Friday, May 10, 2019

MWENENDO WA HALI YA HEWA HUSUSAN MVUA ZA MFULULIZO ZINAZOENDELEA KUNYESHA KATIKA BAADHI YA MAENEO HAPA NCHINI

Kaimu Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania(TMA) Bw. Samwel Mbuya, mbele ya waandishi wa habari  akielezea mwenendo wa hali ya hewa hususan mvua za mfululizo zinazoendelea kunyesha katika baadhi ya maeneo hapa nchini



Taarifa hii inatoa mwenendo wa hali ya hewa hususan mvua za mfululizo zinazoendelea kunyesha katika baadhi ya maeneo hapa nchini.

Mvua zinazoendelea kunyesha hapa nchini hususan katika maeneo ya pwani ya kaskazini, nyanda za juu kaskazini mashariki na kanda ya ziwa Victoria ni sehemu ya mvua za Masika. Mvua hizi zinatokana na kuimarika kwa ukanda wa mvua (ITCZ). Mvua za mfululizo katika baadhi ya maeneo ya pwani ya kaskazini (mikoa ya Tanga, Dar es salaam na Pwani pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba) zinatarajiwa kuendelea kwa kipindi cha siku mbili zijazo (mpaka siku ya jumapili tarehe 12 Mei 2019). Aidha vipindi vya mvua za mfululizo vinatarajiwa kujirudia kuanzia katikati ya mwezi Mei, 2019. Mamlaka itatoa taarifa za mara kwa mara za mwenendo wa mvua hizo katika taarifa zake za utabiri.
ANGALIZO: Pamoja na kwamba mvua za masika zinatarajiwa kupungua katika maeneo mengi mwishoni mwa mwezi Mei, 2019; athari za mvua kubwa zilizonyesha katika kipindi cha wiki moja mfululizo katika ukanda wa pwani ya kaskazini pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba zimesababisha kutuama kwa maji na mafuriko. Hivyo kutokana na ardhi kuwa na unyevunyevu mwingi, ongezeko kidogo la mvua linaweza kuendelea kusababisha athari kama zilizokwisha jitokeza.

USHAURI: Wananchi wanashauriwa kuendelea kufuatilia taarifa za utabiri kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania na kuzingatia tahadhari zilizotolewa na mirejeo yake pamoja na kupata na kuzingatia ushauri na miongozo ya wataalam katika sekta husika ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...