Monday, June 29, 2015

MKUTANO WA SITINI NA SABA WA KAMATI KUU YA UTENDAJI YA SHIRIKA LA HALI YA HEWA DUNIANI (WMO-EXCECUTIVE COUNCIL-67), WAAZIMIA KUBORESHA HUDUMA ZA HALI YA HEWA DUNIANI



Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Utendaji ya Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) katika picha ya pamoja na washiriki wa Mkutano wa Kamati Kuu ya Utendaji ya WMO (WMO-Excecutive Council-67) uliofanyika tarehe 15-17 Juni 2015, Geneva, Uswisi.



Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Agnes Kijazi alikuwa miongoni mwa wajumbe 37 wa Mkutano wa Sitini na Saba wa Kamati Kuu ya Utendaji ya Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO-EC 67) uliofanyika makao makuu ya Shirika hilo kuanzia tarehe 15 hadi 17 Juni, 2015 Geneva nchini Uswisi. Kamati hiyo ina wajumbe 37 wanaowakilisha Nchi Wanachama wa WMO 191. Kati ya wajumbe hao tisa (9) wanatoka Bara la Afrika na kati yao watano (5) ni wanawake wakiwemo wanawake wawili (2) kutoka Bara la Afrika. Mkutano huo wa WMO-EC 67 ni wa kwanza kwa wajumbe wapya waliochaguliwa wakati wa Mkutano Mkuu wa Kumi na Saba wa WMO (WMO-Congress-17) uliofanyika kuanzia tarehe 25 Mei hadi 12 Juni 2015 ukihusisha wajumbe kutoka Nchi Wanachama wa WMO.
Mkutano wa WMO-EC-67 pamoja na masuala mengine ulijadili utekelezaji wa maazimio ya Mkutano Mkuu wa WMO ambayo ni pamoja na uendelezaji Mpango Mkakati wa WMO (WMO Strategic Plan) ambao una dira na vipaumbele vya WMO na Tasisi za Hali ya Hewa  katika kipindi cha miaka minne ijayo (2016-2019). Mpango Mkakati huu unajumuisha utekelezaji wa programu za utoaji wa huduma bora zaidi za hali ya hewa kwa jamii “Global Framework for Climate Services (GFCS)”, programu ya uboreshaji wa vituo vya upimaji wa hali ya hewa na ubadilishanaji wa data za hali ya hewa “WMO Integrated Global Observing System and Information System (WIGOS/WIS), utoaji wa tahadhari za mapema ili kukabiliana na maafa “High impact services for disaster risk reduction”, Uboreshaji wa huduma za usalama na usafiri wa anga “Aviation meteorological services”, uboreshaji wa huduma za hali ya hewa kwa maeneo yenye barafu ya asili Duniani ikiwa ni pamoja na milima mirefu kama Kilimanjaro “Polar and high mountain regions, Kujenga uwezo wa rasilimali watu na vitendea kazi hasa kwa nchi zinazoendelea na visiwa vidogo “Capacity Development” na masuala ya bajeti ya WMO na utawala bora kwa kipindi cha 2015-2019. Maazimio makubwa yaliyofikiwa katika Mkutano huo ni kuhakikisha wajumbe wote wanatimiza majukumu yao kwa weledi ili kuhakikisha huduma za hali ya hewa duniani zinaboreshwa.
Dkt. Agnes Kijazi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ambaye pia ni mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO), katika picha na Wajumbe wa WMO-EC kutoka Afrika wakati wa Mkutano wa sitini na saba wa Kamati Kuu ya Utendaji ya WMO, Geneva, Uswisi. Wa kwanza kulia kwake ni Dkt. Amosi Makarau, Rais wa Afrika anayeshughulikia masuala ya Hali ya Hewa (RA-1);akifuatiwa na Dkt. Linda Makuleni (Afrika ya Kusini), Dkt. Anthony Anuforom (Nigeria) na Dkt. Mamadou Lamine Bah (Guinea); Wa kwanza kushoto kwake ni Bw. Fetene Teshone (Ethiopia), akifuatiwa na Dkt. Daouda Konate (Ivory Coast). Wajumbe wawili kutoka Afrika ambao ni Bw. Richard Philippe (Cameroon) na Bw. Abdalah Mokssit (Morocco) ambaye pia ni Makamu wa Tatu wa Rais wa WMO hawapo katika picha. 


IMETOLEWA NA: MONICA MUTONI-AFISA MAHUSIANO TMA

No comments:

Post a Comment

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...