
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) inapenda kutoa taarifa ya hali la joto katika maeneo mbalimbali nchini.
Kumekuwepo na ongezeko la joto katika baadhi ya maeneo nchini hususan yapatayo misimu miwili ya mvua kwa mwaka kwa miezi ya hivi karibuni. Hali hii imesababishwa na kusogea kwa jua la utosi sambamba na upungufu wa mvua unaojitokeza katika maeneo hayo. Kwa kawaida vipindi vya jua la utosi nchini hufikia kilele mwishoni mwa mwezi Novemba wakati jua la utosi likiwa linaelekea kusini (Tropiki ya Kaprikoni) na hali hiyo hujirudia tena mwezi Februari wakati jua la utosi likiwa linaelekea kaskazini (Tropiki ya Kansa). Jua la utosi huambatana na hali ya ongezeko la joto kwa sababu uso wa dunia katika eneo tajwa huwa karibu zaidi na jua kuliko maeneo mengine.
Katika kipindi cha mwezi Februari, 2025 hali ya ongezeko la joto imeendelea kujitokeza katika baadhi ya maeneo nchini, ambapo hadi kufikia tarehe 11 Februari, 2025 kituo cha hali ya hewa cha Mlingano (Tanga) kiliripoti kiwango cha juu zaidi cha nyuzi joto 36.0°C mnamo tarehe 05 Februari ikiwa ni ongezeko la nyuzi joto 2.1°C ukilinganisha na wastani wa muda mrefu kwa mwezi Februari. Kituo cha hali ya hewa kilichopo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es salaam kiliripoti kiwango cha juu cha nyuzi joto 35.0°C mnamo tarehe 10 Februari, 2025 (ongezeko la nyuzi joto 2.2°C). Kituo cha Tanga kiliripoti nyuzi joto 35.1°C mnamo tarehe 10 Februari (ongezeko la nyuzi joto 2.3°C), Kibaha nyuzi joto 35.8 °C mnamo tarehe 10 Februari (ongezeko la nyuzi joto 3.0°C), na Kilimanjaro nyuzi joto 34.3°C mnamo tarehe 09 Februari, 2025 (ongezeko la nyuzi joto 0.6°C).
Aidha, ongezeko la unyevu angani (Relative humidity) katika kipindi hiki linalosababishwa na mvuke wa bahari hususan katika maeneo ya ukanda wa pwani na maeneo jirani limechangia pia mwili kuhisi joto zaidi ya viwango vinavyoripotiwa.
Vipindi vya ongezeko la joto vinatarajiwa kuendelea kujitokeza katika mwezi huu wa Februari, 2025 hususan katika maeneo ambayo msimu wa mvua za Vuli umeisha.
Hali ya joto kali inatarajiwa kupungua katika maeneo hayo mwezi Machi, 2025 hususan wakati ambapo mvua za msimu wa Masika zitakapoanza.
Kwa taarifa hii wananchi wanashauriwa kuendelea kuzingatia taarifa na tahadhari za hali mbaya ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania sambamba na kutafuta, kupata na kufuata ushauri wa wataalam katika sekta husika ili kupunguza athari zinazotokana na hali mbaya ya hewa.
Dar es Salaam, 6 Februari 2025
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu wa Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC) Tarehe 6 Februari 2025 alipata fursa ya kuwahamasisha na kuwajengea uwezo zaidi kuhusu sayansi ya mabadiliko ya hali ya hewa na athari zake na namna ya kukabiliana nayo kwa wataalamu wa baadhi ya taasisi zisizo za kiserikali waliokuwa wanashiriki mafunzo ya siku moja yanayohusiana utekelezaji wa miradi ya kijamii kwa kuzingatia athari za mabadiliko ya tabia nchi "Partner's Capacity Building on Climate Action Integration into Development Programming".
Mafunzo hayo yamefadhiliwa na Ubalozi wa Ireland nchini. Taasisi zilizohudhuria mafunzo haya ni pamoja na Taasisi ya Benjamin Mkapa Foundation, AMREF International, UZIKWASA na Pangani fm.
Pamoja na kuelezea shughuli na taratibu za IPCC, Dkt.Chang'a amewahamasisha washiriki wa mafunzo kushiriki kwa wingi katika maandalizi ya ripoti za IPCC katika mzunguko wa saba ulioanza Julai 2023 na utakamilika kati ya 2029 au 2030 kwa kufanya tafiti na kutoa maoni kwenye ripoti mbalimbali za IPCC, "ushiriki wako unaweza kuwa walao kuweka maoni kwenye eneo moja la ripoti za IPCC na ukawa kwenye kumbukumbu miongoni wa wataalamu waliofanikisha ripoti hizi", alisema Dkt. Chang'a.
Tarehe: 04 Februari, 2025; Dodoma.
Katika kuendelea kuboresha usambazaji wa taarifa za hali ya hewa kwa jamii kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetembelewa na Wataalamu wa Shirika lisilo la Kiserikali la Uhifadhi wa Mazingira na Maendeleo ya Kiuchumi la EMEDO ambalo linalojihusisha na uhifadhi wa mazingira katika maeneo yanayozunguka Ziwa Viktoria.Ziara ya EMEDO ilikuwa na lengo la kujadiliana namna ya kuendelea kushirikiana katika usambazaji wa taarifa za hali ya hewa ili kuwafikia wananchi wengi zaidi wa maeneo yanayozunguka Ziwa Viktoria hususani wavuvi. Kikao kati ya TMA na EMEDO kimefanyika Februari 4,2025 kwenye Ofisi za TMA Makao Makuu,Jijini Dodoma.
Wakati wa ziara hiyo yamefanyika majaribio ya matumizi ya kifaa maalumu cha usambazaji wa taarifa za hali ya hali ya hewa “Electronic Weather Board”, ambacho kitawasaidia wavuvi na watumiaji wa Ziwa Victoria kwenye kisiwa cha Goziba kuona utabiri wa hali ya hewa unaotarajiwa katika Ziwa kwa lengo la kufanya maamuzi sahihi ili kuokoa maisha na mali.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA Dkt.Ladislaus Chang'a aliushukuru uongozi wa Shirika la EMEDO kwa ushirikiano unaoendelea kati ya Taasisi hizi wenye lengo la kusambaza taarifa na elimu ya matumizi sahihi ya taarifa zitolewazo na TMA katika maeneo ya ziwa Victoria.
"Haya ni mambo muhimu sana tunapaswa kufanya ili kuoanisha shughuli zetu na maono ya kimkakati na kuleta thamani kwa kile tunachofanya. Nimevutiwa sana na ushirikiano huu kwa sababu tunataka kila mmoja wetu kuchangia katika kufikia maono ya Taifa. Kwa mfano, kuimarisha hatua za kijamii kuhusu mabadiliko ya tabianchi na kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa Duniani ".Alisema Dkt.Ladislaus Chang'a
Awali, Mkurugenzi Mkuu wa EMEDO, Bi. Editrudith Lukanga, alishukuru pia Mamlaka kwa ushirikiano huu na kusema kuwa TMA imekuwa ikitoa wataalamu wake katika kutoa mafunzo kwa jamii na pia kutoa utabiri wa hali ya hewa, jambo ambalo limekuwa na manufaa kwa jamii.
Kwa upande wake Meneja Mradi wa EMEDO,Bw.Arthur Mugema alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya Taasisi hizi ndio umeleta matokeo ya kuandaa na kuweka kifaa cha kielektroniki (Electronic Weather Board) kwenye kisiwa cha Goziba ambacho kinaenda kuboresha upatikanaji wa taarifa za hali ya hewa.
Dar es Salaam, Tarehe 30/01/2025
Katika kuboresha ufanisi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA),Taasisi ya Uongozi imetoa mafunzo ya siku mbili kwa Bodi ya TMA.Mafunzo hayo yalifunguliwa rasmi na Mwenyekiti wa Bodi Mh.Jaji Mshibe Ali Bakari katika ukumbi wa mikutano wa PSSSF Jengo la Millenium II,Jijini,Dar es Salaaam tarehe 29 hadi 30 Januari 2025.
Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo, Mh, Jaji.Mshibe alisema “Jambo muhimu katika mafunzo haya ni kuimarisha ushirikiano na uwazi ili kuleta ufanisi katika utendaji kazi kwenye Taasisi yetu’’
Katika hatua nyingine,Bodi hiyo ilifanya ziara ya kutembelea mradi wa ofisi ya Kanda ya Mashariki na kituo cha Tahadhari ya Matukio ya Tsunami,ambapo Katibu wa Bodi na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi,Dkt.Ladislaus Chang’a aliishukuru Bodi, kwa kutembelea eneo la mradi na kwa maelekezo na miongozo ya kuhakikisha kuwa mradi unafanyika kwa ufanisi.
Mafunzo hayo yamejumuisha Bodi na Menejimenti ya TMA ambapo mada mbalimbali zilitolewa ikiwemo uongozi bora,uongozi wa kimkakati na vihatarishi vinavyoweza kukwamisha ufanisi wa Taasisi.
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetoa rasmi Utabiri wa Msimu wa Mvua za Masika 2025 kwa maeneo yanayopata mvua mara mbili kwa mwaka. Akizungumza wakati wa mkutano na vyombo vya habari katika ukumbi wa mikutano wa Ubungo Plaza, Tarehe 23 Januari 2025, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Mwakilishi wa Kudumu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Changa alisema mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki pamoja na Mashariki mwa mikoa ya Mara na Simiyu huku mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani zikitarajiwa katika maeneo ya Pwani ya Kaskazini, Kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma na Ukanda wa Ziwa Victoria.
“Mvua za Wastani hadi Juu ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya Nyanda za Juu Kaskazini Mashariki pamoja na Mashariki mwa Mikoa ya Mara na Simiyu. Aidha, mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani zinatarajiwa katika maeneo ya Pwani ya Kaskazini, Kaskazini mwa Mkoa wa Kigoma na Ukanda wa Ziwa Victoria (Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga na magharibi mwa mikoa ya Simiyu na Mara) katika kipindi cha Msimu wa Masika, 2025.” Alisema Dkt. Chang’a
Vilevile, taarifa hiyo imeelezea pia ongezeko la mvua linatarajiwa katika kipindi cha mwezi Aprili sambamba na kutoa angalizo la matukio ya hali mbaya ya hewa ikiwemo vipindi vya mvua kubwa kujitokeza hata katika maeneo yanayotarajiwa kupata mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani.
Akizungumzia athari zinazoweza kujitokeza, Dkt. Chang’a alisema Mvua za Wastani hadi Chini ya Wastani zinazotarajiwa katika baadhi ya maeneo zinaweza kupelekea upungufu wa upatikanaji wa maji kwa matumizi ya majumbani, kilimo na ufugaji.
Ili kupata taarifa zaidi za utabiri huu, tembelea: https://www.meteo.go.tz/uploads/publications/sw1735801516-Mwelekeo%20wa%20Hali%20ya%20Hewa%20Januari,%202025.pdf
Dar es Salaam; Tarehe 22, Januari 2025
“TMA inaendelea kuweka mikakati ya kuhakikisha warsha za wanahabari zinaendelea kuwa endelevu na kuboreshwa zaidi, Hatua za uboreshwaji ni pamoja na uanzishwaji wa Tuzo za Wanahabari bora wa habari za hali ya hewa kila mwaka, hivyo ninawakumbusha wanahabari wote nchini, kuwasilisha kazi zenu za ushindani kupitia barua pepe elekezi ili muda wa mchakato ukifika wapatikane washindi waliokidhi vigezo.”
Hayo yalizungumzwa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Mwakilishi wa Kudumu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt. Ladislaus Chang’a alipokuwa akifungua rasmi mkutano wa wanahabari katika kujadili Utabiri wa Mvua za Msimu wa MASIKA unaoanzia mwezi Machi hadi Mei 2025.
Aidha, Dkt. Chang’a aligusia kuhusu changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa kwa kuwa mwaka 2024 ulivunja rekodi kwa kuwa mwaka wenye ongezeko kubwa zaidi la joto Duniani kwa ongezeko la takribani nyuzi joto 1.550C na upande wa Tanzania ongezeko la joto lilifikia nyuzi joto 0.70C, hivyo kuashiria uhitaji wa jitihada kubwa za pamoja za jumuiya ya kimataifa za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa. Aliwahamasisha wanahabari kujipanga vizuri ili kuendelea kuelimisha jamii.
Kwa upande wa mwakilishi wa wanahabari kutoka Daily News Digital Bi. Zaituni Mkwama alitoa mrejesho wa namna walivyosambaza Utabiri wa mvua za Vuli 2024 uliotolewa na TMA kwa kuonesha kuwa mvua hazitakuwa za kutosha, hali iliyosaidia Serikali kuweka miundombinu mizuri na kuhakikisha chakula kinapatikana cha kutosha hapa nchini.
“Baada ya wanahabari kusambaza Utabiri wa Mvua za VULI 2024 uliotolewa na TMA ilipelekea Serikali kuweka miundombinu rafiki kwa kuhakikisha chakula kinapatikana kwa kuitosheleza nchi.”. Alisema Bi. Zaituni Mkwama.
Katika mkutano huu, wanahabari walipata fursa ya kuona utabiri wa hali ya hewa katika kipindi cha mwezi Machi hadi Mei, 2025 na kutoa michango yao juu ya namna bora na sahihi zaidi ya usambazaji wake.
Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...