Wataalamu Wabobezi katika sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi wamekutana jijini Arusha katika kongamano la siku moja kwa lengo la kujadili mchango wao katika kukabiliana na mabadiliko hayo, tarehe 31 Machi 2025.
Kongamano hilo limeandaliwa mahsusi kwa ajili ya kuongeza uelewa kuhusu shughuli za Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (IPCC); Ripoti zitakazoandaliwa katika mzunguko wa saba wa IPCC (AR7) kuhusu tathmini ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi na fursa za kushiriki katika mchakato huo, ikijumuisha uandishi, uteuzi wa wataalamu na mapitio ya ripoti za IPCC. Vilevile kongamano hilo lilihamasisha wanasayansi hasa vijana, watendaji, wakufunzi na wanafunzi kufuatilia na kushiriki katika mchakato mzima wa shughuli za IPCC hasa katika mzunguko wake wa saba ulioanza mwaka 2023 na unatarajiwa kumalizika kati ya mwaka 2029 na 2030.
Kongamano limeratibiwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nelson Mandela, likijumuisha wataalamu wa sayansi ya mabadiliko ya hali ya hewa na tasnia zinazohusiana kutoka Tanzania na Afrika Mashariki.
Mgeni rasmi katika ufunguzi wa kongamano hilo alikuwa Mwenyekiti wa Bodi ya TMA Mhe. Jaji Mshibe Ali Bakari ambaye kupitia hotuba yake alisisitiza ushiriki wa wataalamu wengi kutoka Afrika Mashariki katika mchakato wa IPCC.
“Ni matumaini yangu kuwa kupitia makongamano kama haya ya uhamasishaji wa wanasayansi kujihusisha katika kufanya tafiti zinazokidhi matakwa ya IPCC, wataalam wengi zaidi kutoka Afrika Mashariki wataweza kutoa mchango wao kikamilifu katika utayarishaji wa ripoti za tathmini ya Saba ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi ya IPCC (IPCC AR7). Alisema Jaji. Mshibe
Naye, Dkt. Ladislaus Chang’a, Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na Makamu Mwenyekiti wa IPCC alielezea namna ambavyo ripoti za IPCC zimekuwa na mchango mkubwa katika mapambano dhidi ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi kimataifa na katika nchi moja moja.
“Ripoti ya IPCC ya AR7 inayoandaliwa inatarajiwa kuwa ya kina na itakuwa na jukumu muhimu katika mustakabali wa hatua za kuchukua dhidi ya mabadiliko ya hali ya hewa natabianchi kwa kuzingatia taarifa za kisayansi zilizohakikiwa vyema ambapo zina mchango mkubwa katika kuongeza ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi kikanda na Duniani kote”. Aliongeza Dkt. Changa.