Thursday, September 11, 2025

MVUA ZA VULI 2025: MVUA ZA WASTANI HADI CHINI YA WASTANI ZINATARAJIWA KATIKA MAENEO MENGI YA NCHI


Dar es Salaam; Tarehe 11 Septemba, 2025;

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema Mvua zinatarajiwa kuwa za Wastani hadi Chini ya Wastani katika maeneo mengi na kutawaliwa na vipindi virefu vya ukavu na mtawanyiko wa mvua usioridhisha hususan katika maeneo ya pwani ya kaskazini na nyanda za juu kaskazini mashariki.

Hayo yalisemwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC) Dkt. Ladislaus Chang’a wakati wa mkutano na vyombo vya habari kuhusiana na mwelekeo wa msimu wa mvua za Vuli (Oktoba hadi Disemba 2025), katika ukumbi wa Ubungo Plaza,Dar es Salaam,Tarehe 11 Septemba 2025. “Mvua zinatarajiwa kuanza wiki ya kwanza na ya pili ya mwezi Oktoba, 2025 katika maeneo ya mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Mara na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma na kusambaa katika maeneo ya pwani ya kaskazini na nyanda za juu kaskazini mashariki wiki ya kwanza na ya pili ya mwezi Novemba 2025. Mvua zinatarajiwa kuisha mwezi Januari, 2026”.  Alifafanua Dkt. Chang’a. 

Dkt. Chang’a alitoa wito kwa wananchi kufuatilia taarifa za utabiri wa saa24, siku 10, mwezi na tahadhari zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ikizingatiwa kuwa mwelekeo wa mvua uliotolewa ni kipindi cha msimu wa miezi mitatu, hivyo viashairia vinavyochangia mwenendo wa mifumo ya mvua na mabadaliko ya muda mfupu utazingatiwa katika uchambuzi wa utabiri wa muda wa kati na mfupi. “Mvua za Vuli zinatarajiwa kuongezeka kidogo mwezi Desemba, 2025 na Vipindi vya joto kali kuliko kawaida vinatarajiwa katika msimu huu wa Vuli”. Aliongeza Dkt. Chang’a

Aidha, Dkt. Chang’a alisema kuwa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania imeendelea kutoa taarifa za utabiri wa msimu mahususi kwa ngazi ya Wilaya.Wilaya 86 zilizo katika ukanda unaopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka zitapatiwa utabiri huo wa maeneo madogo.

Msimu wa Mvua za Vuli ni mahususi kwa maeneo ya nyanda za juu kaskazini mashariki (Mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro), pwani ya kaskazini (kaskazini mwa mkoa wa Morogoro, mikoa ya Pwani (ikijumuisha visiwa vya Mafia), Dar es Salaam, Tanga pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba), ukanda wa Ziwa Victoria (Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Mara) pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma.

Wednesday, September 10, 2025

TATHMINI YA MCHANGO WA WANAHABARI YAONESHA KURIDHISHWA NA USAHIHI WA UTABIRI WA HALI YA HEWA











Dar es Salaam; Tarehe 10 Septemba, 2025

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imekutana na wanahabari kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini ili kujadili utabiri wa msimu wa mvua za Vuli (Oktoba – Desemba) 2025, katika ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Usafirishaji (NIT). Akizungumza wakati wa mkutano huo Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a alisema kupitia warsha hizi uelewa wa wanahabari kuhusu masuala ya hali ya hewa umeendelea kuimarishwa kwa kiasi kikubwa na hivyo kuwezesha taarifa zitolewazo na mamlaka kufikia jamii kwa urahisi na kwa wakati.

“Mnamo mwezi Julai mwaka 2025, Mamlaka iliandaa Dodoso maalumu kwa wanahabari ili kufanya tathmini ya utendaji kazi wake kwa Tasnia ya Habari, ambapo kwa taarifa niliyonayo ni kwamba tathmini hiyo imekamilika na matokeo yake yanaonesha asilimia 95 ya wanahabari waliotoa maoni yao wameridhishwa na usahihi wa utabiri wetu na asilimia 96.3 wameonesha kuzielewa taarifa hizo zinazotolewa na TMA hivyo kuzifikisha kwa jamii kwa lugha rahisi”. Alisema Dkt. Chang’a.

Aidha, Dkt. Chang’a ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Wadau wa Maendeleo kwa kuendelea na uwekezaji katika miundombinu ya hali ya hewa nchini na hivyo kuwezesha Mamlaka ya Hali ya Hewa kuendelea kuboresha huduma zake kwa kutoa utabiri mahususi kwa sekta mbalimbali nchini.

“Kwa kuzingatia umuhimu wa huduma za hali ya hewa na changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuboresha miundombinu ya utoaji huduma za hali ya hewa ikiwemo ufungaji wa Rada za hali ya hewa na kuwajengea uwezo wataalam wa hali ya hewa, ambapo watumishi wapatao 97 wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania wanaendelea na masomo ya elimu ya juu ndani na nje ya nchi”. Alisema Dkt. Chang’a

Naye, mwanahabari kutoka Harvest FM, Bw. Yonna Mgaya alitoa mrejesho wa namna taarifa za hali ya hewa zimekuwa rahisi kupatikana kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na kufanikiwa kuzirusha zaidi ya mara mbili kwenye kituo chao. TMA inatarajia kutoa rasmi utabiri wa Msimu wa Mvua za Vuli 2025, tarehe 11 Septemba 2025, katika ukumbi wa Ubungo Plaza, Dar es Salaam.

Monday, September 8, 2025

TMA YAHIMIZWA KUENDELEA KUSHIRIKISHA WADAU ILI KUKABILIANA NA ATHARI ZA MABADILIKO YA HALI YA HEWA






















Dodoma; Tarehe 8, Septemba, 2025.

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imehimizwa kuendelea kushirikisha wadau kutoka sekta mbalimbali ili kukabiliana na athari za mabadiliko ya hali ya hewa nchini. Mgeni rasmi na Mwenyekiti wa Bodi ya TMA, Mhe. Jaji Mshibe Ali Bakari alisema hayo wakati akifungua mkutano wa 24 wa wadau katika kujadili Utabiri wa Msimu wa Mvua za Vuli (Oktoba hadi Disemba) 2025, wenye kaulimbiu “matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa katika kupanga na kutekeleza majukumu ya kila siku kwa maendeleo endelevu” uliofanyika kwenye ukumbi wa PSSSF, jijini Dodoma, tarehe 08/09/2025.

“Tunapoelekea kutoa Utabiri wa Mvua za Vuli (Oktoba hadi Disemba), 2025 napenda kuipongeza TMA na kuwahimiza kuendeleza utaratibu huu wa kuwashirikisha wadau kutoka sekta mbalimbali katika hatua za maandalizi ya utoaji wa utabiri wa mvua za misimu hapa nchini. Ushirikiano huu ni mfano wa kuigwa na unafaa kuendelezwa hasa katika kipindi hiki ambacho Dunia inakabiliwa na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa.” Alisema Jaji Mshibe. 

Aidha, Jaji Mshibe aliwasisitiza TMA kuhakikisha taarifa zinatoka mapema kama inavyostahiki kwa kutumia njia mbalimbali za mawasiliano. “Ulimwengu wa sasa upo kiganjani”. Aliongezea Jaji Mshibe.

Naye, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Tabianchi (IPCC) Dkt. Ladislaus Chang’a alielezea umuhimu wa ushirikishwaji wa wadau kutoka sekta mbalimbali katika utoaji wa huduma za hali ya hewa ambao umesaidia kuimarisha utoaji wa huduma za hali ya hewa na kuchochea matumizi sahihi ya huduma za hali ya hewa kwa jamii.

Wakitoa mrejesho wa athari za Mvua za Masika 2025 katika sekta zao, Mdau kutoka sekta ya kilimo, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Dodoma, Bw. Wilfred Kavishe aliipongeza TMA kwa kutoa taarifa sahihi zilizosaidia upangaji wa malengo ya mkoa katika uzalishaji, aliongezea kwa kusema kuwa Msimu wa Mvua za Masika 2025 Sekta ya Kilimo iliathirika kwa kiwango kikubwa hasa kwa wakulima ambao hawakufuata ushauri wa kitaalamu hali iliyopelekea malengo ya uzalishaji kuwa chini ya wastani ya matarajio yao. 

Naye mwakilishi wa wadau kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Uratibu wa Maafa) Bw. Emmanuel Lyimo alieleza namna taarifa za awali za mvua za Masika 2025 zilivyosaidia katika kuchukua hatua stahiki ikiwa ni pamoja na kuziandikia wizara, Mamlaka za Mikoa, kuandaa mkakati wa kukabiliana na maafa yanayoweza kutokea, kutoa mafunzo pamoja na kuandaa mpango wa dharura kwa maeneo yaliyotarajiwa kuathirika. 

Kupitia mkutano huo, wadau walielezwa tathmini ya utabiri wa Mvua za MASIKA (Machi hadi Mei) kwa mwaka 2025 ulikuwa sahihi kwa 87.5%, huku TMA ikitarajia kutoa rasmi utabiri wa Msimu wa Mvua za Vuli 2025 tarehe 11 Septemba 2025, Jijini Dar es salaam.



Saturday, September 6, 2025

TUKIO LA KUPATWA KWA MWEZI TAREHE 7 SEPTEMBA 2025


Dar es Salaam, 06 Septemba 2025:

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inapenda kutoa taarifa ya tukio la kupatwa kwa Mwezi linalotarajiwa kutokea tarehe 7 Septemba 2025.

Hali ya kupatwa kwa Mwezi ni tukio linalotokea wakati Dunia inapita kati ya Jua na Mwezi na kusababisha kivuli cha Dunia kuwa katika uso wa Mwezi. Aidha, hali hii hutokea wakati Dunia, Mwezi na Jua vinapokaa kwenye mstari mnyoofu. Tukio la kupatwa kwa mwezi limegawanyika katika aina kuu mbili. Aina ya kwanza ni kupatwa kwa Mwezi Kikamilifu (Umbra), hali ambayo Dunia inakuwa imefunika mwanga wote wa Jua na kupelekea kivuli kizito (giza) katika uso wa Mwezi. Aina ya pili ni kupatwa kwa Mwezi Sehemu (Penumbra) ambapo Dunia husababisha kivuli hafifu katika uso wa Mwezi. 

Tukio la kupatwa kwa Mwezi kwa tarehe 7 Septemba 2025 ni la kupatwa kwa Mwezi Sehemu na Kikamilifu. Tukio hili linatarajiwa kuonekana katika maeneo ya bara la Ulaya, Asia, Australia na Afrika. Kwa hapa nchini, hali ya kupatwa kwa Mwezi inatarajiwa kuanza kwa kupatwa kwa Mwezi Sehemu kuanzia pale Jua linapozama hadi saa 2:29 usiku na kufuatiwa na kupatwa kwa Mwezi Kikamilifu kuanzia saa 2:30 hadi saa 3:52 usiku. Aidha, tukio hili linatarajiwa kuhitimishwa kwa kupatwa kwa Mwezi Sehemu kuanzia saa 3:53 hadi 5:55 usiku. Kwa ujumla hali hii inatarajiwa kudumu kwa muda wa takriban masaa sita.

Kwa kawaida, mzunguko wa mwezi una uhusiano mkubwa na Kupwa na Kujaa kwa maji baharini. Hali hii inatarajiwa kuongezeka kwa kina cha maji katika Bahari wakati wa tukio hilo. Hata hivyo, hali hiyo haitarajiwi kupekelea athari kubwa. Hali ya anga inatarajiwa kuwa yenye mawingu kiasi na kutoa fursa nzuri ya kuonekana kwa tukio hilo kwa macho.

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania inaendelea kufuatilia tukio hili la kupatwa kwa Mwezi na na itatoa mrejesho kila inapobidi.

Wednesday, September 3, 2025

TMA YAKABIDHIWA RASMI HATI NA: DSMT1086126 YA ENEO LAKE LA KIPAWA



Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo ya Sayansi ya Mabadiliko ya hali ya Hewa Duniani (IPCC) Dkt. Ladislaus B. Chang'a amekabidhiwa rasmi hati  ya Kiwanja namba 173 chenye ukubwa wa mita za mraba 10,280 kilichopo Kipawa Wilayani Ilala, Dar es Salaam,tarehe 01/09/2025. Makabidhiano hayo yamefanyika katika ofisi ya Msajili wa Hati Kanda ya Mashariki Adv. Burton Rutta zilizopo Kivukoni, Dar es Salaam. Dkt. Chang'a aliishukuru  Ofisi ya Msajili wa Hati kwa ushirikiano uliotolewa na watumishi wa ofisi hiyo katika kufanikisha upatikanaji wa hati hiyo muhimu kwa TMA na Serikali kwa ujumla.

Sunday, August 31, 2025

DKT. LADISLAUS CHANG’A ASHIRIKI KATIKA MKUTANO WA 6 WA MAWAZIRI NA MAMLAKA ZA MAZINGIRA WA ASIA NA PASIFIKI

 




Nadi, Fiji – 29 Agosti 2025

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC), Dkt. Ladislaus Chang’a, kwa mwaliko wa Programu ya Umoja wa Mataifa uratibu wa Mazingira (UNEP) ameshiriki kikamilifu katika Mkutano wa 6 wa Mawaziri na Mamlaka za Mazingira wa Asia na Pasifiki (6th AP Forum) uliofanyika kuanzia tarehe 26–29 Agosti 2025 Jijini Nadi, Fiji. Mkutano huo uliandaliwa kwa pamoja na Serikali ya Fiji na UNEP ukiwa na kaulimbiu “Kutafuta Suluhisho Endelevu katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi Duniani”.

Sambamba na mkutano huo, Dkt. Chang’a alikuwa na vikao mbalimbali na waheshimiwa na taasisi mbalimbali ikiwa ni pamoja na kikao na Mhe. Rupa B. K., Waziri wa Serikali ya Nepal, Wizara ya Misitu na Mazingira, ambapo alimpatia taarifa kuhusu mpango kazi wa IPCC unaotekelezwa hadi mwaka 2029. Mazungumzo hayo yalijikita katika kuimarisha ushirikiano wa kikanda na kimataifa katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kuboresha sera za mazingira. Mhe. Rupa alishukuru na kupongeza sana kazi kubwa inayofanywa na IPCC.

Aidha, Dkt. Chang’a alishiriki na kuratibu kikao cha ngazi ya Mawaziri kuhusu Mfumo wa tahadhari za majanga ikiwa ni pamoja na yale yanayosababishwa na hali ya hewa. Kikao hiki cha Waheshimiwa Mawaziri wa Asia na Pasifiki kilikuwa na wazungumzaji (panelists) wakiwemo: Mhe. Thoriq Ibrahim, Waziri wa Utalii na Mazingira wa Maldives; Mhe. Bi. Mona Ainu’u, Waziri wa Rasilimali Asili wa Niue; Mhe. Dkt. Maina Vakafua Talia, Waziri wa Mambo ya Ndani, Mabadiliko ya Tabianchi na Mazingira wa Tuvalu; Bi. Fleur Downard, Mkurugenzi wa Masuala ya Mazingira ya Kimataifa na Kitengo cha Umoja wa Mataifa, Wizara ya Mabadiliko ya Tabianchi, Nishati, Mazingira na Maji, wa Australia; na Bw. Sefanaia Nawadra, Mkurugenzi Mkuu, Sekretarieti ya Programu ya Mazingira kanda ya Pasifiki (Pacific Regional Environment Programme-SPREP).

Kikao hicho kiliangazia umuhimu wa mifumo ya tahadhari za majanga (multi-hazard early warning systems-MHEWS) kama mojawapo ya hatua bora zinazotekelezeka katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi, kwa lengo la kulinda maisha na mazingira”.

Mkutano huu wa 6 wa Waheshimiwa Mawaziri wa Asia na Pasifiki wenye dhamana ya sekta ya mazingira ulikuwa pia jukwaa muhimu kwa makundi mbalimbali katika ukanda huo wawakilisha serikali zao, mashirika ya kikanda, vijana, sekta binafsi na wadau ambapo mchango na maoni yao vitasaidia katika maandalizi ya Mkutano wa 7 wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mazingira (Seventh Session of the United Nations Environment Assembly (UNEA-7) unaotarajiwa kufanyika mwezi Desemba 2025 jijini Nairobi, Kenya.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...