Tuesday, April 7, 2015

ALIYEKUWA MKURUGENZI MKUU WA MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA AFARIKI DUNIA




Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Dkt. Agnes Kijazi anasikitika kutangaza kifo cha aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu mstaafu Dkt. Mohamed Mhita aliyezaliwa tarehe 17 Februari 1946 na kufariki siku ya  Jumatatu tarehe 06 Aprili 2015 katika hospitali ya Agakhan  jijini Dar es Salaam.
Dkt. Mhita alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa iliyokuwa Idara Kuu ya Hali ya Hewa kwa kipindi cha miaka 8 kuanzia 1992 hadi 1999 na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kwa kipindi cha miaka 9 kuanzia 1999 hadi 2008. Dr. Mhita kwa kushirikiana na uongozi wa iliyokuwa idara Kuu ya Hali ya Hewa alishiriki katika kuishauri Serikali kuhusu kuanzishwa kwa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania kutoka iliyokuwa Idara Kuu ya Hali ya Hewa.
Pamoja na nafasi ya Mkurugenzi Mkuu pia alikuwa Mwakilishi wa kudumu wa Tanzania katika Shirika la Hali ya Hewa Duniani kuanzia mwaka 1992 hadi 2008. Alichaguliwa kuwa Mjumbe katika Baraza Kuu la Shirika la Hali ya Hewa Dunia kuanzia mwaka 1995 hadi 2007. Alichaguliwa  kushika nafasi ya Rais wa Jumuiya ya Hali ya Hewa katika Bara la Afrika (RA 1)  kuanzia mwaka 1998 hadi 2007. Dkt Mhita alikuwa Rais wa ‘Tanzania Meteorological Society’ sambamba na nafasi nyingine nyingi mbalimbali alizoshika ndani na nje ya nchi.
Akielezea baadhi ya mambo makubwa yatakayomfanya Dkt. Mhita aendelee kukumbukwa, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini Dkt. Agnes Kijazi alisema ‘Dkt. Mhita atakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika kuendeleza sayansi ya hali ya hewa hapa nchini, katika Bara la Afrika na Duniani kwa ujumla hususani katika ushiriki wake wa kuianzisha Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini kwa kuandaa dira (vision) na dhamira (mission) ya Mamlaka kwa kipindi cha miaka kumi na tano (15) kuanzia mwaka 2000 hadi 2015’.  
Dkt. Mohamed Mhita ni mmoja kati ya wanasayansi waliokuwa zao la chuo kikuu cha Stolkholm, Sweden ambako alitunukiwa shahada ya hali ya hewa (BSc. Met) mwaka 1977.  Kuanzia mwaka 1981 hadi 1984 alikuwa mafunzoni katika  chuo Kikuu cha Reading, Uingereza ambako alitunikiwa shahada ya uzamivu (PhD). Hapa nchini alipata mafunzo ya Sekondari katika shule za Tanga na Kamrimjee zote zikiwa mkoani Tanga.
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania inajumuika na familia, ndugu, jamaa na marafiki katika kuomboleza msiba huu.
Bwana Alitoa na Bwana Ametwaa Jina lake lihimidiwe.

IMETOLEWA NA: MONICA MUTONI AFISA MAHUSIANO MAMLAKA YA HALI YA HEWA TANZANIA.

1 comment:

  1. Hakika sisi sote ni wa Mwenyezi Mungu, na Hakika kwake ndio marejeo yetu. Mwenyezi Mungu amlaze mahali pema peponi..Amin

    ReplyDelete

Featured Post

DKT. KIJAZI: KIWANGO CHA USAHIHI WA UTABIRI WA MSIMU WA VULI 2019 KIWE CHA JUU ZAIDI.

Mkurugenzi mkuu wa TMA na Makamu wa Tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani Dkt. Agnes Kijazi (katikati mwenye suti nyeusi) waka...