Monday, March 11, 2019

TMA YAKUTANA NA WADAU WA HUDUMA ZA BAHARINI KUJADILI NAMNA YA KUBORESHA HUDUMA ZA HALI YA HEWA KWA USALAMA WA MAISHA YA WATU NA MALI ZAO.
















Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) katika jitihada zake za kutambua umuhimu wa ushirikishwaji wa wadau wa huduma za hali ya hewa ili kuhakikisha huduma zitolewazo zinakidhi matwaka ya watumiaji, imekutana na wadau wa huduma za hali ya hewa baharini ili kupata mrejesho wa huduma zinazotolewa na kuweza kuzifanyia maboresho kulingana vigezo vya kitaifa na kimataifa.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho cha wadau wanaotumia huduma za hali ya hewa kwa shughuli baharini kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Baharia (DMI), tarehe 08 Machi 2019, mkurugenzi mkuu wa TMA Dkt. Agnes Kijazi aliwaeleza washiriki wa mkutano lengo ni kutoa uelewa wa huduma zitolewazo na kupokea mrejesho pamoja na kuibua fursa za ushirikiano kati ya TMA na wadau hao na kusaidia katika kuboresha huduma.

lengo la mkutano huu ni kuwapa uelewa wa huduma za hali ya hewa zinazotolewa kwaajili ya watumiaji wa bahari na pia kupata mrejesho kutoka kwenu kuhusu huduma hizo sambamba na kuibua fursa za ushirikiano kati ya TMA na ninyi watumiaji wa huduma za hali ya hewa ili kuboresha huduma zinazotolewa katika sekta hii ya bahari ‘Alizungamza Dkt. Kijazi’.

Aidha, aliongezea kwa kueleza kuwa mkutano huo unasaidia kuibua fursa na changamoto zilizopo ili kwa pamoja tuweze kufanikiwa katika utoaji na utumiaji wa huduma za hali ya hewa kwa shughuli za bahari na maziwa makuu kwa kuzingatia miongozo ya ndani na miongozo inayotolewa na Mashirika ya kimataifa ikiwemo  Shirika la Hali ya Hewa Duniani - (WMO);  Shirika la Kimataifa la Bahari – (IMO) na Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa kupitia kamisheni inayohusu masuala ya bahari ya Hindi - (UNESCO-IOC).

Vile vile, wadau walipata fursa ya kupitia mfumo mpya wa mawasiliano unaoitwa Mfumo wa Mawasiliano wa Taarifa za za Hali ya Hewa Baharini – Marine Meteorological Information System (MMIS) unaoundwa na kuweza kutoa michango yao ya maboresho kabla ya kuzinduliwa rasmi.

Kwa upande wa wadau waliipongeza TMA kwa kuandaa warsha/mkutano kama huo wenye lengo la kukidhi mahitaji ya wadau na kushauri kuwa endelevu ili kufika malengo ikiwa ni pamoja na mafunzo ya mfumo, kufanikisha huduma za baharini zinapata cheti cha ubora kama zilivyo huduma za usafiri wa anga.

Mkutano huo wa wadau uliwakutanisha wadau kutoka Mamlaka ya Bandari za Tanzania Bara na Visiwani (TPA na ZPC), Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC),   Chuo cha Bahari (DMI), Wakala wa Ufundi na Umeme (TEMESA), Chama cha Maafisa wa Meli Tanzania (MNOAT), Shirika la Maendeleo ya Mafuta (TPDC),  wakala wa makampuni ya meli kama vile PIL, MESSINA, Chama cha Mabaharia (TSC), Flyinghorse na wengine wengi

IMETOLEWA NA
OFISI YA UHUSIANO
MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...