Monday, December 30, 2019

MENEJIMENT YA TMA YAJIPANGA UTEKELEZAJI WA SHERIA YA MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA

Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi katika picha ya pamoja na washiriki wa kikao kazi cha kujenga uelewa na mkakati wa utelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa kilichofanyika Kibaha, Tarehe 27-28 Desemba 2019.
Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi akizungumza na washiriki wa kikao kazi cha kujenga uelewa na mkakati wa utelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa kilichofanyika Kibaha, Tarehe 27-28 Desemba 2019.
 Mwanasheria wa TMA Ndugu, Emmanuel Ntenga akifafanua baadhi ya vifungu vya sheria kwa washiriki wa kikao kazi cha kujenga uelewa na mkakati wa utelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa kilichofanyika Kibaha, Tarehe 27-28 Desemba 2019.
 Mkurugenzi wa Ofisi ya Zanzibar-TMA, Ndugu, Mohamed Ngwali akizungumza katika kikao kazi cha kujenga uelewa na mkakati wa utelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa kilichofanyika Kibaha, Tarehe 27-28 Desemba 2019.
Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri-TMA, Dkt. Hamza Kabelwa akizungumza katika kikao kazi cha kujenga uelewa na mkakati wa utelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa kilichofanyika Kibaha, Tarehe 27-28 Desemba 2019.
Mkurugenzi wa Utafiti na Matumizi-TMA, Dkt. Ladislaus Chang'a akizungumza katika kikao kazi cha kujenga uelewa na mkakati wa utelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa kilichofanyika Kibaha, Tarehe 27-28 Desemba 2019.
Mkurugenzi wa TEHAMA na Huduma za Ufundi-TMA, Dkt. Pascal Waniha akizungumza katika kikao kazi cha kujenga uelewa na mkakati wa utelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa kilichofanyika Kibaha, Tarehe 27-28 Desemba 2019.
Meneja Rasilimali Watu Bi. Mariam Is-Haaq akizungumza katika kikao kazi cha kujenga uelewa na mkakati wa utelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa kilichofanyika Kibaha, Tarehe 27-28 Desemba 2019.
Washiriki wakizungumza katika kikao kazi cha kujenga uelewa na mkakati wa utelezaji wa sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa kilichofanyika Kibaha, Tarehe 27-28 Desemba 2019.

Kibaha, 28 Desemba 2019;

Menejimenti ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imefanya kikao kazi kwa siku mbili ili kupitia kwa pamoja na kupata uelewa wa namna bora ya utekelezaji wa sheria Na. 2 ya mwaka 2019 ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania.

Akizungumza wakati wa kufunga kikao kazi hicho, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na mwenyekiti wa kikao aliwataka wakurugenzi na mameneja kujenga utamaduni wa utendaji kazi wenye lengo la uboreshaji huduma ilikufikia malengo ya Mamlaka katika utekelezaji wa sheria iliyopo. Aidha, aliwapongeza na kuwashukuru washiriki wa kikao kazi hicho kwa jinsi walivyojitoa kuifanya kazi hiyo kwa umakini mkubwa kwa zaidi ya saa kumi na mbili za kazi kila siku pasipo mtu yoyote kuondoka.

‘Nataka baada ya kikao hiki viongozi wote muwe mstari wa mbele katika kuhakikisha watumishi mnaowasimamia wana fahamu sheria, taratibu na kanuni kwenye utekelezaji wa majukumu yao kwa maslahi ya Mamlaka na Taifa kwa ujumla’. Alizungumza Dkt. Kijazi.

Awali, akifungua kikao kazi hicho Dkt. Kijazi aliwapongeza wafanyakazi wote wa TMA kwa utendaji mzuri wa kazi uliopelekea kufanikiwa kukishikilia cheti cha ubora cha ISO 9001:2015 baada ya ukaguzi uliofanyika kati ya tarehe 16 na 20 Disemba, 2019 ambapo TMA ilikaguliwa na Mkaguzi wanje kutoka Canada.

Kikao kazi hicho kiliwakutanisha Mkurugenzi Mkuu, wakurugenzi, Mkurugenzi Ofisi ya Zanzibar, Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Hali ya Hewa- Kigoma, mameneja kutoka makao makuu, mameneja wa Kanda na wanasheria wa TMA.

Awali, wajumbe walipitia vifungu vyote vya sheria na kujadili kwa kina ili kuhakikisha viongozi wote wa Mamlaka wanakuwa na uelewa wa pamoja wa sheria hiyo ili kurahisisha utekelezaji wake katika maeneo yao ya kazi na hivyo kuchangia katika ustawi wa maendeleo ya nchi kupitia sayansi ya hali ya hewa.

Aidha, wajumbe hao waliainisha maeneo ya uboreshaji katika kanuni hususan kwenye udhibiti wa huduma za hali ya hewa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ukusanyaji mapato, utoaji huduma za hali ya hewa kwa usahihi na kwa wakati pamoja na kutoa elimu kwa umma na wadau kuhusu sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania. 

‘Tunapaswa kutoa elimu kwa umma hasa wale wadau ambao wanamiliki vituo vya hali ya hewa watambue kwamba ni kosa kisheria kuwa na vituo ambavyo havijasajiliwa na pia kutumia vifaa ambavyo havijahakikiwa (calibration) na TMA’ . Alisema Dkt. Kijazi.

Naye Mkurugenzi wa Ofisi ya Zanzibar-TMA, Ndugu. Mohamed Ngwali akitoa salamu za shukrani kwa niaba ya washiriki wote, alimshukuru Mkurugenzi Mkuu wa TMA kwa kufanikisha kikao kazi ambacho kimeongeza uelewa mpana wa matumizi ya sheria mpya ya TMA na kuahidi kudumisha umoja katika utendaji kazi kwa watumishi wote.

Tuesday, December 24, 2019

TMA YASISITIZA WADAU KUCHOCHEA MATUMIZI SAHIHI YA TAARIFA ZA HALI YA HEWA KATIKA SEKTA ZAO.

Wadau wakiwa kwenye picha ya pamoja na mgeni rasmi, Dkt. Hamza Kabelwa (katikati mwenye miwani) katika warsha ya wadau kutoka sekta mbalimbali inayohusu matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa baina ya muandaaji na mtumiaji, iliyofanyika katika ukumbi wa Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Pwani kuanzia Tarehe 22-24 Disemba, 2019.
Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania(TMA), Dkt. Hamza Kabelwa (Kushoto) akizungumza wakati akifungua warsha ya wadau kutoka sekta mbalimbali inayohusu matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa baina ya muandaaji na mtumiaji, iliyofanyika katika ukumbi wa Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Pwani kuanzia Tarehe 22-24 Disemba, 2019.
Wataalam wa hali ya hewa kutoka TMA wakiwasilisha mada katika warsha ya wadau inayohusu matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa baina ya muandaaji na mtumiaji, iliyofanyika katika ukumbi wa Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Pwani kuanzia Tarehe 22-24 Disemba, 2019.
Wadau mbalimbali wakichangia mada katika warsha ya wadau kutoka sekta mbalimbali inayohusu matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa baina ya muandaaji na mtumiaji, iliyofanyika katika ukumbi wa Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Pwani kuanzia Tarehe 22-24 Disemba, 2019.



MKURANGA, PWANI  22/12/2019;
Mkurugenzi wa Huduma za Utabiri wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Hamza Kabelwa kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TMA Dkt. Agnes Kijazi alifungua warsha ya wadau kutoka sekta mbalimbali iliyohusu matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa baina ya muandaaji na mtumiaji wa taarifa za hali ya hewa, iliyofanyika katika ukumbi wa Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Pwani kuanzia Tarehe 22-24 Disemba, 2019.

Katika hotuba  yake Dkt. Kabelwa  alisisitiza wadau mara watakapomaliza warsha hiyo kuchochea matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa katika sekta zao ili kupunguza au kuepusha athari zinazoweza kusababishwa na hali mbaya ya hewa.

“Mkiwa kama kiunganishi kati ya  TMA na wananchi tunawaomba ninyi washiriki kuchochea matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa katika sekta zenu”, alisisitiza Dkt. Kabelwa.

Aidha, washiriki walikumbushwa kutambua kuwa majanga ya asili hayawezi kuepukika, lakini taarifa zikiwafikia walengwa kabla ya janga husika kutokea basi zitasaidia kujipanga ili kukabiliana na madhara yanayoweza kujitokeza, hivyo Dkt. Kabelwa aliwataka washiriki kushirikiana na TMA kuhakikisha taarifa za hali ya hewa zinawafikia walengwa kwa wakati na kueleweka.

Warsha hiyo iliandaliwa na TMA na kufadhiliwa na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (World Meteorological Organization – WMO), chini ya mwamvuli wa Programu ya kidunia ya kuwaongezea ujuzi waandaaji na watumiaji wa taarifa za hali ya hewa barani Afrika (Weather and Climate Information Services for Africa - WISER).

Thursday, December 19, 2019

TMA YAWEKA MSISITIZO WA KUKABILIANA NA CHANGAMOTO ZA MABADILIKO YA HALI YA HEWA BAHARINI.

Dkt. Agnes  Kijazi, akitoa mada kuhusu umuhimu wa kuzijengea uwezo mamlaka za hali ya hewa katika nchi wanachama wa shirika la hali ya hewa duniani.

Dkt. Agnes  Kijazi,  akishiriki katika jopo la majadiliano kuhusiana na  matukio ya hali mbaya ya hewa yanayojitokeza ikiwemo vimbunga katika bahari.

Dkt. Agnes Kijazi, akitoa mada kuhusiana na mahusiano ya masuala ya Jinsia na changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa.

Kutokea kulia ni Dkt. Agnes Kijazi akifuatiwa na Mwenyekiti wa IPCC Profesa. Hoesung Leena pamoja na Dkt. Ladislaus Chang’a katika picha ya pamoja wakati wa majadiliano kuhusiana na maandalizi ya ripoti ya sita ya tathmini ya mabadiliko ya hali ya hewa inayotarajiwa kukamilishwa mwaka 2022.

Dkt. Ladislaus Chang’a (kulia) akishiriki katika majadiliano kuhusiana na maandalizi ya Ripoti ya sita ya tathmini ya mabadiliko ya hali ya hewa inayotarajiwa kukamilishwa mwaka 2022.



Katibu Mkuu wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Prof. Petteri Taalas (wa pili kutoka kulia) wakijadiliana na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ambaye pia ni Makamu wa tatu wa Rais wa  Shirika la Hali ya Hewa Duniani, Dkt. Agnes Kijazi, wakiwa pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Uganda pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa  Malawi (wa kwanza kutoka kushoto) mara baada ya kusainiwa kwa makubaliano ya kuimarisha huduma za hali ya hewa katika nchi zinazoendelea baina ya shirika la hali ya hewa duniani na taasisi za kibenki na mashirika mengine ya kimataifa yakiwemo, UNDP, AfDB, WFP.

Madrid, Hispania Tarehe 13/12/2019;
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imeshiriki Mkutano wa 25 wa Kimataifa wa Mabadiliko ya Hali ya Hewa (2019 United Nations Framework Convention on Climate Change-UNFCCC-COP25) uliofanyika tarehe 02-13 Disemba 2019 nchini Hispania.

Pamoja na kutoa mchango na ushauri katika sayansi ya hali ya hewa kwa ujumbe wa Tanzania ulioshiriki katika Mkutano huo, TMA ilishiriki pia katika mikutano iliyofanyika sambamba na Mkutano huo wa UNFCCC-COP25, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), Dkt. Agnes Kijazi, alishiriki kutoa mada na baadae katika jopo la majadiliano kuhusiana na umuhimu wa kujenga uwezo na kuimarisha huduma za hali ya hewa, hususan katika nchi zinazoendelea sambamba na kuweka msisitizo wa kuhakikisha dunia inaongeza jitihada za kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa katika maeneo ya bahari na yaliyo kandokando ya bahari.

“Kumekuwa na ongezeko la kina cha bahari, ongezeko kubwa la vimbunga kwa upande wa Afrika, mfano kimbunga IDAI kilishosababisha vifo vya mamia ya watu na kuharibu mazao na makazi ya watu katika nchi za Msumbiji, Zimbabwe na Malawi, hii inaonesha kuwa changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa ni halisia, ni vyema tukachukua hatua stahiki sasa”. Alisema Dkt. Kijazi. 

Kwa upande mwingine, Dkt Kijazi alishiriki kutoa mada kuhusiana na masula ya jinsia na changamoto ya mabadiliko ya hali ya hewa. Dkt. Kijazi, alisisitiza kuwa kuna tofauti kubwa ya namnna ambavyo mabadiliko ya hali ya hewa yanawaathiri wanawake, watoto, wazee na wanaume. Wanawake, watoto na wazee wanaathirika zaidi na mabadiliko ya hali ya hewa hasa katika nchi zinazoendelea kutokana na nafasi na shughuli zao katika jamii. Dkt. Kijazi aliitaka jumuiya ya kimataifa kufuata mfano wa Tanzania katika kutoa nafasi kwa wanawake katika nafasi za maamuzi, ambapo Makamu wa Rais wa Tanzania ni mwanamke, Naibu Spika ni mwanamke na akasema vilevile na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa ni mwanamke ambaye ni yeye mwenyewe.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi wa Utafiti na Matumizi kutoka TMA alielezea umuhimu wa kuimarisha uangazi na uboreshaji wa huduma za hali ya Hewa katika bara la Afrika na nchi zinazoendelea pamoja na kushiriki katika jopo la majadiliano kuhusiana na maandalizi ya ripoti ya sita ya tathmini ya mabadiliko ya hali ya hewa duniani, ambapo tayari kuna ripoti maalamu tatu zimetolewa na maandalizi yanaendelea kukamilisha ripoti kuu nne na zinatarajiwa kukamilika mwaka 2022.

Aidha, TMA ilishiriki pia hafla ya WMO ya kusaini ushirikiano na  washirika wa maendeleo katika uboreshaji wa huduma za hali ya hewa (Alliance for Hydromet). Hafla hiyo ilimshirikisha Katibu Mkuu wa WMO, Prof. Petteri Taalas, viongozi mbalimbali wa WMO na viongozi wa Taasisi za Hali ya Hewa-Afrika ikiwemo Malawi, Uganda na Tanzania.

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...