Friday, June 3, 2022

TAARIFA POTOFU INAYOSAMBAA KATIKA MITANDAO YA KIJAMII KUHUSU HALI YA BARIDI HAPA NCHINI


 

Dar es Salaam, Tarehe 03 Juni 2022:

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inapenda kutoa ufafanuzi wa taarifa potofu kuhusu hali ya baridi inayoendelea nchini. Taarifa hiyo imesambaa kwenye mitandao ya kijamii ikieleza, “kuanzia kesho hadi Agosti 22 mwaka huu kutakuwa na baridi zaidi kuliko miaka ya nyuma”. Taarifa hiyo potofu imehusisha Aphelion. Tukio la Aphelion ni hali ya kawaida katika mzunguko wa dunia kwenye mfumo wa jua (solar system). Hata hivyo, mchango wake katika mwenendo wa hali ya baridi kati ya msimu mmoja na mwingine ni mdogo katika maeneo yetu kutokana na kuwa karibu na Ikweta.

Kipindi cha miezi ya Juni hadi Agosti kila mwaka, ni majira ya Kipupwe katika maeneo mengi hapa nchini ambapo mifumo ya hali ya hewa hutawaliwa na hali ya baridi na upepo mkali. Utabiri wa msimu wa Kipupwe uliotolewa na TMA tarehe 1 Juni 2022 unaonesha kuwa hali ya baridi ya wastani hadi joto kiasi inatarajiwa katika maeneo mengi ya nchi. Viwango vya joto la chini vinatarajiwa kuwa kati ya nyuzi joto 140C hadi 260C kwa maeneo ya ukanda wa pwani, kati ya nyuzi joto 40C hadi 140C kwa maeneo ya nyanda za juu kusini-magharibi na kati ya nyuzi joto kati ya 100C hadi 200C kwa maeneo mengine ya nchi. Aidha, TMA imetoa tahadhari ya uwepo wa vipindi vya upepo mkali na mawimbi makubwa. Tahadhari hiyo ni kwa baadhi ya maeneo ya ukanda wa pwani ya Bahari ya Hindi kuanzia Alhamisi tarehe 2 na inatarajiwa kudumu hadi tarehe 6 Juni 2022 na ambayo itakuwa ikihuishwa kila inapobidi.

TMA inapenda kuwakumbusha kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa, Tanzania Na. 2 ya Mwaka 2019, TMA ndio taasisi pekee yenye jukumu la kutoa taarifa za utabiri na tahadhari za hali ya hewa kwa Umma na kuwa ni kosa kisheria kusambaza taarifa kutoka katika vyanzo visivyo rasmi kwa mujibu wa kifungu cha 27 na 31(5) cha Sheria hiyo.

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...