19 kwa shughuli za MASA zililitokana pia na kutetereka kwa hali ya kifedha kutokana na Nchi Wanachama kushindwa kulipa ada za uanachama za kila mwaka.

Katika hatua nyingine, MASA ilifanya uchaguzi wa viongozi wapya wa umoja huo katika nafasi ya Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, na wajumbe wa Bodi kwa kipindi kingine cha miaka miwili. Katika uchanguzi huo, Nchi ya Msumbiji ilichanguliwa kuwa Mweyekiti mpya wa MASA na Lesotho kuwa Makamu Mwenyekiti. Kwa upande wa Wajumbe wapya wa Bodi ya MASA waliochanguliwa ni Afrika ya Kusini, Tanzania, na Zambia. 

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...