Morogoro, tarehe 07 Agosti 2025
Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Bi. Pili Mnyema amewakumbusha viongozi mbalimbali nchini kuendelea na jitihada za kuhamasisha wananchi kutumia taarifa za hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na wananchi kupitia vyombo vya habari katika Maonesho ya Nane Nane 2025 yanayoendelea kwenye viwanja vya Nane Nane, Morogoro.
“Kama viongozi tunajukumu la kuwaelimisha na kuwahamasisha wananchi wetu ikiwemo wakulima, wafugaji na wavuvi ili watumie utabiri wa hali ya hewa unaotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, itawasaidia wananchi kujikinga na athari zinazoweza kujitokeza kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa yaliyopo”. Alisisitiza Bi. Pili Mnyema
Kwa upande wa Meneja wa Kanda ya Mashariki-TMA, Bi. Hidaya Senga ameelezea njia mbalimbali zinazotumiwa na TMA katika usambazaji wa taarifa zake kama vile vyombo vya habari, tovuti, mitandao ya kijamii pamoja ushirikiano mkubwa na Taasis za kisekta ambao umesaidia kufikia wadau wengi wa sekta mbalimbali.
Bi. Hidaya ameongezea kwa kuwashauri wanafunzi kutembelea banda la TMA lililopo katika maonesho hayo ya Nane Nane ili kujifunza teknolojia mpya inayotumika TMA kwa kuona mtambo wa kisasa unaojiendesha wenyewe (Automatic Weather Station) kwa uhalisia zaidi.
No comments:
Post a Comment