Friday, January 31, 2025

TAASISI YA UONGOZI YAINOA BODI YA MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA (TMA)




















Dar es Salaam, Tarehe 30/01/2025

Katika kuboresha ufanisi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA),Taasisi ya Uongozi imetoa mafunzo ya siku mbili kwa Bodi ya TMA.Mafunzo hayo yalifunguliwa rasmi na Mwenyekiti wa Bodi Mh.Jaji Mshibe Ali Bakari katika ukumbi wa mikutano wa PSSSF Jengo la Millenium II,Jijini,Dar es Salaaam tarehe 29 hadi 30 Januari 2025.

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo, Mh, Jaji.Mshibe alisema “Jambo muhimu katika mafunzo haya ni kuimarisha ushirikiano na uwazi ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi kwenye Taasisi yetu’’

Katika hatua nyingine,Bodi hiyo ilifanya ziara ya kutembelea mradi wa ofisi ya Kanda ya Mashariki na kituo cha Tahadhari ya Matukio ya Tsunami,ambapo Katibu wa Bodi na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi,Dkt.Ladislaus Chang’a aliishukuru Bodi, kwa kutembelea eneo la mradi na kwa maelekezo na miongozo ya kuhakikisha kuwa mradi unafanyika kwa ufanisi.

Mafunzo hayo yamejumuisha Bodi na Menejimenti ya TMA ambapo mada mbalimbali zilitolewa ikiwemo uongozi bora,uongozi wa kimkakati na vihatarishi vinavyoweza kukwamisha ufanisi wa Taasisi.

Thursday, January 23, 2025

TMA YATOA UTABIRI WA MSIMU WA MVUA ZA MASIKA 2025 KWA MAENEO YANAYOPATA MVUA MARA MBILI KWA MWAKA.



 Dar es Salaam; Tarehe 23 Januari 2025;

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi Utabiri wa Msimu wa Mvua za Masika 2025 kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka. Akizungumza wakati wa mkutano na vyombo vya habari katika ukumbi wa mikutano wa Ubungo Plaza, Tarehe 23 Januari 2025, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Mwakilishi wa Kudumu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Changa alisema mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki pamoja na Mashariki mwa mikoa ya Mara na Simiyu huku mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani zikitarajiwa katika maeneo ya Pwani ya Kaskazini, Kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma na Ukanda wa Ziwa Victoria.

“Mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki pamoja na Mashariki mwa Mikoa ya Mara na Simiyu. Aidha, mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo ya Pwani ya Kaskazini, Kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma na Ukanda wa Ziwa Victoria (Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga na magharibi mwa mikoa ya Simiyu na Mara) katika kipindi cha Msimu wa Masika, 2025. Alisema Dkt. Chang’a

Vilevile, taarifa hiyo imeelezea pia ongezeko la mvua linatarajiwa katika kipindi cha mwezi Aprili sambamba na kutoa angalizo la matukio ya hali mbaya ya hewa ikiwemo vipindi vya mvua kubwa kujitokeza hata katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani.

Akizungumzia athari zinazoweza kujitokeza, Dkt. Chang’a alisema Mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani zinazotarajiwa katika baadhi ya maeneo zinaweza kupelekea upungufu wa upatikanaji wa maji kwa matumizi ya majumbani, kilimo na ufugaji.

Ili kupata taarifa zaidi za utabiri huu, tembelea: https://www.meteo.go.tz/uploads/publications/sw1735801516-Mwelekeo%20wa%20Hali%20ya%20Hewa%20Januari,%202025.pdf


Wednesday, January 22, 2025

WANAHABARI WAKUMBUSHWA KUWASILISHA KAZI ZAO ZA USHINDANI WA TUZO ZA WANAHABARI BORA WA HABARI ZA HALI YA HEWA













Dar es Salaam; Tarehe 22, Januari 2025 

“TMA inaendelea kuweka mikakati ya kuhakikisha warsha za wanahabari zinaendelea kuwa endelevu na kuboreshwa zaidi, Hatua za uboreshwaji ni pamoja na uanzishwaji wa Tuzo za Wanahabari bora wa habari za hali ya hewa kila mwaka, hivyo ninawakumbusha wanahabari wote nchini, kuwasilisha kazi zenu za ushindani kupitia barua pepe elekezi ili muda wa mchakato ukifika wapatikane washindi waliokidhi vigezo.” 

Hayo yalizungumzwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Mwakilishi wa Kudumu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a alipokuwa akifungua rasmi mkutano wa wanahabari katika kujadili Utabiri wa Mvua za Msimu wa MASIKA unaoanzia mwezi Machi hadi Mei 2025. 

Aidha, Dkt. Chang’a aligusia kuhusu changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa kwa kuwa mwaka 2024 ulivunja rekodi kwa kuwa mwaka wenye ongezeko kubwa zaidi la joto Duniani kwa ongezeko la takribani nyuzi joto 1.550C na upande wa Tanzania ongezeko la joto lilifikia nyuzi joto 0.70C, hivyo kuashiria uhitaji wa jitihada kubwa za pamoja za jumuiya ya kimataifa za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa. Aliwahamasisha wanahabari kujipanga vizuri ili kuendelea kuelimisha jamii. 

Kwa upande wa mwakilishi wa wanahabari kutoka Daily News Digital Bi. Zaituni Mkwama alitoa mrejesho wa namna walivyosambaza Utabiri wa mvua za Vuli 2024 uliotolewa na TMA kwa kuonesha kuwa mvua hazitakuwa za kutosha, hali iliyosaidia Serikali kuweka miundombinu mizuri na kuhakikisha chakula kinapatikana cha kutosha hapa nchini. 

“Baada ya wanahabari kusambaza Utabiri wa Mvua za VULI 2024 uliotolewa na TMA ilipelekea Serikali kuweka miundombinu rafiki kwa kuhakikisha chakula kinapatikana kwa kuitosheleza nchi.”. Alisema Bi. Zaituni Mkwama. 

Katika mkutano huu, wanahabari walipata fursa ya kuona utabiri wa hali ya hewa katika kipindi cha mwezi Machi hadi Mei, 2025 na kutoa michango yao juu ya namna bora na sahihi zaidi ya usambazaji wake.

UZINDUZI WA MRADI WA MFUKO WA UMOJA WA MATAIFA WA KUIMARISHA UANGAZI WA HALI YA HEWA


 














Dodoma, Tarehe 21/01/2025, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa (Mb) amezindua rasmi awamu ya utekelezaji wa mradi wa Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Kuimarisha Uangazi wa Hali ya Hewa (SOFF) kupitia hafla iliyofanyika mjini Dodoma.

Mpango huu mkubwa unaofanywa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) na Taasisi ya Hali ya Hewa ya Denmark (DMI), unalenga kuimarisha uwezo wa Tanzania wa kufanya uangazi wa hali ya hewa, ubadilishanaji wa data za hali ya hewa na katika kukabiliana na changamoto zinazotokana na mabadiliko ya hali ya hewa.

 

Katika hotuba yake, Waziri Mkuu alisema “uzinduzi wa awamu ya utekelezaji wa mradi wa Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Kuimarisha Uangalizi wa Hali ya Hewa (SOFF) ni hatua muhimu kwa Tanzania na jumuiya za kimataifa.” Aliendelea kusema, “Utaongeza uwezo wa Tanzania katika kukusanya na kusambaza data za hali ya hewa, mpango huu utasaidia kujiandaa katika kukabiliana na maafa yatokanayo na mabadiliko ya hali ya hewa, na kuzisaidia sekta muhimu kama vile kilimo, nishati na usafirishaji katika kufanya maamuzi sahihi. Aliongeza kuwa mradi wa SOFF unaendana na mikakati ya Serikali ya kuleta maendeleo kwa ustawi na uendelevu wa Taifa.

Naibu Waziri wa Uchukuzi, David Kihenzile (MB), alisisitiza kuwa "SOFF sio tu inawekeza katika teknolojia 
ya kisasa bali ni kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi sababu data sahihi za hali ya hewa 
huokoa na kulinda maisha na kuleta maendeleo endelevu." Naibu Waziri ameeleza kuwa Wizara ya 
Uchukuzi ambayo inasimamia sekta ya hali ya hewa nchini Tanzania inatambua kuwa mafanikio ya 
mpango wa SOFF yanategemewa kuwa endelevu na kuleta manufaa ya muda mrefu.

 

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Mwakilishi wa Kudumu wa 
Shirika la Hali ya Duniani (WMO) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko 
ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dk.Ladislaus Chang'a alisisitiza namna mradi wa SOFF unavyosaidia 
katika kukabiliana na mapungufu yaliyobainika katika miundombinu ya hali ya hewa nchini Tanzania ili 
kukidhi viwango vya Kimataifa vya Mtandao wa Kimataifa wa Uangazi wa Msingi (GBON). Utafiti wa 
mapungufu hayo ulifanyika  mwaka 2023, "ulionyesha kuwa Tanzania inahitaji angalau vituo 27 vya 
uangazi usawa wa ardhi kwa eneo la kilomita 200 kwa kilomita 200, na vituo vitano (5) vya uangazi 
angani kwa eneo la  kilomita 500 kwa kilomita 500."

 

Naye Mwakilishi Mkazi wa UNDP, Shigeki Komatsubara, aliipongeza Serikali kwa hatua inayochukua 
katika kufanya mipango ya kukabiliana na maafa, akisema kuwa “SOFF itakuwa ni nyenzo muhimu ya 
kuwezesha mifumo ya utoaji wa tahadhali za mapema, kusaidia kufanya mifumo hii kuwa ya uhalisia 
kwa jamii zilizo hatarini ulimwengu.” Alisema hayo akienda sawa na mpango wa Katibu Mkuu wa Umoja 
wa Mataifa wa Tahadhali za Mapema kwa Wote, unaolenga kuhakikisha, ifikapo mwaka 2027, kila mtu 
Duniani analindwa na mifumo madhubuti ya tahadhari za mapema.

 

Jumla ya bajeti iliyotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya uwekezaji wa mradi wa SOFF nchini 
Tanzania ni dola milioni 13.9, ambapo dola milioni 9 zinatolewa na Mfuko wa Mashirika ya Wadau wa 
Hisani (Multi-Partner Trust Fund (MPTF)) huku sehemu iliyobaki ikifadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya 
Muungano wa Tanzania. Mradi wa SOFF ni hatua kubwa katika kuboresha miundombinu ya data za 
hali ya hewa kitaifa na kimataifa, kuwezesha maamuzi sahihi ya kusaidia ustahimilivu wa kiuchumi na 
kimazingira. Kama sehemu ya mradi huo, Tanzania itanufaika kwa kuimarisha mifumo ya uangazi, 
teknolojia ya kisasa, pamoja na ushirikiano wa kimataifa.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...