Monday, March 23, 2026

UJUMBE WA MKURUGENZI MKUU TMA, DKT. LADISLAUS CHANG’A KATIKA SIKU YA HALI YA HEWA DUNIANI, TAREHE 23 MACHI, 2026.


Leo tunaungana na jumuiya ya kimataifa kuadhimisha Siku ya Hali ya Hewa Duniani (World Meteorological Day – WMD). Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), ikiwa Mamlaka ya Kitaifa yenye jukumu la kutoa huduma za hali ya hewa kwa umma, taasisi mbalimbali na watumiaji binafsi wa huduma maalum kwa ajili ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi, pamoja na kusimamia na kuratibu shughuli za hali ya hewa katika mipaka ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kutoa tahadhari na ushauri kuhusu matukio ya hali mbaya ya hewa kwa lengo la kulinda maisha ya watu na mali zao, inaungana na jumuiya ya hali ya hewa duniani kote kuadhimisha Siku ya Hali ya Hewa Duniani kwa mwaka 2026. Maadhimisho ya mwaka huu ni kumbukizi ya miaka 76 tangu kuanzishwa kwa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) tarehe 23 Machi 1950. Tanzania ni mojawapo ya nchi wanachama 193 wa WMO, ambapo kupitia TMA inaendelea kuthibitisha dhamira yake thabiti ya kuimarisha huduma za hali ya hewa ambazo ni msingi muhimu wa usalama, ustawi wa jamii na maendeleo endelevu ya taifa.

Kaulimbiu ya Siku ya Hali ya Hewa Duniani mwaka huu ni: “Pima hali ya hewa leo, ili kesho iwe salama" (Observing Today, Protecting Tomorrow)”. Kaulimbiu hii inalenga kusisitiza umuhimu wa kuimarisha mifumo ya uangazi wa hali ya hewa na matumizi sahihi ya data za hali ya hewa zinazokusanywa ili kuwezesha maamuzi yenye tija katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi. Taarifa hizi zimeendelea kusaidia kuongeza uzalishaji, usalama na ustahimilivu wa jamii yetu kwa sasa na kwa vizazi vijavyo. Kaulimbiu hii pia inatukumbusha sisi wataalamu wa hali ya hewa, wataalamu wa rasilimali maji, wanasayansi, watunga sera na wadau mbalimbali kuwa, uangazi na ufuatiliaji wa mifumo ya hali ya hewa ni msingi wa kazi zote tunazozifanya. Kuanzia vituo vya uangazi wa ardhini na anga za juu, RADA na mitandao ya uangazi wa maji, mifumo hii hutuwezesha kuelewa mienendo ya mifumo ya hali ya hewa, kutambua hatari zinazoweza kujitokeza, na kutoa taarifa sahihi za hali ya hewa pamoja na tahadhari za mapema kwa wakati muafaka. Kwa kufanya hivyo, tunachangia kwa kiasi kikubwa kuokoa maisha ya watu na mali zao, pamoja na kusaidia maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi ya taifa letu.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imeendelea kufanya uwekezaji mkubwa wa kimkakati katika huduma za hali ya hewa ambao ni muhimu kwa kuimarisha ustahimilivu wa taifa dhidi ya athari za mabadiliko ya hali ya hewa ikiwa ni pamoja na tahadhari dhidi ya matukio ya hali mbaya ya hewa yanayoendelea kuongezeka kwa ukubwa na idadi kutokana na mabadiliko haya. Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya hali ya hewa katika mnyororo mzima wa utoaji wa huduma hizi nchini. Miongoni mwa uwekezaji huo ni pamoja na ujenzi unaoendelea wa Jengo la Kanda ya Mashariki ambalo litatumika pia kama Kituo cha Tahadhari za Tsunami; pia ujenzi wa Kituo cha Uhakiki wa Vifaa vya Hali ya Hewa (Instrument Calibration Centre) jijini Dar es Salaam. Aidha, Serikali imeendelea kuboresha na kuongeza vifaa vya kisasa vya uangazi wa hali ya hewa ili kuimarisha usahihi wa data za hali ya hewa, ufuatiliaji mifumo na utabiri wa hali ya hewa.

Miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana katika uwekezaji katika sekta ya hali ya hewa nchini ni pamoja na uwekaji wa Rada tano (5) za hali ya hewa zilizoko Mwanza, Dar es Salaam, Mtwara, Kigoma na Mbeya kati ya Rada saba (7) zilizopangwa katika mtandao wa kitaifa wa Rada za hali ya hewa. Aidha, Serikali imenunua na kufunga vifaa mbalimbali vya kisasa vya hali ya hewa ikiwa ni pamoja na: Vifaa 10 vya hali ya hewa kwa ajili ya usafiri wa anga (Aviation Meteorological Systems (AVIMET); Vituo 50 vya hali ya hewa vinavyojiendesha vyenyewe (Automatic Weather Stations – AWS); Vipima mvua 60 vinavyojiendesha vyenyewe (Automatic rain gauges); Vituo 15 vya kisasa vya hali ya hewa kwa ajili ya huduma za hali ya hewa-kilimo (Agrometeorological AWS).

Serikali pia imewezesha ufungaji wa Kompyuta yenye uwezo mkubwa wa kuchakata taarifa (High Performance Computer – HPC) ambayo imeimarisha sana uchakataji na uchambuzi wa data za hali ya hewa na kuboresha shughuli za utabiri na uandaaji wa taarifa mahsusi za hali ya hewa kwa watumiaji na sekta mbalimbali. Vilevile, mfumo wa kisasa wa utabiri wa hali ya hewa (forecasting system) umefungwa ili kuimarisha uchakataji wa data na taarifa na kuongeza usahihi wa utabiri wa hali ya hewa hivyo kusaidia kulinda maisha ya watu na kuendeleza shughuli mbalimbali za kiuchumi.

Vilevile, TMA pia imeendelea kushikilia cheti cha ubora cha ISO 9001:2015 katika utoaji wa huduma za hali ya hewa kwa usafiri wa anga, na hivyo kuendelelea kuthibitisha ubora wa huduma mahususi za hali ya hewa kwa ajili usafiri wa anga.

Kwa upande wa ushiriki na mchango wetu kimataifa, TMA imeendelea kuiwakilisha Tanzania ipasavyo katika majukwaa mbalimbali ya kimataifa ambapo wataalamu 15 wa Tanzania wanahudumu katika vikosi kazi na kamati mbalimbali za Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) pamoja na Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa (IPCC).

Kwa mfano: Dkt. Ladislaus Chang’a, Mkurugenzi Mkuu wa TMA, alichaguliwa mwezi Julai 2023 kuwa Makamu Mwenyekiti wa IPCC kwa kipindi cha miaka saba; Dkt. Pascal Waniha, Mkurugenzi wa Miundombinu na Huduma za Ufundi wa TMA, anahudumu kama Makamu Rais wa Kamisheni ya WMO ya uangazi , miundombinu na ubadilishajaji wa data na taarifa za hali ya hewa (WMO Commission on Observation, Infrastructure, and Information Systems-INFCOM) tangu mwaka 2024; Dkt. Hamza Kabelwa, Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri, anahudumu kama Mwenyekiti Mwenza wa Kamati ya WMO inayoshughulikia mfumo jumuishi wa WMO wa uchakataji wa taarifa za hali ya hewa na utabiri (WMO Standing Committee on WMO Integrated Processing and Prediction System (SC-WIPPS)) tangu mwaka 2024. Ushiriki wa wataalamu hawa katika ngazi na vyombo hivi muhimu vya kimataifa ni kudhihirisha mchango mkubwa wa Tanzania katika kuandaa na kutekeleza kanuni na miongozo ya utoaji wa huduma za hali ya hewa duniani.

Katika juhudi za kuimarisha huduma za hali ya hewa nchini, TMA haijabaki nyumba katika matumizi ya teknolojia za kisasa ikiwemo matumizi ya Akili Mnemba (Artificial Intelligence – AI) ili kuboresha utoaji wa huduma na mifumo ya utoaji wa maamuzi katika sekta mbalimbali nyeti hususan zile zinazoathiriwa sana na hali ya hewa na kwa umma kwa ujumla. Katika kukabiliana na mabadiliko na maendeleo ya kiteknolojia, wataalamu wa TMA wamebuni mifumo ambayo ni pamoja na; Mfumo wa mawasiliano na ubadilishanaji wa taarifa na data za hali ya hewa kutoka vituo vya hali ya hewa kote nchini na kuzikusanya kwenye kituo kikuu cha utabiri kilichopo Dar es Salaam kabla ya kubadilishana nan chi nyingine duniani ujulikanao kwa jina “Digital Meteorological Observatory (DMO)”, pia mfumo wa ukusanyaji na usambazaji wa taarifa za hali ya hewa kwa watumiaji wa bahari na maziwa “Marine Meteorological Information System (MMIS)” na mfumo wa mawasiliano ya taarifa za hali ya hewa kwa sekta ya usafiri wa anga “Meteorological Aviation Information System (MAIS)” . Ubunifu huu umeimarisha uangazi, usimamizi wa data za hali ya hewa, usambazaji wa taarifa hizi na utoaji wa huduma. Juhudi hizi ni utekelezaji wa kazi zetu sambamba na dira ya TMA ya kuwa  “Kitovu bora cha huduma za hali ya hewa kwa maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii”

Katika Nyanja za Kikanda na Kimataifa, Mamlaka ya Hali ya Hewa ya Tanzania inaendelea kutoa usaidizi wa kiufundi kwa Taasisi nyingine za Hali ya Hewa za nchi nyingine hususan za barani Afrika katika maeneo muhimu ya sekta hii ya hali ya hewa, ikiwa ni pamoja na uboreshaji wa Mfumo wa Usimamizi wa Ubora (Quality Management System-QMS) na Tathmini ya Wataalamu (Competence-based Assessment) na mafunzo kuhusu mifumo ya TMA ya DMO, na MAIS. Kwa siku za karibuni, TMA imetoa usaidizi wa kiufundi kwa baadhi ya Taasisi za Hali ya Hewa za Afrika Mashariki na Kusini mwa Afrika kwa kushirikiana na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) kupitia programu zake za kikanda barani Afrika.Nchi tulizosaidia ni pamoja na; Burundi na Sudani Kusini,Namibia na Zimbabwe. Matarajio yetu ni TMA kuwa kitovu bora barani Afrika cha kukuza ujuzi na uvumbuzi katika sekta ya hali ya hewa.

Kwa kutambua pia umuhimu wa elimu kwa wataalamu wa hali ya hewa katika kuboresha huduma za tahadhari za hali ya hewa, TMA inasimamia na kuendesha Chuo cha Taifa cha Hali ya Hewa “National Meteorological Training Centre (NMTC)” kilichopo Mkoani Kigoma. Chuo cha NMTC kina ithibati ya NACTE na kina jukumu la kutoa mafunzo kwa wataalamu ikiwa ni pamoja na mafunzo ya uangazi na ufuatiliaji wa mifumo ya hali ya hewa, matumizi ya taarifa za Rada za hali ya hewa, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi kwa ngazi za cheti na stashahada. Mafunzo ya ngazi za juu, kuanzia ngazi ya Shahada ya kwanza hadi Shahada ya Uzamivu, yanapatikana kupitia ushirikiano wa TMA na taasisi za elimu ya juu za kitaifa na kimataifa ikiwa ni pamoja na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela (NM-AIST) kilichopo Jijini Arusha.

Ili kuimarisha zaidi mitandao ya uangazi wa hali ya hewa, Tanzania inaendelea kuimarisha ushirikiano na washirika mbalimbali wa maendeleo na mashirika ya kimataifa, ikiwa ni pamoja na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO). Kupitia TMA, Tanzania inaendelea na utekelezaji wa Programu ya WMO ya “Systematic Observing Financing Facility (SOFF)” yenye lengo la kuwekeza katika miundombinu ya uangazi wa hali ya hewa kwa nchi zinazoendelea. Uwekezaji huu utaimarisha ufuatiliaji na uangazi wa hali ya hewa na kuboresha uwezo wa kutoa tahadhari za mapema na hivyo kuimarisha ustahimilivu wa jamii zilizo hatarini dhidi ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.

Tunapoadhimisha Siku ya Hali ya Hewa Duniani 2026, napenda kusisitiza tena kuhusu dhamira thabiti ya TMA ya kuendelea kuimarisha mifumo ya uangazi wa hali ya hewa kwa kipindi tulichonacho ili tuweze kulinda maisha ya watu na mali zao kwa maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi kwa kesho yetu.

Nachukua fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uwekezaji mkubwa wa kuendelea kuimarisha huduma za hali ya hewa hapa nchini. Pia tunaendelea kuwashukuru Wadau mbalimbali wa Maendeleo, wa Kitaifa na Kimataifa, Vyombo vya Habari pamoja na Wafanyakazi wote wa TMA kwa juhudi zao kubwa na mchango wao katika kuendeleza huduma za hali ya hewa kitaifa, kikanda na kimataifa.

Tuendelee kushirikiana kuimarisha uangazi wa hali ya hewa leo kwa usalama wa kesho yetu. Siku ya Hali ya Hewa Duniani inatukumbusha kuwa, masuala ya hali ya hewa na maji yanatuunganisha binadamu wote. Na kuwa kila utabiri wa hali ya hewa tunaotoa, kila tahadhari inayotolewa, na kila data na taarifa ya hali ya hewa tunazokusanya na kubadilishana; vyote vina lengo moja kuu: kulinda ustawi wa maisha yetu ya sasa na baadaye.

 Pima hali ya hewa leo, ili kesho iwe salama" (Observing Today, Protecting Tomorrow)”





UJUMBE WA MHE. WAZIRI WA UCHUKUZI, PROF. MAKAME MNYAA MBARAWA (MB) KWENYE KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA HALI YA HEWA DUNIANI (WORLD METEOROLOGICAL DAY - WMD)”, 23 MACHI, 2026.


 Leo, tarehe 23 Machi 2026, nina furaha kuungana na jamii ya kimataifa katika kuadhimisha miaka 76 ya kuanzishwa kwa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO). Siku hii ni fursa ya kutambua na kupongeza mchango muhimu unaotolewa na Taasisi za Hali ya Hewa Duniani kote katika kuokoa maisha, mali, na kusaidia kuleta maendeleo endelevu ya kijamii na kiuchumi.


Kaulimbiu ya Siku ya Hali ya Hewa Dunia mwaka huu 2026 ni Pima hali ya hewa leo, ili kesho iwe salama. Kaulimbiu hii inasisitiza umuhimu wa ufuatiliaji endelevu wa mifumo ya hali ya hewa na maji na upimaji wa taarifa zake. Kwa kuimarisha mifumo hii ya ufuatiliaji na uangazi wa hali ya hewa na maji, nchi nyingi ikiwemo Tanzania, zinajizatiti zaidi kutoa taarifa za tahadhari za mapema hivyo kupunguza athari zinazohusiana na ongezeko la mabadiliko ya hali ya hewa hususan matukio ya hali mbaya ya hewa yanayoongezeka kwa ukubwa na idadi.


Sote tunafahamu umuhimu wa taarifa sahihi na za wakati za hali ya hewa katika kufanya maamuzi sahihi kwa sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi. Sekta hizi ni pamoja na uchukuzi, kilimo, nishati, maji, afya, miundombinu, ujenzi, madini, na nyingine nyingi zinazohusiana na zinazoathiriwa na hali ya hewa. Hata hivyo, mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi yanaendelea kusababisha changamoto kubwa katika sekta hizi kutokana na kuongezeka kwa idadi na ukubwa wa matukio ya hali mbaya ya hewa.

 

Kwa mujibu wa WMO, kati ya mwaka 1970 na 2021, matukio ya hali mbaya ya hewa yamesababisha hasara ya dola za Kimarekani takriban trilioni 4.3 na vifo vipatavyo milioni 2, ambapo zaidi ya 90% ya vifo hivyo vimetokea katika nchi zinazoendelea, hivyo kuonesha udharura wa kuimarisha miundombinu na mifumo ya ufuatiliaji na uangazi wa hali ya hewa ambayo itasaidia kuimarisha mifumo ya utoaji wa tahadhari za mapema kwa jamii leo na wakati ujao, sambamba na kuongeza uwezo wa wataalamu.


Uwekezaji katika miundombinu ya hali ya hewa ikiwa ni pamoja na mifumo ya utoaji wa tahadhari za mapema ni uamuzi wa kimkakati ambao Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendelea kuufanya. Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeweka juhudi za kipekee katika kuwekeza katika miundombinu na mifumo ya hali ya hewa ili kupunguza pengo katika mtandao wetu wa kitaifa wa uangazii wa hali ya hewa, kuendana na teknolojia za kisasa ikiwemo matumizi ya Akili Mnemba (AI) katika sekta utoaji wa huduma za hali ya hewa. Jitihada zote hizi zinafanywa kwa lengo la kupunguza athari za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi leo na siku zijazo kama ilivyoainishwa katika kaulimbiu ya Siku ya Hali ya Hewa ya mwaka huu. Hivyo, uwekezaji huu katika utoaji wa huduma za hali ya hewa sio mzigo kwa walipa kodi, bali ni uwekezaji katika usalama wa kitaifa, uthabiti wa kiuchumi na ustahimilivu wa muda mrefu kwa taifa letu.


Aidha, Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050 (Dira 2050) iliyozinduliwa mwezi Julai mwaka jana, inatambua mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi kama hatari kubwa kwa ukuaji wa uchumi wa muda mrefu, maisha ya watu, na usalama wa kitaifa, na inasisitiza haja ya kujenga ustahimilivu dhidi ya hali ya hewa hususan mabadiliko ya muda mrefu katika sekta zote. Kaulimbiu ya Siku ya Hali ya Hewa Duniani kwa mwaka huu inashabihiana vyema na Dira 20250 na inachangia katika utekelezaji wa nguzo tatu za Dira 2050, hasa nguzo ya tatu inayohusiana na Uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya hali ya hew ana tabianchi. Mojawapo ya malengo ya Nguzo hii ya tatu ni kujenga Taifa linaloweza kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi na linaloweza kulinda watu, miundombinu na mali zake kutokana na majanga ya asili na yale yanayotokana na binadamu, huku vijana na wanawake wakiwekwa mstari wa mbele katika hatua za kukabiliana na mabadiliko haya ya hali ya hewa na tabianchi.


Vilevile, nguzo ya tatu ya Dira inatambua kuwa, mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi, yanayoambatana na ongezeko la joto la dunia, mabadiliko ya mifumo ya hali ya hewa, na kuongezeka kwa matukio ya hali mbaya ya hewa, yanatishia maendeleo endelevu ya Tanzania. Na kuwa, athari zake ni kubwa kwa sekta zinazotegemea sana hali ya hewa, ambazo ni uti wa mgongo wa uchumi wa Tanzania. Kwa kuzingatia haya, kuna haja ya hatua za maksudi kuimarisha uangazi na uchambuzi wa taarifa za hali ya hewa ili taarifa hizi zitumike katika utoaji wa maamuzi sahihi katika sekta mbalimbali kwa jamii kujengewa uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na hivyo kuwa na maendeleo endelevu.


Chini ya uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali imeendelea kuweka kipaumbele katika kuimarisha huduma za hali ya hewa na kuboresha utoaji wa huduma hizi kwa nchi nzima. Serikali inaendelea kuhakikisha kuwa taarifa bora za hali ya hewa zinawafikia wananchi katika ngazi zote. Kama nilivyoainishwa hapo awali, uwekezaji mkubwa uliofanywa katika kuboresha miundombinu ya hali ya hewa, ikiwemo ujenzi wa Kituo cha Uhakiki wa vifaa vya hali ya hewa kinacho endelea kujengwa jijini Dar es Salaam, utaboresha uwezo wetu wa ufuatiliaji na uangazi wa hali ya hewa na hivyo kuongeza usahihi wa taarifa za hali ya hewa. Huu ni uthibitisho wa dhati wa adhma ya Tanzania kuimarisha mifumo ya uangazi na ufuatiliaji wa hali ya hewa leo ili kesho yetu iwe salama zaidi kama kaulimbiu ya siku ya hali ya hewa Dunia kwa mwaka huu inavyosema.


Kupitia ushirikiano imara na mzuri na wadau wetu wa maendeleo, ikiwa ni pamoja na Shirika la Hali ya Hewa la Dunia (WMO), Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendelea kuimarisha mtandao wake wa uangazi  na ufuatiliaji wa taarifa za hali ya hewa kupitia utekelezaji wa programu mbalimbali, ikiwemo programu ya WMO ya uwekezaji katika miundombinu ya hali ya hewa wa  “Systematic Observing Financing Facility (SOFF)” na ile ya kuboresha mpango wa utoaji wa tahadhari za mapema kwa wote yaani  “Early Warning for All (EW4ALL)”. Programu ya SOFF, inatoa mchango mkubwa kwa kuwekeza vituo tisa (9) vipya vya hali ya hewa vinavyojiendesha vyenyewe "Automatic Weather Stations (AWS); vituo vine (4) vya uangazi wa hali ya hewa ya angani za juu "Upper-Air stations", pamoja na ukarabati na uboreshaji wa vituo 18 vya AWS na kituo kimoja (1) cha uangazi wa hali ya hewa ya anga za juu. Mipango mkakati hii ya Serikali inayochagizwa na mchango wa Wadau wetu wa Maendeleo itaongeza uwezo na ufanisi wa Mamlaka yetu ya Hali ya Hewa ya Tanzania (TMA), na kuifanya iendelee kutoa huduma zilizoboreshwa na kwa wakati.


Katika kuadhimisha Siku ya Hali ya Hewa Dunia 2026, Serikali inapongeza kazi nzuri inayofanywa na Mamlaka ya Hali ya Hewa ya Tanzania (TMA) kwa kuendelea kutoa huduma za hali ya hewa zilizoboreshwa, kwa wakati na kwa umakini mkubwa. Taarifa za TMA ni muhimu sana katika kuokoa maisha, kulinda mali na kusaidia sekta kuu za uchumi wan chi yetu. Napenda pia kutoa shukrani za dhati kwa Shirika la Hali ya Hewa la Dunia (WMO) na Washirika wa Maendeleo kwa mchango wao muhimu na mkubwa katika kuimarisha huduma za hali ya hewa nchini Tanzania, hasa katika kuboresha miundombinu ya uangazi na ufuatiliaji wa hali ya hewa na kujenga uwezo wa wataalamu. Ushirikiano wenu ni muhimu sana katika kuongeza ustahimilivu wetu kama Taifa dhidi ya athari za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.


Tunapoendelea kuadhimisha siku hii muhimu, natoa rai kwa wadau wote wakiwemo Taasisi za Serikali, Washirika wa Maendeleo, Sekta Binafsi, Taasisi za Elimu, Vyombo vya Habari na Umma kwa ujumla, kuendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuwekeza kwenye mifumo na miundombinu ya uangazi na uchakataji wa taarifa za hali ya hewa nchini. Aidha, natoa wito kwa wadau wote kuendelea kutumia ipasavyo taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na TMA na kuzingatia Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya mwaka 2019.

 

Taarifa sahihi na za wakati za hali ya hewa ni nyenzo muhimu katika kufanya maamuzi ya kimkakati na kufanikisha maendeleo endelevu ya nchi yetu. Hivyo, tushirikiane kujenga Taifa lenye ustahimilivu dhidi ya athari za mabadiliko ya hali ya hewa kwa kuimarisha zaidi huduma za hali ya hewa, hususan miundombinu ya uangazi ambayo ndiyo msingi wa upatikanaji wa taarifa bora za hali ya hewa na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.

 

Tuendelee kuwekeza katika mifumo ya uangazi na ufuatiliaji wa hali ya hewa kwa wakati huu ili kulinda mustakabali wa nchi yetu pendwa na wananchi wake.

 

Nawatakia nyote maadhimisho yenye mafanikio na tija ya Siku ya Hali ya Hewa ya Mwaka 2026.

 

 Pima hali ya hewa leo, ili kesho iwe salama".”



Tuesday, March 17, 2026

MHE. KAKOSO ATOA WITO KWA WATANZANIA KUFUATILIA NA KUZINGATIA TAARIFA ZA HALI YA HEWA.

 






Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Selemani Kakoso (MB) ametoa wito kwa watanzania kufuatilia na kuzingatia taarifa za hali ya hewa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), kwa kuwa ni muhimu katika kupanga na kutekeleza mipango na shughuli katika sekta zote  za kiuchumi na kijamii hapa nchini, aliyasema hayo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu katika ofisi ya TMA, Dar es Salaam.

 

“Natoa wito kwa Watanzania kufuatilia na kuzingatia  taarifa za utabiri zinazotolewa na TMA kabla ya kuanza kutekeleza majukumu yenu katika sekta zenu ikiwemo kilimo, maji au kibiashara kwa kuwa TMA imekuwa ikitoa taarifa za uhakika kila siku kupitia vyombo mbalimbali vya habari. Kutokana na ubora na ufanisi wa huduma zao,  na weledi na umahiri wa wataalamu wake, TMA  wameaminiwa kutoa misaada ya kitaalamu kwa  baadhi ya Taasisi za hali ya hewa katika nchi mbalimbali barani Afrika.” Alisisitiza Mhe. Kakoso

 

Kupitia ziara hiyo yenye lengo la kukagua miradi inayotekelezwa na TMA, kamati ilipata fursa ya kupokea taarifa ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa Ofisi ya TMA Kanda ya Mashariki na Kituo cha Tahadhari ya Matukio ya Tsunami pamoja na Kituo cha Taifa cha Uhakiki wa vifaa vya hali ya hewa na baadaye Mamlaka ilielekezwa kuongeza jitihada za usimamizi katika kuhakikisha miradi hiyo inakamilika kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa kwa kuzingatia matakwa ya mkataba.

 

Naye Waziri wa Uchukuzi mwenye dhamana ya kusimamia sekta ya hali ya hewa Prof. Makame Mbarawa (MB) alisema Serikali ya awamu ya sita itaendelea kuwekeza kwenye sekta ya hali ya hewa na kuisimamia kwa karibu. Mh. Mbarawa aliahidi kufuatiilia kwa karibu kuhakikisha kuwa fedha zinazohitajika kwa ajili yya ukamilishaji wa miradi hiyo muhimu ya ujenzi wa miundombinu ya huduma za  hali ya hewa zinapatikana kwa wakati.

 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu, TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a aliishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kwa kuwa sababu mafanikio ya TMA yamechagizwa pia na mchango mkubwa wa kamati kutaka kuona changamoto za TMA zinatatuliwa, kupitia maelekezo mbalimbali waliyokuwa wanatoa kwa nyakati tofauti.

 

“Kupitia ziara ya mwaka 2022 Mwanza, kamati hii iliiongezea nguvu TMA katika kuhakikisha tunaimarisha miundombinu ya hali ya hewa ikiwemo ukamilishaji wa rada 5 za hali ya hewa, mitambo mbalimbali ya kiutendaji, ongezeko la rasilimali watu pamoja na kujengewa uwezo wa kiutendaji wataalam wa hali ya hewa” Alisema Dkt. Chang’a

 

Dkt. Chang’a aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuiwezesha Mamlaka katika utekelezaji wa miradi miwili ya ujenzi wa jengo la Ofisi ya TMA Kanda ya Mashariki na Kituo cha Tahadhari ya Matukio ya Tsunami, ambapo ujenzi wake umefikia asilimia 65 pamoja na ujenzi wa Kituo cha Taifa cha Uhakiki wa vifaa vya hali ya hewa ambapo ujenzi wake umefikia asilimia 40. Kukamilika kwa miradi hii miwili kutaifanya TMA kuwa katika nafasi nzuri ya kuwa kitovu cha kuhakiki vifaa vya hali ya hewa hadi Ukanda wa Afrika.

Sunday, March 8, 2026

IWD 2026: TMA na masuala ya jinsia katika utoaji wa tahadhari za hali ya hewa


 

WANAWAKE WA TMA WAADHIMISHA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI 2026, KWA KUFANYA SHUGHULI ZA KIJAMII.

 WANAWAKE WA TMA WAADHIMISHA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI 2026, KWA KUFANYA SHUGHULI ZA KIJAMII.







Wanawake wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) wameadhimisha Siku ya Wanawake Duniani katika mikoa mbalimbali nchini Tanzania kwa kufanya shughuli tofauti za kijamii zinazolenga kuimarisha mshikamano na kusaidia jamii.


Maadhimisho hayo yalifanyika kwa kuzingatia kaulimbiu ya mwaka huu isemayo: “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana; Msingi Jumuishi kufikia Dira ya Maendeleo 2050.”


Katika Mkoa wa Dodoma, watumishi wanawake wa TMA walipata fursa ya kutembelea Kituo cha Watoto Yatima cha Safina  kilichopo Ntyuka, ambapo walikutana na watoto wanaolelewa katika kituo hicho na kuwapa faraja pamoja na kuwasaidia kwa mahitaji mbalimbali.


Ziara hiyo ililenga kuonesha upendo, mshikamano na kuwapa matumaini watoto wasiokuwa na wazazi au wale wanaoishi katika mazingira magumu.

Sunday, March 1, 2026

DKT CHANG’A AFANYA MAZUNGUMZO NA KATIBU MKUU WA SHIRIKA LA HALI YA HEWA DUNIANI (WMO)

DKT CHANG’A AFANYA MAZUNGUMZO NA KATIBU MKUU WA SHIRIKA LA HALI YA HEWA DUNIANI (WMO)

 

 Geneva, 27 Februari 2026

Katibu Mkuu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (World Meteorological Organization - WMO) Prof. Celeste Saulo ameahidi kuendelea kushirikiana na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) katika kuboresha huduma za hali ya hewa kwa matumizi katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii.

Ameyasema hayo wakati wa kikao cha pembezoni mwa kikao cha 70 cha Kamati Kuu Tendaji ya Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (Seventieth Session of the Intergovernmental Panel on Climate Change-IPCC (70th IPCC Bureau), alipokutana na  Dkt. Ladislaus Chang’a, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya hali ya Hewa Tanzania (TMA), ambaye pia ni Mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika WMO na Makamu wa Mwenyekiti wa Jopo la IPCC kwa lengo la kujadiliana kuhusu maendeleo ya utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini Tanzania na mipango ya kuendeleza ushirikiano na WMO tarehe 27 Februari 2026 Jijini Geneva, Uswisi.

Prof. Celeste Saulo amempongeza Dkt. Chang’a na kufurahishwa na namna TMA wanavyoendelea kusimamia vyema utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini Tanzania. Aidha, Prof. Celeste Saulo ameahidi kuendelea kushirikiana na Tanzania katika kuboresha huduma za hali ya hewa kupitia programu mbalimbali za WMO ikiwa ni pamoja na eneo la matumizi ya akili mnemba (AI) katika mnyororo mzima wa utoaji wa huduma za hali ya hewa. 

“Nimefurahishwa na maendeleo ya utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini kwenu. Sisi kama WMO tuko tayari kuendelea kushirikiana ili kuboresha zaidi huduma huduma za hali ya hewa nchini Tanzania ikiwa ni pamoja na kuwaunganisha na taasisi nyingine zilizopiga hatua zaidi ili kubadilishana ujuzi zaidi” Alisema Prof. Celeste Saulo.

Katika Kikao hicho, Dkt. Ladislaus Chang’a amemshukuru Katibu Mkuu wa WMO kwa usaidizi kwa TMA kupitia programu zake mbalimbali za uboreshaji wa huduma za hali ya hewa kikanda na kitaifa zikiwemo za “Climate Risk and Early Warning Systems (CREWS-EA), “Systematic Observations Financing Facility (SOFF)” na “Weather and Climate Information Services for Africa (WISER)” ambazo zinatekelezwa kwa ushirikiano na Wadau wa Maendeleo na Nchi Wanachama wa WMO ambapo utekelezaji wake unaendelea vizuri. 

“Nashukuru sana kwa usaidizi wa WMO kupitia programu zake mbalimbali zikiwemo za CREWS, SOFF na WISER ambazo zinachangia pakubwa katika kuboresha utoaji wa huduma za hali ya hewa nchini na kuongeza nguvu katika uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hususan katika uboreshaji wa miundombinu ya hali ya hewa nchini na kuwajengea uwezo wataalamu. Programu hizi sio tu zimechagiza katika uboreshaji wa huduma za hali ya hewa bali zinawajengea uwezo wataalamu wa TMA wa kusaidia nchi nyingine kuboresha huduma zao za hali ya hewa” Alisema Dkt. Chang’a.

Dkt. Chang’a alimjulisha Katibu Mkuu wa WMO kuwa, Taasisi za Hali ya Hewa za Nchi wanachama wa WMO ambazo wataalamu wa TMA wametoa msaada wa kiufundi Barani Afrika hivi karibuni ni pamoja na Burundi, Sudan Kusini na Zimbabwe ambapo nchi nyingine ikiwa ni pamoja na Zambia, Sierra Leone na Uganda wataalamu wanaendelea na majadiliano ya namna wanavyoweza kusaidiwa na TMA katika maeneo ambayo TMA tumepiga hatua zaidi. Maeneo ambayo TMA imezisaidia nchi nyingine katika tasnia hii ya hali ya hewa ni pamoja na uboreshaji wa “Mfumo wa Usimamizi wa Ubora wa huduma (Quality Management System-QMS and Competency Assessment )”, “Utabiri wa Hali Mbaya ya Hewa (Severe Weather Forecasting)”, “Utabiri wa Hali ya Hewa kwa Kutumia Modeli za Kompyuta (Numerical Weather Prediction-NWP)”, “Mchakato wa kisheria katika sekta ya hali ya hewa (Legal Matters)” na Usambazaji wa Huduma za Hali ya Hewa kwa Umma (Public Weather Services-PWS). 

Katika kuhitimisha mazungumzo yao, Dkt. Chang’a alimshukuru Katibu Mkuu wa WMO kwa fursa ya kuleta mikutano mikubwa ya kitaalamu nchini ikiwa ni pamoja na mkutano wa nne (4) wa Wataalamu bingwa wa utabiri wa hali ya hewa Duniani utakaojadili maendeleo ya utabiri wa hali ya hewa kwa kuzingatia ukuaji wa teknolojia na matumizi ya huduma hizi kwa sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi “The Fourth WMO Operational Climate Prediction (OCP-4)” unaotarajiwa kufanyika Arusha mwishoni mwa mwezi Juni hadi mwanzo wa Julai 2026 kwa mara ya kwanza barani Afrika na kwa Tanzania.

IMETOLEWA NA:
KITENGO CHA UHUSIANO
MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA (TMA)

Tuesday, February 24, 2026

TMA, UDSM ZAIMARISHA MAHUSIANO YA KITAALAM NA KITAALUMA


 TMA, UDSM ZAIMARISHA MAHUSIANO YA KITAALAM NA KITAALUMA


 Dodoma, Februari 18, 2025.


Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) wamejadiliana namna ya kuimarisha ushirikiano wa kitaalam na kitaaluma kwa lengo la kuimarisha taaluma na sayansi ya hali ya hewa ili kuchangia katika kuboresha huduma za hali ya hewa nchini.


Majadiliano hayo yamefanyika katika kikao maalum kilicholenga kuangalia maeneo ya ushirikiano uliopo na namna ya kuuboresha, hususan katika matumizi ya tafiti zinazofanywa na UDSM kuhusiana na masuala ya hali ya hewa na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.


Akifungua kikao hicho, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang’a, alieleza kuwa ushirikiano kati ya taasisi hizo umedumu kwa muda mrefu na kikao hicho kimeweka mkazo katika kuimarisha maeneo mahsusi ya ushirikiano huo, ikiwemo kuimarisha uelewa na matumizi ya akili mnemba (AI) katika utafiti na huduma za hali ya hewa.


Akiongea wakati wa uwasilishaji wake Dkt. Paul T. S. Limbu Mhadhiri Mwandamizi wa Meteorolojia na Sayansi ya Hali ya hewa katika Idara ya Fizikia, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) amesema kwa zaidi ya miaka 13 ya kufundisha masomo ya hali ya hewa, bado kuna haja ya kuendelea  kuimarisha zaidi ushirikiano kati ya  UDSM na TMA. 


Tunawashukuru sana TMA kwa kushiriki na kutusaidia  katika mchakato wa kuboresha mitaala, ufundishaji na usimamizi wa tafiti.


Pia ameeleza umuhimu wa wanafunzi kupata elimu kwa vitendo kupitia ziara za kitaaluma katika miundombinu ya TMA, fursa za kujitolea baada ya kuhitimu, pamoja na ushiriki wa TMA katika uandaaji wa vitabu vya kufundishia .


Aidha, pande hizo zimejadili ushiriki wa UDSM katika warsha, semina na maadhimisho ya siku muhimu kama Siku ya Hali ya Hewa Duniani ili kuwajengea wanafunzi uzoefu wa moja kwa moja katika mazingira halisi ya kazi.


Kwa ujumla, kikao hicho kimeweka msingi wa kuendeleza mazungumzo ya kitaalam yatakayosaidia kuunganisha tafiti, elimu na utekelezaji katika kuboresha huduma za hali ya hewa nchini.

Thursday, February 12, 2026

SERIKALI YATENGA BILIONI 13 KUWEZESHA UJENZI WA OFISI ZA TMA.

 









SERIKALI YATENGA BILIONI 13 KUWEZESHA UJENZI WA OFISI ZA TMA.


Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi, Mhe. David Kihenzile, ametembelea ujenzi wa ofisi za Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) zilizopo Sinza Simu 2000, jijini Dar es Salaam. Ujenzi huu, unaofadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, unalenga kuongeza ufanisi wa utoaji wa taarifa sahihi za hali ya hewa.


Akizungumza katika ziara hiyo,Naibu Waziri wa Uchukuzi,Mhe.David Kihenzile amesema Serikali ya Awamu ya Sita imetenga takribani shilingi bilioni 13 kwa ajili ya ujenzi wa  ofisi za TMA. Miradi hiyo inahusisha ujenzi wa jengo la kisasa la Kanda ya Mashariki na Utoaji Tahadhari za Hali ya Hewa pamoja na kituo cha tahadhari za Tsunami nchini,pamoja na Kituo cha Taifa cha Uhakiki wa Vifaa vya Hali ya Hewa (National Meteorological Calibration Centre) kitakachosaidia kukagua na kuboresha vifaa vya hali ya hewa.


Mhe. Kihenzile amesema majengo yote mawili, yaliyoanza kujengwa mwaka 2023 na 2025, yanatarajiwa kukamilika kabla ya mwisho wa mwaka huu. Ameeleza kuwa miradi hiyo itaongeza ufanisi katika utoaji wa taarifa za hali ya hewa na kuwawezesha wataalamu kufanya kazi katika mazingira bora na ya kisasa.


Kwa niaba ya Waziri wa Uchukuzi,Mhe.David Kihenzile (MB), ametoa rai kwa Bodi na Menejimenti ya TMA kusimamia miradi hiyo kwa weledi, uzalendo na kuhakikisha inakamilika kwa wakati na kwa ubora uliokusudiwa.Aidha aliipongeza TMA kwa kumchagua mkandarasi wa ndani, Chuo cha DIT (Taasisi ya Teknolojia ya Dar es Salaam), kutekeleza miradi hiyo akieleza kuwa hatua hiyo inachochea maendeleo ya wataalamu na taasisi za ndani.


Pia,Naibu Waziri amewahimiza TMA kutoa taarifa kwa wakati ili kuwasaidia wananchi katika shughuli za kila siku zikiwemo usafiri, kilimo na matumizi ya bahari na amewahimiza wananchi kuendelea kuamini na kutumia taarifa rasmi za hali ya hewa kutoka TMA.

Thursday, February 5, 2026

TMA YATOA UTABIRI WA MSIMU WA MVUA ZA MASIKA 2026 KWA MAENEO YANAYOPATA MVUA MARA MBILI KWA MWAKA.

 


Dar es Salaam, Tarehe 05/02/2026;


Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi utabiri wa msimu wa mvua za Masika 2026 kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka. Akizungumza wakati wa mkutano na vyombo mbalimbali vya habari katika ukumbi wa Ubungo Plaza, tarehe 05/02/2026, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi Dkt. Ladislaus Chan’ga alisema maeneo mengi ya nchi yanayopata misimu miwili ya mvua yanatarajiwa kupata mvua za wastani hadi juu ya wastani.

 

 “Mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya nchi ikihusisha Pwani ya Kaskazini pamoja na baadhi ya maeneo ya Magharibi mwa ukanda wa Ziwa Viktoria (mikoa ya Kagera na Geita) pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma, isipokuwa maeneo ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki na baadhi ya maeneo ya ukanda wa Ziwa Viktoria (mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Mara na Simiyu) mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani zinatarajiwa”. Alisema Dkt. Chang’a.

 

Katika taarifa hiyo ilielezea kuwa Mvua za Masika zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya mwezi Februari na ya kwanza ya mwezi Machi , 2026 katika maeneo ya kanda ya Ziwa Victoria; na wiki ya kwanza na ya pili ya mwezi Machi katika maeneo ya pwani ya kaskazini; na wiki ya pili na ya tatu ya mwezi Machi,  2026 katika maeneo ya nyanda za juu kaskazini mashariki, Mvua hizo zikitarajiwa kuisha wiki ya nne ya mwezi Mei na wiki ya kwanza ya mwezi Juni 2026 katika maeneo mengi yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka huku ongezeko la mvua likitarajiwa katika kipindi cha mwezi Aprili 2026.


Akizungumzia athari zinazoweza kujitokeza, Dkt. Chang’a alisema vipindi vya unyevu wa kuzidi kiasi pamoja na mafuriko vinaweza kujitokeza na kuathiri ukuaji wa mazao katika baadhi ya maeneo, hususan yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani. Kina cha maji katika mito, mabwawa na hifadhi ya maji ardhini kinatarajiwa kupungua hususan katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani. Magonjwa ya mlipuko yanaweza kujitokeza kutokana na uchafuzi wa maji, hivyo kushauri watumiaji wa tarifa hizo kuzingatia ushauri wa wataalamu katika sekta zao.


Angalizo la matukio ya hali mbaya ya hewa ikiwemo vipindi vya mvua kubwa lilitolewa hata katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani huku watumiaji wa taarifa hiyo wakishauriwa kufuatilia taarifa za utabiri wa saa 24, siku 10, mwezi na tahadhari kama zinavyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).

 

Kwa taarifa zaidi tembelea; https://www.meteo.go.tz/uploads/documents/sw-1770290524-Taarifa%20ya%20Mwelekeo%20wa%20Mvua%20za%20Masika%202026.pdf



Tuesday, February 3, 2026

WADAU SEKTA YA HALI YA HEWA WAJADILI UTABIRI WA MASIKA 2026.

Dodoma, tarehe 2 Februari 2026:

Wadau kutoka sekta mbalimbali nchini wamekutana kujadili utabiri wa msimu wa Masika 2026 na kutoa ushauri wa kisekta katika Mkutano wa 25   wa Wadau wa Sekta ya Hali ya Hewa katika msimu wa Masika uliofanyika tarehe 2/2/2026, Jijini Dodoma. Mkutano huo ni mwendelezo wa ushirikishwaji wa wadau katika utoaji wa taarifa za hali ya hewa kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini. 

Mgeni Rasmi kwenye mkutano huo, Mh. Jaji  Mshibe Ali Bakari ambaye ni Mwenyekiti wa Bodi ya TMA  alisema





























“msimu wa Vuli mwaka 2025 ulitawaliwa  na vipindi virefu vya ukavu katika maeneo mengi ya nchi, usahihi wa utabiri ulikuwa kwa asilimia 94.1, ikiwa ni kiwango kikubwa sana, natoa wito kwa wananchi waendelee kuiamini TMA, wazingatie taarifa zinazotolewa na kuzitumia katika shughuli zao za kila siku".  

Aidha, alisisitiza kuwa majadiliano ya mvua za Masika kwa mwaka 2026, yazingatie kwa kina athari zinazoweza kujitokeza pamoja na kutoa ushauri wa hatua stahiki za kuchukua kwa ajili ya matumizi ya taarifa hizo katika sekta mbalimbali zinazochangia ukuaji wa uchumi.

Awali, akimkaribisha Mgeni Rasmi, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Changa, alisema "katika kupunguza pengo la uelewa wa tahadhari za hali ya hewa, Mamlaka imeendelea na juhudi za kushirikisha wadau, katika kuandaa taarifa zinazolenga kuchochea matumizi sahihi ya huduma za hali ya hewa nchini"

Dkt. Changa aliongeza kuwa TMA imeendelea kufanya shughuli zake kwa ubora unaoendana na viwango vya kitaifa na kimataifa na kuifanya Tanzania kuwa moja ya  nchi zinazoaminika kwa utoaji wa huduma bora za hali ya hewa duniani. Kupitia viwango hivyo,Tanzania imechaguliwa kuandaa  Mkutano wa Nne wa Kimataifa wa Watalaam Bingwa wa Hali ya Hewa Duniani, mwezi Juni 2026.

Kwa upande wa wadau, walitoa pongezi na shukrani kwa TMA kwa ushirikiano wanaoendelea kupata katika kuwasilisha taarifa za hali ya hewa kwa jamii. "Naipongeza TMA kwa kuandaa mkutano huu wa wadau wa hali ya hewa.Sisi ili tuweze kufanya kazi zetu ni lazima tupate taarifa zinazotusaidia katika mipango yetu ya kazi ili kulinda usalama wa wananchi na mali zao".Alisema Kaimu Mkurugenzi  wa Kamisheni Ya Maafa, Ofisi ya Makamu wa Rais wa Pili wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Ndg. Muhidin Ali Muhidin 

Mamlaka inatarajia kutoa utabiri wa msimu wa Masika 2026, tarehe 5/2/2026.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...