Monday, October 24, 2022

DKT. NYENZI: TAARIFA ZA HALI YA HEWA NI CHACHU YA KUJENGA UCHUMI WA VIWANDA.

 














Dar es Salaam; Tarehe 24 Oktoba, 2022;

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imekutana na wadau kutoka sekta mbalimbali ili kujadili utabiri wa mvua za msimu unaotarajiwa kuanza mwezi Novemba 2022 hadi Aprili 2023 kwa maeneo yanayopata msimu mmoja wa mvua kwa mwaka ambayo ni Tabora, KigomaKusini,Katavi,Mbeya,Rukwa,Songwe,Njombe,Iringa,Ruvuma,Mtwara,Lindi,Dodoma, singida na Morogoro Kusini . Katika ufunguzi wa kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Tiffany Diamond Hotels uliopo jijini Dar es Salam, Tarehe 24 Oktoba 2022, mgeni rasmi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya TMA, Dkt. Buruhani Nyenzi amehimiza wadau kuendelea kufuatilia taarifa za hali ya hewa ambazo ni chachu katika kujenga uchumi wa viwanda hapa nchini.

“Taarifa za hali ya hewa zinalenga katika kusaidia nchi kufikia malengo ya mpango wa Taifa katika kujenga uchumi wa viwanda kwa kusaidia kupunguza athari zitokanazo na majanga yanayosababishwa na hali mbaya ya hewa ili kusaidia kulinda mafanikio ya uwekezaji katika miundo mbinu ya uchukuzi ikiwemo barabara, reli na vyombo vya usafiri majini”. Alisema Dkt.Nyenzi

Dkt. Nyenzi aliongezea kwa kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan  kwa kuendelea kuijengea uwezo TMA, hatua ambayo imeisaidia kuboresha utabiri wa hali ya hewa na kusaidia Taifa katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa ikiwemo upungufu wa mvua, mafuriko, joto na baridi kali  pale zitakapojitokeza.

Kwa upande wa Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) Dkt. Agnes Kijazi ameelezea namna serikali ilivyoendelea kuijengea uwezo Mamlaka kwa kuboresha miundo mbinu yake ambayo kwa njia moja au nyingine inasaidia kukuza uchumi wa nchi.

Dkt. Kijazi amesema mtandao wa rada upo katika hatua za mwisho ili kukamilika, huku vituo vya hali ya hewa vinavyojiendesha vyenyewe vikizidi kuongezwa na mbiundombinu ya uchambuzi wa taarifa za hali ya hewa ikiendelea kuboreshwa, Aidha mitambo ya mawasiliano imeendelea kuboreshwa ili taarifa hizi ziweze kuwafikia wadau kwa wakati, na pia wataalam wameendelea kujengewa uwezo kupitia mafunzo mbalimbali na hivyo kuwapa uwezo wa kufungasha taarifa zilizoboreshwa.

Aidha, Dkt. Kijazi aliwashukuru ILRI kutoka  Nairobi ambao wamefadhili kwa sehemu kikao hicho cha wadau.

Aidha, wadau mbalimbali wa hali ya hewa walielezea namna wanavyozitumia taarifa za hali ya hewa katika kujiandaa na kukabiliana na hali ya hewa tarajiwa katika sekta zao, ambapo mdau kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi ndugu Emmanuel Kato (Afisa Malisho), alielezea namna sekta hiyo inavyojiandaa katika kukabiliana na hali ya hewa tarajiwa na maandalizi hayo ni pamoja na kuchimba visima virefu vya maji na ujenzi wa mabwawa katika kupunguza au kuepusha migogoro ya wafugaji katika kutafuta maji kwaajili  ya  mifugo pale upungufu wa mvua unapojitokeza.

Kwa upande wa mdau wa kilimo Juma Makandi, alisema kupitia taarifa za TMA timu ya wataalam imeweza kutembelea maeneo yenye dalili za upungufu wa chakula na kwa sasa inaendelea na tathmini na ripoti itatolewa baada ya kazi kukamilika, naye, mdau wa kutoka TANESCO James Kirahuka alisema umuhimu wa taarifa za hali ya hewa katika uzalishaji wa nishati ya umeme nchini ni pamoja na kusaidia katika kutoa tahadhari za hali mbaya ya hewa ambayo inaweza kusababisha uharibifu wa miundombinu ya umeme kama vile kuanguka kwa nguzo za umeme.


No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...